Safari ya Ukawa kwenda Ikulu 2015

Fukuto la kumpata mgombea wa kiti cha urais kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 kwa tiketi ya Umoja

Dar es Salaam. Fukuto la kumpata mgombea wa kiti cha urais kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 kwa tiketi ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), linazidi kupamba moto huku ikielezwa kuwa jina la mgombea litatajwa kabla ya Mei mwakani.
Hatua hiyo inatarajiwa kufikiwa baada ya vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD vinavyounda Ukawa kukubaliana njia ya kumpata kiongozi huyo.
Kwa mujibu wa Utafiti wa Taasisi ya Twaweza uliotolewa Novemba mwaka huu, kama mgombea hatapatikana nje ya umoja huo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa ndiye anayepewa nafasi zaidi ya kupeperusha bendera.
Pia, iwapo Chadema watatoa mgombea urais, mwelekeo unaonyesha kuwa CUF italazimika kutoa mgombea mwenza kutokana na nguvu na ushawishi ilionao upande wa Zanzibar.
Tayari Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia ameshatangaza kuwania ubunge katika Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro na ikielezwa kwamba Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba ananyemelea jimbo moja la ubunge kati ya Dar es Salaam au Tabora.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya vyama hivyo, mpaka sasa hakuna ratiba zozote za uchaguzi zilizoandaliwa, ingawa kampeni za uchaguzi zinaendelea kufanywa chini kwa chini.
Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF, Abdul Kambaya alisema ratiba ya chama hicho inatarajiwa kuwa tayari kuanzia Februari mwakani, ingawa mambo mengine yatategemea makubaliano na wanachama wa Ukawa.
Kambaya alisema kuwa anaamini mchakato wa suala hilo kwa upande wa Ukawa utakuwa umekamilika kabla ya Mei mwakani.
Hata hivyo, Kambaya alisema kuwa haitakuwa jambo la ajabu iwapo Ukawa wakasimamisha mgombea asiyekuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa kwa kuwa wapo baadhi ya watu wanaowaunga mkono lakini siyo wanasiasa.
Iwapo jambo hilo litatokea, itabidi mtu huyo asajiliwe kwenye chama kimoja kama itakavyopendekezwa kwa kuwa mgombea wa urais lazima awe mwanachama wa chama cha siasa.
Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro, alisema njia pekee ya Ukawa kumpata mgombea wake kwa njia ya amani ni kuwa vyama vyote kukaa chini na kuweka vigezo vya mgombea vinavyohitajika.
Alisema baada ya kukubaliana vigezo hivyo, ndipo watakapoangalia ni mgombea wa chama gani anasifa nyingi kati ya zote zilizopendekezwa.
“Ukisema CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi au NLD kila mmoja alete mgombea wake, hilo jambo haliwezekani. Kinachotakiwa ni kuangalia mtu anamvuto kiasi gani au anakubalika kiasi gani,” alisema Mtatiro.
Baada ya kila vyama vyote kumpata mgombea wanayempendekeza, ndipo kila chama kitakwenda kumnadi kwa wanachama wake na atakapokubalika ndipo Ukawa itamtembeza mikoani
Kuhusu muda wa kumchagua mgombea, Mtatiro alisema ni vyema zoezi hilo likafanyika mapema kwa ajili ya mgombea kujiandaa na pia kufahamika kwa wananchi.
“Urais siyo jambo la kushtukiza, mgombea ateuliwe mapema, Ukawa ina wagombea wengi wenye sifa ukilinganisha na CCM kwa hiyo ni vyema akafahamika mapema,” aliongeza.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika alisema kuwa ratiba ya uchaguzi ya chama hicho itategemea makubaliano na wanachama wa Ukawa.
“Zingatia pia kwamba sasa kuna makubaliano ya ushirikiano wa Ukawa, hivyo tutaeleza ratiba nzima ya mchakato wakati mwafaka ukiwadia,” alisema Mnyika.
Aliongeza: “Kwa sasa kitu kinachopewa umuhimu ni kuwahamasisha wananchi kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura na kujiandaa kwa ajili ya kura ya maoni ya Katiba Mpya.”
Hata hivyo, alisema kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho, ratiba inapangwa mwakani na Kamati Kuu itakapokaa katika siku itakayoandaliwa na sekretarieti.
Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ubungo aliongeza kuwa kwa mujibu wa katiba ya Chadema, Kamati Kuu ya chama inafanya utafiti na kupendekeza kwa Baraza Kuu, ambapo baraza hilo linafanya uteuzi wa awali na kupendekeza kwa mkutano mkuu.
Kwa upande wa Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema chama bado kinatafakari Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika hivi karibuni na kwamba ratiba hiyo bado haijawekwa wazi.
Kafulila alipendekeza
Mapema mwezi huu, Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila alijitokeza hadharani na kumpigia debe Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kuwa ndiye anayefaa kupeperusha bendera ya umoja huo.
Kafulila alisema, Dk Slaa ambaye katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 aliitikisa CCM, anafaa kwa sababu ana sifa ya ziada ya kuwa na mvuto.
Hata hivyo, mwananchi aliyejitambulisha kwa jina moja la Mkoba alionya kuwa mapendekezo hayo yanaweza kuwa na madhara kwa Ukawa kwa kuwa kila chama kinaamini mgombea wake anafaa zaidi.
“Kumpendekeza mtu tu kunaweza kuwagawa wapiga kura, CUF wakataka kiongozi wao na Chadema pia wakataka wao. Mgombea ni lazima apendekezwe na kupitishwa na siyo kuchaguliwa tu. Pia, siku ya kufanya hivyo inapasa mchakato uwe wa wazi na wananchi wote wahusikie,” alisema Mkoba.
Mkazi wa Kinondoni, Musa Hussein alisema Ukawa wanapaswa kufanya utafiti wa kina wa kujua sifa na nguvu alizonazo kila mgombea kwa wananchi na nafasi aliyonayo ya kumshinda mgombea wa CCM.
Powered by Blogger.