Idadi ya wapigakura siyo msingi wa vyama kushinda-Wachambuzi

Mwananchi akipiga kura
Dar es Salaam. Wachambuzi wa masuala ya kisiasa nchini wamesema idadi kubwa ya wapigakura katika mikoa ambayo ni ngome kuu za baadhi ya vyama vya siasa siyo msingi wa vyama hivyo kushinda Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Wamesema sababu za wananchi kujiandikisha kupigakura zipo nyingi, ikiwamo kuhitaji vitambulisho vya kupigia kura kufanyia shughuli nyingine, kusisitiza kuwa sera nzuri za vyama husika ni msingi mkuu wa ushindi.
Kauli hiyo inakuja siku moja baada ya gazeti hili kukokotoa na kubaini mikoa tisa yenye idadi kubwa ya wapigakura baada ya mapema wiki hii Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza idadi ya wapigakura waliojiandikisha kuwa ni milioni 22.75 watakaogawanywa katika vituo 65,105 kila kimoja kikiwa kimepangiwa wapigakura wasiozidi 450.
Mikoa yenye wapigakura zaidi ya milioni moja ni Mbeya, Mwanza, Morogoro, Tabora, Dodoma, Kagera, Tanga na Arusha huku Dar es Salaam ukiwa na wapigakura milioni mbili.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria (OUT), Hamad Salim alisema, “Tanzania hakuna utafiti uliotolewa unaoonyesha sababu za wananchi kutojitokeza kupigakura. Taarifa nyingi zinazotolewa ni za kuhisi tu.”
Alisema wapo wanaojiandikisha na kuvitumia vitambulisho vya kupigia kura kwa shughuli nyingine, “Pia wapo ambao hawaoni umuhimu wowote na wapo ambao hawavutiwi na sera za vyama.”
Alisema wananchi wa sasa wanahoji ahadi na kauli zinazotolewa na wagombea ambao hushindwa kutoa majibu sahihi wanapotakiwa kueleza mikakati watakayoitumia kutekeleza mambo hayo.
“Ahadi pia zimekuwa nyingi kiasi cha kuwafanya wananchi kuamini kuwa wagombea wanataka kupigiwa kura tu maana siasa sasa ni ajira. Kifupi ni kwamba ahadi nyingi zinazotolewa hazitekelezeki,” alisema Salim.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu (UDSM), Richard Mbunda alisema jambo la msingi la kutazama ni idadi ya wananchi wanaojitokeza katika mikutano ya kampeni kwa maelezo kuwa wana nafasi kubwa ya kusikiliza sera za vyama na wagombea na kumchagua mwenye sera watakazoridhika nazo.
“Ukitaka kuthibitisha hilo tazama mijadala kuhusu sera inayoibuka baada ya kumalizika kwa kampeni za vyama mbalimbali. Sera nzuri ndiyo zitavipa vyama ushindi si vinginevyo,” alisema.
Mhadhiri mwingine wa UDSM, Bashiru Ally alisema takwimu za idadi ya watu ni kitu kingine na wanaojitokeza siku ya kupigakura ni kitu kingine na kwamba takwimu hizo hazipaswi kuchambuliwa na watu waliovaa miwani ya vyama vya siasa.
“Tangu Uchaguzi Mkuu wa 2010 wanaojiandikisha kupigakura ni wengi kuliko wanaojitokeza kupigakura. Wengi hutumia vitambulisho vyao kwa shughuli nyingine na ili kuvipata ni lazima wajiandikishe na hakuna vitambulisho mbadala wanavyoweza kuvitumia katika mabenki na shughuli nyingine.
“Thamani ya kura inahusiana zaidi na utendaji wa wale wanaochaguliwa. Kama wananchi wataona watu hao ni viongozi bora wataona thamani ya kujitokeza kwa wingi kuwachagua,” alisema.
Alifafanua kuwa zipo sababu nyingine za wananchi kushindwa kupigakura ambazo ni kufariki dunia, kubanwa na shughuli nyingine muhimu na kuogopa vurugu siku ya uchaguzi.
“Pamoja na hayo hatujawahi kuwa na rais aliyeshinda chini ya asilimia 60 na pia hatujawahi kuwa na rais ambaye hakuchaguliwa na wananchi wote kwa maana kila mkoa,” alisema.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Ruaha, Profesa Gaudence Mpangala alitofautiana na wenzake akieleza kuwa vyama vitapata kura nyingi katika mikoa ambayo vinakubalika zaidi.
“Sera za chama na mgombea ni moja ya sababu ya msingi lakini kukubalika kwa chama katika mkoa husika ni kete muhimu sana. Mfano ni mkoa wa Mwanza, Mbeya, Dar es Salaam na Morogoro chama kikikubalika katika mikoa hiyo kinaweza kupata ushindi.
“Morogoro ni ngome ya CCM ila Dar es Salaam CCM na Ukawa watagawana kura. Mwanza na Mbeya pia wapinzani wanakubalika na wanaweza kupata kura huko. Ruvuma hakuna wapigakura wengi lakini ni ngome ya CCM. Ukifuatilia idadi ya wapigakura katika kila mkoa unaweza kubashiri chama kitakachoshinda,” alisema.

Powered by Blogger.