Boban, Kaseja kuitibulia Simba SC

Wachezaji wa Mbeya City, Haruna Moshi ‘Boban’ (kushoto) na Juma Kaseja (kulia)
Mbeya. Mshambuliaji wa zamani wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ na kipa Juma Kaseja ni miongoni mwa silaha za Mbeya City zilizoandaliwa kuiua timu ya Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam.
Boban alijiunga rasmi na kikosi cha Mbeya City juzi na jana asubuhi aliungana na wenzake kwenye mazoezi yaliyofanyika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya kujiandaa kuikabili Simba.
Kocha msaidizi wa City, Meja Mstaafu Abdul Mingange aliliambia gazeti hili jana kwamba Boban ni mmoja wa wachezaji wanaotarajia kuchezeshwa kwenye mechi ya kesho dhidi ya Simba itakayochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine.
Mbeya City, pia inaye kipa wa zamani wa Simba na Taifa Stars, Juma Kaseja aliyesaini mkataba wa msimu mmoja.
Alisema, “Leo nimesema afanye zoezi kwa lengo kumwangalia, lakini nimeona yupo vizuri na lazima mechi ya keshokutwa (kesho), Jumamosi atacheza dhidi ya Simba.”
Hata hivyo, uongozi wa klabu hiyo haukutaka kuelezea matumaini ya ujio wa Boban ndani ya klabu hiyo, huku ukisema Boban ni mchezaji wao halali na hawawezi kumzungumzia mtu mmoja, bali wanawazungumzia wachezaji wote.
Mwenyekiti wa Mbeya City, Mussa Mapunda alisema, “Kwanini Boban, sisi hapa wachezaji wote wapo sawa, hivyo hatutaki ubaguzi wa kumzungumzia mchezaji mmoja hapa.”
Kuhusu mechi ya kesho dhidi ya Simba, Meja Mingange alisema anaouna mchezo huo kuwa utakuwa mgumu kwake kutokana na kila timu kupania kushinda katika mechi hiyo, lakini amejipanga vizuri kuhakikisha waendeleza ubabe kwa Simba.
Kuhusu mazingira ya ugumu wa mechi hiyo, Afande Mingange alisema kwanza yeye binafsi ana siku tatu tangu aanze kuinoa timu hiyo, hivyo hawezi kuwa jipya la ziada kuwabadili wachezaji wake, lakini pia kuna mchanganyiko mkubwa wa wachezaji ambao ni wapya kwenye kikosi chake.
Alisema, “Kubwa zaidi historia inaonyesha Simba haijawahi kushinda dhidi yetu ( Mbeya City), iwe ni ugenini ama nyumbani, hivyo watakaza ili kuvunja mwiko. Ila, nasema hivi tutapigana hadi dakika ya mwisho na Mungu atakuwa upande wetu.”

Powered by Blogger.