Mchakato Uchaguzi Serikali za Mitaa umevurug

Mchakato Uchaguzi Serikali za Mitaa umevurugwa0

Share

Zikiwa zimebakia siku 10 tu kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, vimejitokeza vioja, vitimbi na matukio mengine mengi ya kuonyesha kwamba uchaguzi huo huenda hautakuwa huru na wa haki. Yote hayo yanatokea baada ya Serikali kutangaza kuanza kwa mchakato wa uchaguzi huo muhimu kwa wananchi kujiandikisha kuanzia Novemba 21 hadi 29, mwaka huu. Serikali ilishikwa na kigugumizi cha muda mrefu kabla haijaweka utaratibu huo, hivyo kusababisha wasiwasi mkubwa kwa wananchi.
Mchakato huo ulianza kwa wananchi kujiandikisha ili kupiga kura Desemba 14, mwaka huu. Kwa utaratibu wa kawaida, muda huo wa siku saba kujiandikisha ulikuwa mfupi mno. Muda huo ulikuwa hautoshi kwa watu wengi kujiandikisha kutokana na kubanwa na shughuli za kazi na mazingira magumu wanayoishi.
Ndiyo maana yaliibuka malalamiko mengi kutoka kila kona kwamba Serikali pengine ilikuwa imedhamiria kukinufaisha chama tawala ambacho kina mifumo ya kuwafikia wafuasi wake katika muda mfupi, tofauti na vyama vya upinzani.
Kampeni za uchaguzi huo zilianza siku nne zilizopita na zitaendelea hadi Desemba 13, siku moja kabla ya kufanyika kwa uchaguzi huo. Lakini wakati mchakato huo ukiendelea na wanachama wa vyama vya siasa wakijitokeza kugombea nafasi mbalimbali, yametokea matukio mengi ambayo yamedhihirisha kwamba siyo tu kuna ubabaishaji mkubwa katika uendeshaji wa mchakato huo, bali pia kwamba Serikali haikuwa imefanya matayarisho ya kutosha au kuweka mazingira mazuri ya kufanyika kwa uchaguzi huo muhimu. Jambo la kusikitisha ni kwamba Serikali imebakia kuwa mtazamaji badala ya kuhakikisha kwamba kasoro zinazojitokeza zinapewa suluhisho stahiki na kwa wakati.
Wananchi wamebakia kujiuliza kama kasoro hizo zinatokea kwa bahati mbaya au kwa makusudi. Mbali na vurugu zinazotokana na waratibu wa uchaguzi huo kukiuka taratibu, kanuni na miongozo iliyowekwa, umejitokeza utamaduni wa watendaji wa serikali za mitaa na kata katika maeneo mengi nchini kuegemea upande mmoja.
Moja ya mikakati inayoharibu mchakato huo ni wagombea wa upinzani kuwekewa pingamizi, huku kamati za rufaa zikionekana wazi kutoa uamuzi unaopendelea baadhi ya wagombea au kukataa kabisa kusikiliza rufani hizo.
Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi) imetoa miongozo na kanuni ambazo kinadharia zinaonekana zinaweza kuendesha mchakato huo kwa haki. Hata hivyo, ni vyema kutambua kuwa, kuweka kanuni na miongozo ni jambo jema, lakini suala la msingi ni usimamizi na utekelezaji wake. Vinginevyo, hakuna sababu ya kuwapo msululu wa watendaji na kamati mbalimbali za kusimamia mchakato huo, kama hakuna mifumo inayowezesha wagombea wote kutendewa haki bila ubaguzi wowote, kwa maana ya kuangalia vyama wanavyotoka.
Sisi tunadhani kwamba hali hiyo ni matokeo ya Serikali kutojiandaa vya kutosha au kutokuwa na utashi. Uchaguzi umeahirishwa katika baadhi ya sehemu kutokana na ugomvi wa mipaka, huku katika sehemu nyingine vurugu zimetokea kutokana na mamlaka husika kushindwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya kanuni na miongozo.
Ni wajibu wa Serikali kuondoa kasoro hizo na nyingine nyingi katika siku 10 zilizobaki kabla ya uchaguzi huo. Vinginevyo ni kuweka mazingira ya uchaguzi huo kutokuwa huru na wa haki kwa kuruhusu matatizo ambayo yanaweza kuepukika.
      chanzo;mwananchi

Powered by Blogger.