SIRI YA OMBI LINALOJIBIWA



 














Anatoli Levitini, mwandishi na mwanahistoria wa Kirusi, alitumia miaka yake mingi katika Gulag ya Siberia, ambako dua zilizotolewa kwa Mungu zilionekana kana kwamba zimeganda ardhini. Lakini alirudi akiwa mzima kiroho. "Mwujiza mkuu kuliko yote ni maombi," aliandika. "Yanipasa tu kumgeukia Mungu kimawazo na mara moja naisikia nguvu inayoingia ndani yangu kutoka mahali fulani, inaingia katika roho yangu, na mwili wangu wote. Je! hicho ni kitu gani? Je, naweza kuipata wapi hiyo nguvu inifanyayo mimi kuwa mtu mpya na kuniokoa mimi, niliye mzee duni sana, niliyechoka na maisha, ambayo itaniinua juu ya dunia hii? Inatoka nje yangu - wala hakuna nguvu yo yote ulimwenguni humu ambyo ingeweza kuipinga."
Katika mwongozo huu tunaona jinsi maombi yanavyotusaidia kujenga uhusiano wenye nguvu zaidi pamoja na maisha ya Kikristo yenye nguvu.
1. Kuzungumza Na Mungu
Je, tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu anatusikia tunapoomba?
"Ndipo mtaniita mimi na kwenda KUNIOMBA, nami NITA SIKILIZA. Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote." - Yeremia 29:12,13.
Je, ni uthibitisho gani aliotoa Yesu kuonyesha kwamba atasikia na kujibu maombi yetu?
"Basi nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, na mlango utafunguliwa kwenu." - Luka 11:9.
Maombi ni maongezi ya pande mbili. Hii ndiyo maana Yesu anaahidi anasema:
"Tazama nasimama mlangoni, nabisha. Mtu ye yote akiisikia sauti yangu, na kuufungua malngo, nitaingia na kula pamoja naye, na yeye pamoja nami." - Ufunuo 3:20.
Kwa jinsi gani inawezekana kwetu kuketi na kuwa na maongezi mazuri wakati wa chakula cha jioni pamoja na Kristo? Kwanza, kwa kumwambia kila kitu tulicho nacho moyoni mwetu kwa njia ya maombi. Pili, kwa kusikiliza kwa makini. Tunapotafakari wakati wa maombi, Mungu anaweza kuongea nasi moja kwa moja. Na tunapolisoma Neno la Mungu kwa roho ya ibada, Mungu ataweza kuongea nasi kupitia katika kurasa zake.
Maombi yanaweza kuwa njia ya maisha kwa Mkristo.
"OMBENI BILA KUKOMA; shukuruni kwa kila jambo, maana hayo ndiyo mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu." - 1 Wathesalonike 5:16-18.
Je! sisi tunawezaje "kuomba bila kukoma?" Je, yatupasa kupiga magoti wakati wote au kurudia-rudia kusema maneno ya kumsifu au kutoa dua? La, hasha. Lakini tunapaswa kuishi karibu sana na Yesu kiasi cha kujisikia huru kusema naye wakati wo wote, na mahali po pote.
"Tukiwa katika makundi ya watu mitaani, katika shughuli ya kibiashara, tunaweza kutoa dua yetu kwa Mungu na kumsihi atupe uongozi wake… Daima tungeacha wazi mlango wa moyo wetu na kuuacha mwaliko wetu ukipanda juu ili Yesu aweze kuja moyoni mwetu na kukaa humo kama mgeni wetu wa mbinguni." - Steps to Christ, uk. 99.
Mojawapo ya njia bora sana ili kujenga uhusiano huo wa karibu sana ni kujifunza kutafakari wakati tunapoomba.
"Kutafakari kwangu na kumpendeze yeye, mimi ninapomfurahia BWANA." -Zaburi 104:34.
Unapoomba usiharakishe tu kupitia orodha ya mambo unayotaka. Ngojea. Sikiliza. Kutafakari kidogo ukiwa katika maombi kunaweza kuuboresha sana uhusiano wako na Mungu.
"Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi." - Yakobo 4:8.
Kadri sisi tunavyozidi kumkaribia sana Yesu ndivyo kadri tunavyoweza kuonja kuwako kwake. Basi wewe unapaswa kuwa katika umbali wa kuweza kuongea na Yesu, wala usiwe na wasi wasi juu ya kusema maneno yaliyo sahihi. Ongea tu naye kwa unyofu wa moyo na bila kuficha kitu. Ongea juu ya kila kitu. Yeye amepitia maumivu makali sana ya kifo kile chenyewe ili apate kuwa Msiri wako.
2. Jinsi Ya Kuomba
Tunapoingia katika maombi, tunaweza kupenda kufuata muhtasari wa sala ya Bwana, sala ya mfano ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuitikia ombi lao hili:
Tufundishe sisi kuomba.
"Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tulivyowasamehe wadeni wetu. Wala usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu, kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina" - (Mathayo 6:9-13).
Kulingana na mfano huo ambao Yesu aliutoa katika sala yake, sisi tunatakiwa kumwendea Mungu kama Baba yetu aliye mbinguni. Tumwombe kwamba mapenzi yake yatawale mioyo yetu kama vile mapenzi yake yanavyotawala katika mbingu yote. Tunamtafuta ili atupatie mahitaji yetu ya kimwili, msamaha wake, kwa ajili ya kuwa na roho ya kuwasamehe wengine.
Kumbukeni ya kwamba uwezo wetu wa kuipinga dhambi unatoka kwa Mungu. Sala ya Kristo inahitimisha kwa maneno ya sifa kwake.
Safari nyingine Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kumwomba Baba "kwa jina langu" (Yohana 16:23) - yaani, kuomba kulingana na kanuni zake Yesu. Hii ndiyo maana Wakristo kwa kawaida hufunga sala zao kwa maneno haya: "Katika jina la Yesu, Amina." Amen (amina) ni neno la Kiebrania limaanishalo "Na iwe hivyo".
Japokuwa sala ya Bwana inatoa mwongozo juu ya mambo tunayotakiwa kuyaomba na jinsi ya kutunga sala, mawasiliano yetu na Mungu yanakuwa bora sana kama yanatoka moyoni mwetu kwa hiari.
Tunaweza kuomba juu ya kila kitu. Mungu anataka tumwombe msamaha kwa dhambi zetu (1Yohana 1:9), tumwombe atuongezee imani (Marko 9:24), tumwombe uponyaji wa maumivu na magonjwa yetu (Yakobo 5:15), na kumwagiwa kwa Roho (Zakaria 10:1). Yesu anatuthibitishia kwamba tunaweza kumpelekea yeye mahitaji yetu yote, pamoja na mashaka yetu; mno kuweza kumwomba.
("Mwekeeni matatizo yenu yote, maana yeye anawatunzeni") - 1 Petro 5:7.
Mwokozi wetu anapendezwa na mambo yo yote madogo yahusuyo maisha yetu. Moyo wake huchangamka wakati inapomwendea mioyo yetu kwa upendo na imani.
3. Maombi Ya Faragha
Wengi wetu tunayo mambo fulani ambayo tunasita kuwaambia hata marafiki zetu wa karibu sana. Kwa hiyo, Mungu anatualika sisi kuutua mzigo huo katika maombi yetu ya faragha: tukiwa kila mmoja peke yake na yeye. Si kwamba yeye anahitaji maelezo yote. Mwenyezi anajua vizuri sana kuliko sisi tunavyojua, makusudi yetu yaliyojificha moyoni mwetu, na chuki zetu zilizojificha ndani. Lakini tunahitaji kuifunua mioyo yetu kwake yeye atujuaye mpaka ndani kabisa, na atupendaye milele. Uponyaji unaweza kuanza Yesu anapoweza kuyagusa majeraha yetu.
Tuombapo, Yesu, Kuhani wetu Mkuu, yu karibu nasi kutusaidia:
"Tunaye mmoja ALIYEJARIBIWA KWA KILA NJIA, KAMA SISI TUNAVYOJARIBIWA -lakini alikuwa hana dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupate kupokea rehema na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji" - (Waebrania 4:15,16).
Je, una wasi wasi, mfadhaiko, hatia? Weka hayo mbele zake Bwana. Ndipo yeye anaweza kukidhi kila hitaji tulilo nalo.
Je, ni lazima tuwe na mahali maalumu pa maombi hayo ya faragha?
"wewe unaposali, ingia katika chumba chako, funga mlango na kumwomba Baba yako, ambaye.. atakujazi." - Mathayo 6:6.
Zaidi ya kuomba wakati wa kutembea mitaani, kufanya kazi, au kufurahia mkutano fulani, kila Mkristo angekuwa na muda fulani uliotengwa kila siku kwa maombi yake yeye peke yake pamoja na kujifunza Biblia. Tunza miadi yako ya kila siku na Mungu wako wakati unapokuwa mchangamfu sana na wakati unapokuwa makini sana.
4. Maombi Ya Hadhara
Kujiunga pamoja na wengine katika maombi huwaunganisha watu kwa kifungo maalum na kukaribisha uweza wa Mungu kwa njia ya pekee.
"Kwa kuwa wawili au watatu wanapokusanyika pamoja katika jina langu, nipo pamoja nao pale." - Mathayo 18:20.
Mojawapo ya mambo makuu kuliko yote tuwezayo kufanya sisi kama familia ni kukuza maisha ya maombi ya pamoja. Waonyesheni watoto kwamba tunaweza kupeleka mahitaji yetu kwake moja kwa moja. Watakuwa na msisimko juu ya Mungu watakapoona anajibu maombi yanayohusu mambo halisi ya maisha yao. Ifanyeni ibada ya familia kuwa wakati wa furaha na kubadilishana uzoefu wa maisha katika hali ya uhuru.
5. Siri Saba Za Maombi Yanayojibiwa
Musa alipoomba, Bahari ya Shamu iligawanyika. Eliya alipoomba, moto ulishuka kutoka mbinguni. Danieli alipoomba, malaika aliyafumba makanwa ya simba wale wenye njaa kali. Biblia inatueleza visa vingi vya kusisimua vya maombi yaliyojibiwa. Tena inapendekeza kwetu maombi kama njia ya kupata ule uweza kwetu maombi kama njia ya kupata ule uweza mkuu wa Mungu. Yesu anaahidi hivi:
"Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nami nitalifanya" - (Yohana 14:14).
Lakini maombi mengine bado yanaonekana kana kwamba hayasikilizwi. Kwa nini? Hapa chini zipo kanuni saba zitakazokusaidia wewe kuomba kwa ufanisi zaidi:
(1) Uwe karibu sana na Kristo.
"NINYI MKIKAA NDANI YANGU, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtapewa." - Yohana 15:7.
Tunapoupa kipaumbele uhusiano wetu na Mungu na kuwa karibu naye, tutakuwa tunasikiliza na kutazamia kupata majibu kwa maombi yetu ambayo, vinginevyo, tusingeyatambua.
(2) Endelea Kumtumaini Mungu.
"MKIAMINI, mtapokea yote myaombayo katika sala zenu" - (Mathayo 21:22).
Kuamini au kuwa na imani, maana yake ni kwamba tunamtazamia Baba yetu aliye mbinguni kwamba kweli atatupa hayo mahitaji yetu. Kama wewe una wasiwasi kwamba huna imani, basi, kumbuka kwamba Mwokozi alitenda mwujiza kwa mtu yule aliyemsihi sana akiwa amekata tamaa, aliyesema:"
"Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu!" - (Marko 9:24).
Wewe kazana tu kuitumia imani ULIYO nayo; usiwe na waiswasi juu ya imani ile usiyo nayo.
(3) Jisalimishe kimya kimya chini ya mapenzi ya Mungu.
"Huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu cho chote SAWA SAWA NA MAPENZI YAKE, anatusikia" - (1 Yohana 5:14).
Kumbuka kwamba Mungu anataka kutufundisha sisi, pamoja na kutupa sisi vitu, kwa njia ya maombi. Kwa hiyo, wakati mwingine anatuelekeza upande mwingine. Maombi ni njia ya kutusogeza sisi zaidi na zaidi karibu na mapenzi ya Mungu. Hisia zetu zinatakiwa ziwe kali kutambua majibu ya Mungu na kujifunza kitu kutokana nayo. Kuyafuatilia kwa karibu maombi yetu fulani fulani ya pekee pamoja na kile kinachotokea kuhusiana nayo ni msaada mkubwa kwetu.
Roho Mtakatifu atakusaidia kulenga shabaha yenyewe: "Roho anawaombea watakatifu kulingana na mapenzi ya Mungu" (Warumi 8:27. Kumbuka kwamba mapenzi yetu yangeweza kulandana siku zote na mapenzi ya Mungu endapo sisi tungeweza kuona kama yeye anavyoona.
(4) Mngojee Mungu kwa Saburi.
"NALIMNGOJA BWANA KWA SABURI, akaniinamia akakisikia kilio changu" - (Zaburi 40:1).
Jambo kubwa hapo ni kukaza mawazo yako yote kwa Mungu, kukaza mawazo yako yote juu ya suluhisho lake. Wala usithubutu kumwomba Mungu akusaidie kwa dakika moja, na halafu kujaribu kuzizamisha shida zako kwa kujifurahisha katika anasa dakika inayofuata. Umngoje Bwana kwa saburi; tunahitaji kuwa na nidhamu hiyo vibaya sana.
(5) Usiing'ang'anie Dhambi iwayo yote.
("Kama ningalinuia maovu moyoni, Mwenyezi-Mungu hangalinisikiliza")- Zaburi 66:18.
Dhambi ijulikanayo hukata mara moja uweza wa Mungu katika maisha yetu; inatutenga mbali na Mungu (Isaya 59:1-2). Huwezi kuishika na kuing'ang'ania dhambi kwa mkono mmoja na kunyosha mkono mwingine kupokea msaada wa Mungu. Ungamo la dhambi litokalo moyoni hasa pamoja na toba ya kweli ndilo suluhisho la tatizo hilo.
Kama sisi hatutaki kumruhusu Mungu kutuweka huru mbali na mawazo, maneno na matendo yetu mabaya, basi, maombi yetu hayawezi kutuletea jibu lo lote.
"Hata mwaomba, wala hampati, kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu" - (Yakobo 4:3).
Mungu hatajibu "ndiyo" kwa maombi ya uchoyo. Acha wazi masikio yako yapate kuisikia sheria ya Mungu [Amri Kumi], yaani, mapenzi yake, naye ataacha masikio yake wazi kuzisikia dua zako.
"Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria [Amri Kumi], hata sala yake ni chukizo" - (Mithali 28:9).

(6) Tambua Kwamba Unamhitaji Mungu.
Mungu huwajibu wale wanaoomba kuwako kwake na uweza wake katika maisha yao.
"Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa." - Mathayo 5:6.
(7) Kuendelea Kuomba Tu.
Yesu alitoa kielelezo cha kuwapo kwa haja ya kuendelea tu kutoa dua zetu kwa kusimulia kisa kile cha mjane aliyekuwa anaendelea tu kuomba na kuendelea kuja kwa hakimu akiwa na ombi lake lile, lile. Mwishowe yule hakimu alisema, huku akiwa ameudhika vibaya sana, "Kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitahakikisha kwamba nampatia haki yake." Kisha Yesu alitoa hitimisho lake hili: "Je! Mungu hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku? Je! atazidi kuahirisha kuwapatia haki yao?" (Luka 18:5-7).
Zungumza na Mungu juu ya mahitaji yako yote, matumaini yako yote, na ndoto zako zote. Omba mibaraka ya pekee, omba msaada unapokuwa na shida. Endelea kutafuta, tena endelea tu kusikiliza, mpaka ujifunze kitu fulani kutokana na jibu lake Mungu.
6. Malaika Wanayahudumia Mahitaji Ya Waombao
Mtunga Zaburi alishangilia kwamba kwa njia ya huduma ya malaika wa Bwana maombi yake yalijibiwa:
"Nalimtafuta BWANA akanijibu; akaniponya na hofu zangu zote... malaika wa BWANA hufanya kituo kuwazunguka wale wamchao na kuwaokoa" (Zaburi 34:4-7).
Tunapoomba, Mungu anawatuma malaika zake kujibu maombi yetu (Waebrania 1:14). Kila Mkristo anaye malaika wake mlinzi anayetembea pamoja naye:
"Angalieni msimdharau mmojawapo wa wadogo hawa. Kwa maana nawaambia ya kwamba MALAIKA WAO mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni." - Mathayo 18:10.
Kwa sababu ya maombi yetu tunayotoa:
"Bwana yu karibu. Msiwe na wasiwasi na jambo lo lote, lakini katika kila jambo kwa maombi na dua zetu pamoja na kushukuru, wekeni mambo yenu myatakayo mbele zake Mungu. Ndipo amani ya Mungu, ipitayo ufahamu wote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu." - Wafilipi 4:5-7.
7. Mtindo Wa Maisha Ya Kikristo
Biblia inaeleza wazi juu ya mtindo wa maisha ya Kikristo. Kulingana na Waefeso 4: 22-24, Mkristo anatakiwa ku"vua" mtindo wake wa maisha ya zamani uliotokana na "tamaa zenye kudanganya", na ku"vaa" mtindo mpya wa maisha ambao ume"umbwa kwa mfano wa Mungu." Katika maandiko hayo na mwongozo tuligundua kwamba wakati ule wa kuzaliwa upya sisi tuna"umbwa upya" kuwa watu tofauti ndani ya Kristo.
Mwongozo huu na miongozo sita inayofuata hutangaza upya mtindo wa maisha ya Mkristo; huifunua siri ya maisha ya Kikristo yenye furaha. Itakusaidia wewe kujenga uhusiano wenye nguvu zaidi na Kristo, ambao matokeo yake yatakuwa mtindo wa maisha ya Kikristo ulio tofauti. Kwa hiyo kaza macho yako kwa Yesu leo hii, nawe unaweza kuwa na sehemu katika sherehe ile ya mwisho ya ushindi wakati amani yake Kristo itakapotawala bila kupingwa.

© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.

 
Powered by Blogger.