DC abaini mchezo mchafu wa wauguzi

Bagamoyo. Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani, Ahmed Kipozi amesema atawachukulia hatua baadhi ya wahudumu wa Hospitali ya Bagamoyo wanaolalamikiwa na wagonjwa kuwa huwalazimisha kwenda kununua dawa nje wakati zinapatikana hospitalini hapo.
Alisema hayo jana alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa wadau wa afya uliolenga kuzungumzia changamoto mbalimbali zinazoikabili hospitali hiyo ya wilaya.
Kipozi alikiri kuwapo malalamiko ya mara kwa mara kuhusu wananchi kunyimwa dawa hospitalini hapo na baadhi ya wahudumu ambao huwataka kwenda kununua kwenye duka moja la jirani na eneo la hospitali.
Alisema wilaya imefanyia kazi malalamiko na kubaini kuna udhaifu wa kiutendaji unaowahusu baadhi ya wahudumu ambao alisema wameamua kuchafua sifa ya hospitali hiyo na Serikali. Alisema hatakubali kuona hali hiyo ikiendelea na kwamba umefika wakati wa kuchukua hatua stahili dhidi ya wahusika wote.
“Kamwe hatuwezi kuwavumilia tena wahudumu wenye tabia hii. Wamekuwa kero kwa wakazi wa wilaya na wale wanaotoka nje ya wilaya wanaofika kupata huduma za afya katika hospitali yetu. Mimi binafsi nimekuwa shuhuda wa haya ninayoeleza na bahati nzuri leo hii wadau pia wanazungumzia hilo,” alisema Kipozi.
ADVERTISEMENT
Kaimu mganga mkuu wa hospitali hiyo, Kusekwa Mashaka alisema kinachochangia hospitali nyingi za Serikali kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi ni kutokana na urasimu wa utoaji wa vibali vya kuchukulia dawa unaofanywa na baadhi ya watendaji wa Bohari ya Dawa (MSD).
Alisema hospitali yake hushindwa kununua dawa nje ya utaratibu wa kawaida wanapokuwa wamepungukiwa.
Daktari huyo ameongeza kuwa kama huduma ya afya katika Serikali ya wilaya ya Bagamoyo zikiboreka basi malalamiko ya wakazi wa wilaya hiyo yatapungua .
Aidha kwa upande wake mratibu wa asasi ya Uhakika kituo cha ushauri nasaha UKUN-PHI Charles Njonjele ambao ndio walioratibu mkutano huo chini ya ufadhili wa shirika la Action Aid alisema lengo la mkutano huo ni kujadili changamoto na matatizo mbalimbali yanayoikabili sekta ya afya wilayani humo na pia kupata majawabu ya nini kifanyike kuzitatua ama kuzipunguza kabisa.
“Lengo kubwa hasa ilikuwa ni kujadili changamoto mbalimbali katika sekta ya afya wialayani hapa na zaidi tulilenga kujadili changamoto zlizopo hospitali ya wilaya haswa suala zima la utoaji wa huduma na kutafuta mbinu mbalimbali za kukabiliana na changamoto hizo, ili jamii iweze kuamini hudumu wanazipatiwa, kama dawa hakuna waamini hivyo na kama zipo basi zitolewe kwa wagonjwa na sio kuleta usumbufu kwao ”alisema Njonjele.
Powered by Blogger.