Vijana kete muhimu kupata urais 2015

ya urais ashinde
Dar es Salaam. Wiki moja kabla ya Uchaguzi Mkuu imebainika kwamba, ili mgombea yeyote wa nafasi ya urais ashinde kiti hicho ni lazima awe na ushawishi mkubwa kwa vijana, hasa wa kike.
Taarifa iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikiainisha idadi ya watu waliojiandikisha kiumri, inaonyesha kuwa asilimia 57 ya wapigakura wote waliojiandikisha na kuthibitishwa kupigakura Oktoba 25, wana umri chini ya miaka 35.
Taarifa hiyo ambayo imewagawa wapigakura wote 22.75 milioni kwenye makundi matatu; miaka 18 mpaka 35; 36 mpaka 50 na 51 na kuendelea, inaonyesha mshindi wa urais ni lazima alishike kundi hilo ili aibuke kidedea wakati kinyang’anyiro hicho kitakapokuwa kinahitimishwa.
Taarifa hiyo ambayo imewagawa wapigakura wote 22.75 milioni kwenye makundi matatu; miaka 18 mpaka 35; 36 mpaka 50 na 51 na kuendelea, inaonyesha mshindi wa urais ni lazima alishike kundi hilo ili aibuke kidedea wakati kinyang’anyiro hicho kitakapokuwa kinahitimishwa.
Kati ya wapigakura wote waliopo, vijana wenye umri kati ya 18 na 35 ni 12,894,576. Kati yao wanaume ni 6,155,613 (asilimia 27) na wanawake ni 6,738,964 ( asilimia 30) ya wapigakura wote waliojiandikisha mwaka huu.
Hii ina maana kwamba, endapo kundi hili lote litamuunga mkono mgombea mmoja na kumchagua, basi atashinda kwa asilimia 57 na ambazo haziwezi kupatikana kwa rika nyingine zilizobaki.
Takwimu hizi zinadhihirisha mikakati ya ziada, ambayo vyama husika inatakiwa kuwa nayo ili kuongeza wafuasi na kujihakikishia ushindi.
Mchanganuo huo unaonyesha zaidi kuwa watu wa rika ya kati, kati ya miaka 36 mpaka 50 hawafiki hata nusu ya vijana hawa, kwani wapo 5,690,668. Hiyo ni asilimia 25 ya wote waliojiandikisha. Wao wanajumuisha wanaume 2,744,422 (asilimia 12) na wanawake 2,946,247 (asilimia 13) ya wapigakura wote.
Makundi haya mawili pekee yanatengeneza asilimia 82 ya wapigakura wote huku asilimia 18 zinazosalia yaani wapigakura 4,165,544 zikiwa ni za wazee.
Kwa wazee hawa, wamo wanaume 1,900,555 au asilimia nane ya wanawake 2,264,990 ambao ni asilimia 10.
Akizungumzia takwimu hizo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udsm), Dk Benson Bana alisema kuna haja kwa washauri na wagombea kuzitumia vizuri taarifa hizi katika kunadi sera zao, kwani kila kundi lina mahitaji yake maalumu na ndani yake pia yapo madaraja.
Alifafanua kwamba haitoshi kusema vijana au wanawake wanajitokeza kwa wingi bila kueleza ni kwa namna gani kero zao zitataliwa, endapo chama au mgombea husika atapewa ridhaa na kundi hilo.
“Ni vigumu kutabiri misimamo ya kiitikadi ya kundi hili. Inaweza kuwa rahisi kujua wanafunzi wa vyuo wanahitaji nini kwa sababu mawazo na mitizamo yao ni kama huwa inafanana, lakini haiwezekani kwa wale wanaofuga, kulima au waliojiajiri.
Ni muhimu sera zikabainisha zitafanya nini na wajane, wasio na ajira, wajasiriamali na makundi mengineyo ndani ya lile la vijana,” alisema Dk Bana.
Profesa Gaudence Mpangala wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ruaha (Ruco), alisema kuna umuhimu wa kila kundi kushiriki kwa mapana kwenye mchakato wa uchaguzi ili kuwa na nafasi nzuri ya kufanya uamuzi unaostahili. Alisema ingawa ipo dhana, inayohitaji kufanyiwa utafiti, kwamba wanawake wanaipenda CCM na vijana upinzani bado haitoshi kujiaminisha juu ya ushindi.

Powered by Blogger.