Tanzania yaikosoa filamu ya albino UN

Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi (kulia) akizungumza kwenye umoja huo ikiwa ni muda mfupi kabla ya kuonyeshwa kwa filamu ya “The Boy from Geita” ambayo inaelezea uovu wanaotendewa watu wenye ulemavu wa ngozi. Picha na UN
New York, Marekani. Siku moja baada ya mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, kuelezea kwa waandishi wa habari juhudi zinazofanywa na Serikali dhidi uovu wanaofanyiwa watu wenye ulemavu wa ngozi, Kamisheni ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa (UNHR ) imesema itashirikiana na Serikali ya Tanzania katika juhudi hizo za kuukabili uovu unaofanywa dhidi ya jamii hiyo ya Watanzania.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Msaidizi wa Ofisi ya Kamisheni ya Haki za Binadamu, Ivan Simonovic muda mfupi kabla ya kuonyeshwa kwa filamu iliyochezwa Tanzania ya “The Boy from Geita”.
Simonovic alisema kuwa ushirikiano huo ni katika kutambua juhudi zinazofanywa na Serikali katika siyo kwa kuhakikisha tatizo hilo linatoweka pia kwa kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaohusika na ukatili huo.
“Tofauti na nchi nyingine, Serikali ya Tanzania imeonyesha ujasiri na uthubutu wa kukabiliana na uovu unaofanywa dhidi ya watu wenye ualibino. Ni kwa kutambua juhudi hizo tutashirikiana na serikali katika kukomesha uovu huu,” alisema Simonovic.
Kauli Simonovic ya kutambua juhudi hizo imetokana na juhudi iliyofanywa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania, Balozi Tuvako Manongi ya kuonana na wakuu wa idara ambazo zimefadhili kuonyeshwa kwa filamu hiyo UN pasipo kuushirikisha wala kuujulisha uwakilishi wa Tanzania. Maelezo ya awali kuhusu filamu hiyo yanadaiwa kupotosha baadhi ya mambo hali iliyomfanya mwakilishi huyo wa Tanzania kuchukua fursa ya kuyatolea ufafanuzi.
“Usiku huu ninapenda kutambua juhudi zinazofanywa na moja ya nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa, Tanzania, ambayo mwakilishi wake yupo pamoja nasi. Siyo tu kwamba Tanzania imeonyesha ujasiri na uthubutu wa kutambua ukubwa wa tatizo linalowakumba watu wenye ualibino pia imefanya juhudi za kuwaelimisha wananchi wake huku ikichukua hatua muhimu,” alieleza Simonovic. Alipopewa nafasi ya kuzungumza mbele ya hadhara hiyo. Balozi Manongi alirejea kauli aliyoitoa mbele ya waandishi siku ya Jumatano, kwamba, Tanzania haikatai na wala haipingi kwamba kuna tatizo kwa watu wenye ulemavu wa ngozi. Alisema pamoja na kukiri kuwapo kwa matukio ya uovu dhidi ya Watanzania hao, lakini angependa pia kuweka rekodi sawa na hasa kufuatia maelezo ya upotoshaji ambayo yametolewa kwenye vipeperushi vinavyoitangaza filamu hiyo.
Baadhi ya mambo ambayo balozi ameyatolea ufafanuzi ni lile linaloelezwa na waandaaji wa filamu hiyo wanaodai kuwa ualbino ulianza Tanzania miaka 2000 iliyopita jambo analosema halijathibitishwa kisayansi.
-
Powered by Blogger.