Wajisaidia vichakani kwa kukosa choo



Moshi. Kituo cha kulelea watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu cha Global Vision, kilichopo Chekereni Wilaya ya Moshi, Kilimanjaro kinakabiliwa na ukosefu wa choo hali inayosababisha watoto kujisaidia vichakani.
Mlezi wa kituo hicho Anastasia Peter alisema alipopokea msaada na magodoro kutoka kwa wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco). Alisema hali hiyo inasababisha watoto hao kupata magonjwa ya mlipuko mara kwa mara.
Peter aliitaka Serikali kutenga fungu kwa ajili ya kuvisaidia vituo vya kulelea watoto vinavyomilikiwa na watu binafsi.
Alisema hiyo itwasidia kuwajengea uwezo badala ya kuwaachia mzigo huo wamiliki peke yao. Kaimu Meneja wa Tanesco, mkoani Kilimanjaro Mathias Solongo alisema msaada huo umetolewa ili kukabiliana na changamoto walizonazo.
Alisema wafanyakazi hao wametoa Sh5 milioni kwa ajili ya kununua magodoro na chakula na wakiahidi kujenga choo kituoni hapo.
Mmiliki wa kituo hicho, Mchungaji Saimon Sori alisema msaada huo utaondoa tatizo la muda mrefu kituoni hapo watoto kulala kitanda kimoja na wengine wakitandika maboksi sakafuni.
Sori alisema mashirika mengine yaige mfano huo wa kutembelea watu wenye uhitaji ili wawasaidie na watabarikiwa na Mungu.
Powered by Blogger.