Raia 77 wa Uchina washtakiwa Kenya

Wizi wa mitandaoni
Polisi nchini Kenya wamewafikisha mahakamani raiya 77 wa Uchina kwa kushukiwa kushiriki udukuzi wa mawasiliano na ulanguzi wa fedha.
Washukiwa hao wamewekwa rumande kwa siku tano zaidi ili kutoa nafasi kwa polisi kufanya uchunguzi wa kina.
Wakili wa washukiwa hao anataka waachiliwe kwa dhamana na ombi lake litasikizwa kesho katika mahakama kuu mjii Nairobi.
Washukiwa hao 77 walikamatwa katika nyumba moja kwenye mtaa wa kifahari wa Runda jijini Nairobi siku ya Jumatatu na hapo jana na wanadaiwa kushiriki katika vitendo vya udukuzi na ulanguzi wa fedha.
Upande wa mashtaka uliomba mahakama muda zaidi kuwachunguza washukiwa hao.
Hata hivyo wakili wa washukiwa hao Tom Wachakana aliishawishi mahakama kusikiza ombi lake kutaka washukiwa waachiliwe kwa dhamana.
Wakati maafisa wa polisi walipovamiwa makazi ya washukiwa hao walipata mitambo ya teknolojia ya hali ya juu inayodhaniwa inatumika kufanya ujanja katika mitandao.
Mbali na maafisa wa polisi, wakuu katika wizara za mambo ya nje na habari na mawasiliano walihusishwa katika msakao huo. Afisa katika ubalozi wa Uchina mjini Nairobi ambaye hakutaka kutajwa aliiambia BBC kuwa
watashirikiana na serikali ya Kenya inayochunguza asili ya raia hao katika kuangalia stakabadhi zao za usafiri.
Washukiwa hao wamekamwatwa wakati kampuni nyingi za Kichina zimewekeza katika biashara hasa katika sekta ya ujenzi.
Kadhalika serikali ya Kenya imetia saini mikataba mingi na wachina huku baadhi yao wakihusisha katika miradi ya serikali hususan katika taasisi za elimu ya juu.