Mwanamke aliyetekwa nyara Kenya aokolewa

Dadaab
  • 16 Oktoba 2015
Image caption Maelfu ya Wasomalia waliotoroka vita nchini mwao hukaa kama wakimbizi Dadaab
Wanajeshi wa Kenya na Somalia wamefanikiwa kumuokoa mwanamke aliyekuwa ametekwa nyara katika eneo la Dadaab, kaskazini mashariki mwa Kenya.
Taarifa ya msemaji wa Majeshi ya Ulinzi ya Kenya (KDF) Kanali David Obonyo imesema Judy Mutua ameokolewa kwenye operesheni ya kijeshi eneo la Shaba-Difu, kilomita 15 ndani ya Somalia.
Operesheni hiyo imeshirikisha majeshi ya Kenya, kikosi cha polisi wa utawala Kenya, na wanajeshi wa Somalia.
Bi Mutua, aliyetekwa nyara Oktoba 12 na watu wasiojulikana, anapokea matibabu na atasafirishwa hadi Nairobi baadaye leo, Kanali Obonyo amesema.
Ameongeza kuwa mtekaji nyara mmoja ameuawa na mwingine kukamatwa.
Mkuu wa usalama wa serikali ya Kenya eneo la Kaskazini Mashariki Mohammud Swaleh amesema Bi Mutua alipelekwa mji wa Dobley kwenye mpaka wa Kenya na Somalia baada ya kuokolewa.
Ingawa kundi ya al-Shabab halijadai kuhusika katika utekaji nyara huo, Kanali Obonyo amedai ndio waliohusika katika utekaji nyara huo kwenye taarifa yake.
Bi Mutua alikuwa akifanya kazi na shirika shirika lisilo la kiserikali la Windle-trust, moja ya mashirika yanayohudumu katika kambi ya wakimbizi ya Dadaab, inayotoa hifadhi kwa takriban wakimbizi 450,000 kutoka Somalia.
Powered by Blogger.