Sumaye: Chagueni kiongozi mzalendo asiye na makundi

Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye
Mbeya. Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye amewataka Watanzania kuchagua kiongozi mzalendo asiye na makundi atakayewainua kwa kadri inavyowezekana ili wawe na maisha bora.
Sumaye alisema hayo jana kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya katika tamasha la kuliombea Taifa na kusherehekea Sikukuu ya Krismasi.
“Watanzania, mwakani tunayo nafasi ya kumuweka kiongozi wa aina hiyo. Hivi sasa kuna tatizo la kuporomoka kwa uzalendo katika nchi yetu.
“Watu wanaanza kuthamini masilahi binafsi na hili limewakumba viongozi wengi wa umma hadi wanasiasa,” alisema na kuongeza kuwa upotevu wa uzalendo wa kweli unasababisha hasara nyingi kwa mali za nchi hasa maliasili.
“Mauaji ya wanyama wetu kama tembo, faru, utoroshaji wa rasilimali zetu, uharibifu wa misitu, mikataba isiyofaidisha wananchi, vyote hivi ni matunda ya watu kukosa uzalendo wa dhati,” alisema.
Alisema watu huangalia zaidi kujitajirisha hata kama ni kwa gharama kubwa kwa nchi.
“Hili ni jambo la hatari sana kwa amani ya nchi likiachiwa kuota mizizi, hivyo ni vyema kiongozi tutakayemtafuta mwakani awe mzalendo wa dhati adhibiti hali hiyo,” alisema.
Sumaye anayetajwa kuutaka urais mwakani, alisema nchi inahitaji kiongozi mwenye upeo, kuielewa nchi barabara, kuwaelewa Watanzania vyema na matatizo yao yawe yanamgusa moyoni mwake.
ADVERTISEMENT
“Kiongozi huyo lazima aelewe Watanzania wanataka nini, yeye anataka kutupeleka wapi na anatufikishaje huko. Asiwe kiongozi wa kutuburuza anavyotaka au asiyejali yanayotupata ambayo yana maumivu kwetu,” alisema Sumaye.
Huku akisikilizwa na waumini hasa wa madhehebu ya dini ya Kikristo, Sumaye alisema utawala wa sheria na demokrasia ni muhimu.
Alisema nchi nyingi zimejikuta katika machafuko kwa sababu kiongozi wake wakati mwingine huweka katiba na sheria kando na kutawala kwa imla kadiri anavyoona inafaa.
“Utaratibu unaomweka madarakani kiongozi ni vyema akauheshimu na kuutii. Tunahitaji atakayeheshimu katiba ya nchi na sheria zinazowekwa mara kwa mara kwa masilahi ya umma,” alisema.
Sumaye alisema kiongozi anayefaa kuongoza Tanzania ni lazima awe tayari kuilinda na kuikuza demokrasia ya vyama vingi ambayo imeanzishwa kwa masilahi ya wananchi.
“Ili aina hii ya utawala iwasaidie wananchi ni lazima vyama vya upinzani viwe na nguvu ya kuwa changamoto kwa chama tawala, hiyo ndiyo maana na faida ya demokrasia ya vyama vingi,” alisema na kuongeza kuwa:
“Kiongozi mkuu wa nchi hawezi kuongoza Serikali peke yake bila wasaidizi kama mawaziri, wakuu wa vyombo vya dola, makatibu wakuu, wakuu wa mikoa na wilaya, ni wajibu wake kuwaweka watakaomsaidia na wanaoelewa majukumu yao vyema kwa wananchi.
Sumaye alisema kiongozi stahiki ni lazima awe na uwezo wa kuweka madarakani serikali itakayowajibika kwa umma na kusimamia masilahi yake.
Powered by Blogger.