Magufuli akubali, Lowassa achomoa mdahalo


Dar es Salaam. Siku moja kabla ya kufanyika kwa mdahalo wa wagombea urais nchini, Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) umesema mgombea wao kupitia Chadema, Edward Lowassa hatashiriki shughuli hiyo huku CCM ikithibitisha mgombea wake, Dk John Magufuli kushiriki.
Kitendo cha Lowassa kutokuwapo katika mdahalo huo utakaofanyika kesho saa 7:30 mchana hadi saa 10 jioni, kutapunguza ushindani miongoni mwa wagombea wakuu wawili ambao wanachuana vikali katika uchaguzi unaotajwa kuwa wa kihistoria.
Licha ya vyama vinane kusimamisha wagombea urais, vinavyochuana zaidi ni Chadema chini ya mwamvuli wa Ukawa na CCM, huku ACT-Wazalendo ikionekana kuleta upinzani.
Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, Salum Mwalimu aliliambia Mwananchi jana kuwa, kwa sasa mgombea wao yupo katika Kanda ya Ziwa kwenye kampeni, hivyo itakuwa ngumu kuhudhuria mdahalo huo unaosubiriwa kwa hamu.
Hata hivyo, wakati Lowassa akikosekana katika mdahalo huo, Mkurugenzi wa Taasisi ya Twaweza, Aidan Eyakuze alisema hadi jana vyama vinne vilikuwa vimethibitisha ikiwamo CCM.
Vyama vingine vitakavyoshiriki mdahalo huo kwa mujibu wa Eyakuze ni Alliance for Democratic Change (ADC), ACT-Wazalendo na Chaumma.
Alisema jana walipokea barua ya uthibitisho kutoka CCM ikisema itashiriki, hivyo kuongeza idadi ya vyama vitakavyochuana hadi kufikia vinne kati ya vitano ambavyo vilikidhi vigezo vya kushiriki mdahalo.
“Tunatarajia atakuwapo Dk John Magufuli katika mdahalo wetu na bado tunaendelea na mazungumzo na Ukawa ili watupatie majibu kwa maandishi kama watashiriki au la.
“Mlango wetu utakuwa wazi kuhakikisha tunawapatia fursa ya kujibu maswali ya wananchi watakayowauliza, lakini tumeshaeleza kuwa watakaoshiriki mdahalo huu ni wagombea wa urais na siyo vinginevyo,” alisema Eyakuze.
Hata hivyo, Mwalimu alisema suala la muda ni kikwazo kwao kitakachofanya mgombea wao kutoshiriki mdahalo huo ulioandaliwa na Twaweza, Tanzania Media Foundation (TMF), Taasisi ya CEO roundtable na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa).
“Huwezi kumwondoa mgombea kwenye kampeni aende kwenye mdahalo akatumie siku mbili kujiandaa na kusafiri bila kuwafikia wananchi vijijini ambao wanamsubiri kwa hamu, kifupi sisi tunawatakia kila la kheri,” alisema Mwalimu kwa njia ya simu.
Naye Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi, Uendeshaji na Utawala wa ADC, Jumanne Magafu alipendekeza maboresho ya sheria ya uchaguzi ili midahalo iwe sehemu ya mchakato wa Uchaguzi Mkuu siku zijazo.
Alisema kwa sasa hakuna sheria wala kanuni zinazowalazimisha watu muhimu kama wagombea wa urais kuhudhuria midahalo na kujibu maswali ya wananchi, jambo ambalo huwa ni adimu katika mikutano yao ya kampeni.
“Tunaendelea kujiandaa vizuri na mdahalo huu, mgombea wetu wa urais, Anna Mghwira kwa sasa yupo kwenye kampeni atarudi kesho maalumu kwa ajili ya shughuli hiyo ya Jumapili,” alisema Vanance Msebo, Mkurugenzi wa Kampeni wa ACT-Wazalendo.
Powered by Blogger.