Mfanyabiashara ashikiliwa kwa kutishia kuuwa wafanyakazi wa kampuni ya ukandarasi ya Hema Tec mkoani Rukwa.

Katika hali isiyokuwa ya kawaida mfanyabiashara mmoja wa maeneo ya mazwi kwenye manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa, amewatishia kuwapiga risasi wafanyakazi wa kampuni ya ukandarasi ya Hema Tec, inayotekeleza mradi wa kuchimba mtaro wa kupitishia mkongo wa taifa wa mawasiliano mjini humo, kwa kukataa kutii amri yake ya kuwakataza kuchimba kwenye eneo lake, na wafanyakazi hao kutimua mbio kunusuru maisha yao.
Kaimu kamanda wa polisi wa mkoa wa Rukwa kamishna msaidizi wa polisi Lewins Rwegasira, amesema wanamshikilia mtuhumiwa huyo ambaye amemtaja kuwa Juma Mussa mkazi wa maeneo ya mazwi, kwa tuhuma za kutishia kuuwa kwa bastola aina ya Browning yenye namba a 729321, na kuwakimbiza wafanyakazi wa kampuni hiyo ya Hema Tec kwa gari lake, ambao waliamua kukimbia baada ya kuona ameingia ndani na kutoka na bastola hiyo.
 
Akiongea na ITV msemaji wa kampuni hiyo ya ukandarasi ya Hema Tec Bw Abdallah Seleman, amesema mtuhumiwa huyo kwanza aliwakataza wafanyakazi hao wasichimbe mtaro kwenye eneo hilo, lakini wao wakawaambia waendelee na kazi kwani wanaitekeleza kwa mujibu wa ramani iliyotolewa na manispaa ya Sumbawanga, na ndipo alipoamua kuchukua bastola yake baada ya kuona ameshindwa kupambana na mmojawao aliyemtaja kwa jina la Daud William.
 
Powered by Blogger.