Juhudi za kuisaka ndege AirBus A320 zasitishwa.

Ndege AirBus 320
Juhudi zinazoongozwa na jeshi la majini za kusaka ndege ya abiria iliyokuwa na watu takriban 162 zimeahirishwa wakati wa usiku. Ndege hiyo aiya ya Airbus A320 ilipotea Jumapili asubuhi, kwa saa za  Asia ikitokea Surabaya, Indonesia kuelekea Singapore.
Wengi waliokuwemo ndani ya ndege walikuwa raia wa Indonesia. Ndege hiyo ya Indonesia AirAsia 8501 iliondoka Surabaya kwenda uwanja wa ndege wa Changi nchini Singapore ikikadiriwa kutumia masaa mawili ikivuka bahari ya Java.
Mkurugenzi mkuu wa masuala ya anga katika wizara ya usafiri ya Indonesia Djoko Atmojo amewaambia waandishi wa habari kuwa mawasiliano ya  mwisho kutoka kwa mmoja wa wafanyakazi wa ndege hiyo lilikuwa saa 12:12 asubuhi kwa saa za ndani na kulikuwa hakuna ishara yoyote ya matatizo  iliyopokelewa.
Anasema rubani alieleza kwamba alikuwa anajaribu kuepuka mawingu na alikuwa anakwenda upande wa kushoto badala ya njia ya kawaida na aliomba ruhusa ya kuruka mita 1800 juu zaidi.
Dakika chache baadae ndege hiyo ilipotea kwenye rada  na hakuna mawasiliano yaliyopatikana tena.
Kulikuwa na radi na umeme  vilivyoripotiwa huku upepo mkali ukivuma.
Maafisa wa usalama wa Indonesia wanasema mara ya mwisho kuonekana ndege hiyo ilikuwa karibu na  nusu ya safari yake, kwenye kisiwa cha Belitung ambacho katika miaka ya hivi karibuni kimekuwa sehemu ya kutembelewa na watalii.
Waziri wa usafiri Ignasius Jonan amesema timu ya kijeshi na  uokozi kutoka nchini kwake pamoja na Singapore zilishiriki katika operesheni za awali.
Amesema meli zote katika eneo hilo zimetakiwa kutoa maelezo yoyote yanayoweza kufahamisha kuhusu kupotea  kwa ndege hiyo na zimeombwa kujiandaa kutoa msaada utakapohitajika.
Ndege hiyo yenye miaka sita mara ya mwisho ilifanyiwa matengenezo novemba 16.
Powered by Blogger.