Serikali yaanza kulipa madeni ya walimu

Mwalimu wa shule ya msingi akifundisha darasani
Sengerema. Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, imeanza kulipa madeni ya walimu yanayofikia Sh162.1 milioni.
Ofisa Elimu ya Msingi wa wilaya hiyo, Oscar Kapinga alisema juzi kuwa hatua hiyo inatokana na Serikali kusikia kilio cha muda mrefu cha walimu kuhusu madeni yao.
Kapinga alisema kabla ya uhakiki madeni ya walimu yalikuwa Sh276.4 milioni kwa idara za elimu ya msingi na sekondari, lakini baada ya uhakiki ilibainika yaliyokuwa halali ni Sh162.1 milioni.
Alisema kwa Idara ya Elimu ya Msingi pekee, walimu walikuwa wanadai Sh130 milioni ambazo zimeanza kulipwa na kwamba, madeni hayo hayahusu mishahara bali ni malimbikizo ya likizo, uhamisho, masomo, wastaafu, mazishi na matibabu.
Ofisa huyo alisema halmashauri itaendelea kulipa madeni hayo kwa wakati ili kuondoa kero za walimu zinazotokana na kudai malimbikizo mbalimbali.
Aliongeza kuwa licha ya malipo hayo, Serikali imelipa malimbikizo ya mishahara ya Januari, Mei, Juni na Agosti huku walimu 591 wakilipwa Sh141 milioni.
Aliwataka walimu kufanya kazi kwa bidii na weledi kwa kuwa Serikali imesikia kilio chao.
Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Wilaya ya Sengerema, Luhumbika Francis alisema licha ya kuanza kulipwa madeni hayo, wanaidai Serikali zaidi ya Sh800 milioni zikiwa ni fedha za malimbikizo ya mishahara.
-
osted Friday, October 16, 2015 | by- Daniel Makaka, Mwananchi
Powered by Blogger.