Hakimu ajitoa kesi ya jumuiya ya Uamsho

Baadhi ya watuhumiwa wa Ugaidi wakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu, jijini Dar es Salaa. Picha na Tausi Ali

Dar es Salaam.Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Hellen Liwa amejitoa kusikiliza kesi ya ugaidi inayowakabili viongozi 23 wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI).
Ni baada ya wakili wa washtakiwa hao wa ugaidi, Abubakar Salim  kumtaka ajitoe kuisikiliza kesi hiyo ili iweze kupangiwa hakimu mwingine ambaye atatoa uamuzi juu ya hoja zao walizozitoa mahakamani hapo Septemba 19,2014.
Salim aliiambia mahakama kuwa baada ya kushauriana na wateja wao na uamuzi uliotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu, Dk Fauzi Twaib  wakaona kuwa ni ukweli kuwa Hakimu Liwa alikwisha toa uamuzi wake juu ya hoja zao Oktoba Mosi, 2014 kuwa mahakama hiyo ya kisutu haina mamlaka ya kuzikiliza.
Alidai Mahakama Kuu katika uamuzi wake uliotolewa na Jaji Twaib umeelekeza kuwa Mahakama ya  Kisutu  inayo mamlaka ya kuzisikiliza hoja za washtakiwa hao wa ugaidi  na hata kuzitolea uamuzi.
“Mahakama Kuu imeelekeza mawakili  wa upande wa utetezi  kama tutakuwa na hoja mpya ama za  zile za awali tuzitoe kwenye mahakama hii ya Kisutu  ili ziweze kutolewa maamuzi hivyo naona ni bora ujitoe tupate neno kutoka kwa hakimu mwingine.”Alisisitiza kusema wakili huyo mahakamani hapo.
Wakili wa Serikali Mkuu, Benard Kongola  alimuomba Hakimu Liwa asijitoe katika  kuisikiliza kesi kwa madai sababu zilizotolewa na upande wa utetezi za kumtaka ajitoe hazina msingi.
Kongola alieleza kuwa uamuzi uliotolewa na Jaji Twaib  aliamuru utekelezaji wa hoja za upande wa utetezi katika kesi hii ya ugaidi zisikilizwe na kutolewa uamuzi katika Mahakama ya Kisutu.
“Tukiendekeza hii tabia tutamaliza  mahakimu wote wa mahakama hii tunasisitiza upande wa utetezi utoe sababu za msingi za wewe kujitoa.”Alisema Kongola.
Akijibu hoja hizo, Wakili Salim alieleza kuwa ili haki ionekane inatendeka wewe Hakimu Liwa ujitoe ili hakimu mwingine atoe maamuzi wa hoja zetu.  
Hakimu Liwa alisema ni kweli nilikwisha toa uamuzi wangu juu ya maombi ya washtakiwa lakini Mahakama Kuu imeona kivingine kuwa sijatumia mamlaka yangu vizuri nakubaliana na uamuzi huo.
Lakini uamuzi huo  wa Jaji Twaib haukufafanua nini kifanyike, umetuacha hoi, ila  alitoa angalizo kuwa ushahidi wa kesi hauwezi kutoka hewani na kwamba maelezo yaliyomo katika hati ya mashtaka ya kesi hiyo yapo sahihi.
“Kitu ambacho hata mimi nilikuwa nakishangaa ni hii hati ya mashtaka kuletwa Tanzania Bara badala ya Visiwani, lakini nilipoisoma sheria ya ugaidi nikabaini mtu anaweza kushtakiwa mahali popote.” Alisema Hakimu Liwa.
Alisisitiza kuwa kwa mujibu wa sheria Mahakama Kuu ndiyo yenye uwezo wa kuisikiliza kesi hii na siyo mahakama ya Kisutu hivyo yeye hawezi kusema kitu labda kesi ingekuwa imefikia kwenye mwenendo wa uhamishaji shauri  (Committal Preceding).
Hatua hiyo inafikiwa  baada ya upelelezi wa kesi  kukamilika inahamishwa  kutoka mahakama ya Kisutu kwenda Mahakama Kuu ambayo inamlaka ya kusikiliza kesi hizo.
“Mimi nimejifunza kitu hapa, kuwa mimi najua nini na wenzangu wanajua nini hivyo siwezi kuendelea na kesii haitakuwa haki  najitoa.”Aliongeza kusema Hakimu Liwa na akajitoa na kuiahirisha hadi Januari 13,2015 ili ipangwe kwa  hakimu mwingine.
Powered by Blogger.