Sakata la kulinda kura latua Mahakama Kuu

Peter Kibatala
Dar es Salaam. Hatimaye mvutano kati ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na vyama vya siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuhusu umbali wa mwananchi kusimama baada ya kupiga kura, umetinga Mahakama Kuu.
Aliyefungua kesi hiyo ya kikatiba mahakamani ni mpigakura na mgombea ubunge wa viti maalumu katika Jimbo la Kilombero kupitia Chadema, Amy Pascience Kibatala akiomba litolewe tamko kuhusu tafsiri ya kifungu cha 104 (1) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, sura ya 343 Ilivyorejewa mwaka 2010.
Chadema, Amy Pascience Kibatala akiomba litolewe tamko kuhusu tafsiri ya kifungu cha 104 (1) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, sura ya 343 Ilivyorejewa mwaka 2010.
Kibatala amefungua kesi hiyo dhidi ya Mwasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Mwenyekiti wa NEC, chini ya hati ya dharura. Shauri hilo namba 37 la mwaka 2015, limefunguliwa baada ya NEC kuwataka wananchi, baada ya kupiga kura Oktoba 25, warudi nyumbani huku Ukawa unaoundwa na Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD wakihimiza wanachama na wafuasi wao kulinda kura kwa kukaa umbali wa mita 200 baada ya kupiga kura kama sheria inavyosema.
Awali NEC iliwataka wapigakura kurudi nyuma hadi mita 200 baada ya kupiga kura lakini baadaye iliwataka wapigakura kurudi nyumbani. Msimamo huo ulitolewa pia na Rais Jakaya Kikwete siku ya maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 16 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ambapo aliwataka wapigakura kwenda nyumbani baada ya kupiga kura.
Akihutubia katika maadhimisho hayo Oktoba 14 yaliyokwenda sambamba na tukio la kuzima Mwenge wa Uhuru, mjini Dodoma, Rais Kikwete alitoa wito kwa watu wote kurudi majumbani kwao mara tu baada ya kumaliza kupiga kura.
Katika shauri hilo, Kibatala anaiomba Mahakama Kuu itoe tamko la tafsiri sahihi ya kifungu hicho kinachohusu haki ya wapigakura na wadau wengine wa uchaguzi kukaa zaidi ya umbali wa mita 200 kutoka katika kituo cha kupigia kura na cha kuhesabia kura.
Kwa mujibu wa Kibatala msimamo wa NEC ni kinyume cha Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania hususan Ibara ya 18 (1), 21 (2), 29 (2). Pia, anadai kuwa Rais Kikwete wakati akihutubia wananchi kwenye maadhimisho ya kifo cha Baba wa Taifa,licha ya kuamuru watu wasikae katika eneo hilo, pia alikwenda mbali kwa kuwatisha wapigakura kuwa watakaokaidi amri hiyo vyombo vya dola vitatumia nguvu dhidi yao.
Kibatala anadai kuwa akiwa mpigakura aliyesajiliwa na anayekusudia kutumia haki ya msingi kushiriki mchakato huo wa uchaguzi, zuio hilo linakiuka haki za kikatiba zinazobainishwa katika Ibara ya 5(1), 18 (1), 21 (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kibatala anadai kuwa zuio hilo linaathiri haki ya kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi uliotangazwa kuwa utakuwa wa wazi.
Vilevile, anadai kuwa zuio hilo linaelekea kumnyima haki ya kufuatilia kwa karibu mchakato wa uchaguzi kutoka umbali uliowekwa kisheria ambao unamwezesha kuwapo wakati wa kutangazwa kwa matokeo kwa kuzingatia kuwa hakuna utaratibu rasmi wa NEC kuwaita wapiga kura kusikiliza matokeo.

Powered by Blogger.