Mdomo wamponza Mourinho afungiwa, kupigwa faini

Kocha Jose Mourinho
London, England. Klabu ya Chelsea na kocha wake, Jose Mourinho wamepinga uamuzi wa Chama cha Soka (FA) kumwadhibu kocha huyo kwa kauli alizozitoa karibuni.
Juzi, Mourinho alifungiwa mechi moja na kupigwa faini ya Pauni 50,000 kwa kauli dhidi ya waamuzi wanaochezesha Ligi Kuu. Adhabu hiyo dhidi ya Mourinho imetolewa wiki moja baada ya mbaya wake, Arsene Wenger wa Arsenal kunusurika adhabu kwa kauli dhidi ya mwamuzi Mike Dean aliyemwita dhaifu na asiyejua wajibu wake.
Mourinho ambaye ataikosa mechi dhidi ya Aston Villa Jumamosi alionyesha kuwa mwenye hasira.
Kocha huyo Mreno aliwatuhumu waamuzi kuwa walikuwa wakizipendelea timu nyingine za Ligi Kuu zinapocheza na Chelsea.
Mourinho alimwelekezea shutuma Wenger akidai kuwa amekuwa akifanya mambo yake na kuonekana kuwa juu ya sheria na FA.
Baada ya mechi dhidi ya Southampton, Oktoba 3, ambayo Chelsea ilifungwa mabao 3-1, Mourinho aliwashushia lawama waamuzi.
Kauli hiyo ilimlenga mwamuzi Robert Madley baada ya mshambuliaji Radamel Falcao ambaye kwa mtazamo wa Mourinho aliangushwa na kipa wa Southampton, Maarten Stekelenburg. Picha za marudio za televisheni zilipingana na mtazamo wa Mourninho.
Mourinho alisema: “Ninafikiri kwamba ni muda mwafaka kuwa wakweli na kusema bila kificho kwamba waamuzi wanaogopa kutoa uamuzi unaoinufaisha Chelsea.”
“Kama FA inataka kuniadhibu, inaweza kufanya hivyo. Lakini, hawatoi adhabu kwa makocha wenzangu, wananiangalia mimi. Hilo siyo tatizo kwangu.”
Klabu yake, Chelsea ilieleza jana kuumizwa na kufungiwa kwa kochake ambaye akirudia kosa hilo ndani ya mwaka mmoja atazuia kuingia uwanjani.
Naye Mourinho alieleza kusikitishwa na uamuzi dhidi yake huku baada ya kumshambulia mwamuzi Dean kwenye mchezo wa ligi ambao Arsenal ilifungwa mabao 2-0 na Chelsea, Septemba 19.
Kocha huyo, The Special One amekuwa akidai kwamba kauli zake zimekuwa zikichukuliwa kinyume na kile alichokimaanisha, kuonyesha kuwa wanamlenga yeye zaidi.

Powered by Blogger.