HOJA YA UCHUMI: Hatuhitaji kusubiri rais mpya kuiokoa shilingi

Mwishoni mwa wiki iliyopita nilipata fursa ya kubadilisha kiasi kidogo cha  fedha za kigeni katika moja ya maduka ya kubadilishia fedha  Kariakoo jijini Dar es Salaam.
Mara nyingi nikibadilisha fedha hizo katika maduka mbalimbali huwa sipatiwi risiti zinazonitambulisha kuwa nimeuza Shilingi au nimenunua fedha ya kigeni.
Hali  hiyo nimekumbana nayo kwa muda sasa kiasi cha kunipa wasiwasi juu ya ufanisi katika udhibiti wa fedha za kigeni nchini.
Tofauti na kipindi cha nyuma safari hii nilikuta tangazo la Benki Kuu ya Tanzania lililoandikwa kwa Kiingereza likiwa limebandikwa katika  duka hilo.
Tangazo hilo lilikuwa linayataka maduka ya kubadilishia fedha kutoa risiti kwa wateja mara baada ya mauzo ya fedha za kigeni ikiwa ni utekelezaji wa kanuni ya 15 (C) ya Sheria ya Kubadilisha Fedha za Kigeni ya mwaka 2008.
Kama wateja wengine, nilitoa Dola za Marekani nilizokuwa nahitaji kuziuza nipate fedha za nyumbani, lakini baada ya kukokotoa kiwango na kupatiwa fedha hizo, mhudumu hakunipatia risiti zaidi ya kunishukuru kwa kufika dukani kwake.
Kwa kuwa nilidhamiria kudai risiti nilimuomba mhudumu huyo haki  yangu ambaye alishtuka na kuuliza “kaka kwani unataka na risiti?”
Kwa mazingira ya haraka haraka duka hilo huwa halina utamaduni wa kutoa risiti kwa wateja, kwani iliwabidi waanze kuhangaika kuwasha kompyuta mpakato kuunganisha na printa ili wachapishe risiti hiyo.
Kama njia ya kunikatisha tamaa walitumia takriban dakika tano hivi na kunieleza niwe mvumilivu kwani kulikuwa na tatizo wanashughulikia. Baada ya kuona sikati tamaa waliharakisha “kutatua tatizo” na baada ya dakika  10 hivi walichapisha risiti hiyo huku mmoja akikejeli “kaka unapeleka ofisini nini wakaiweke kwenye rekodi.”
Nimeamua kusimulia kwa kirefu kisa hiki kwa kuwa umekuwa utamaduni kwa wafanyabiashara kukwepa kutoa risiti na wateja tumekuwa tukishawishika kufuata uovu huo hata katika mahali ambapo hautengenezewi ahueni ya aina yoyote.
Tofauti na nchi za wenzetu hata kwa majirani zetu wa Kenya, ukibadilisha fedha katika maduka ya kubadilishia fedha ni lazima wahudumu wakuhoji kitambulisho chako, wachukue jina lako na kukupatia risiti. Huo ndiyo utaratibu mzuri ambao hata sheria hapa nchini zinausisitiza.
Hata hivyo, hapa nyumbani jambo hilo siyo la msingi licha ya kuwa ni kinyume na sheria za nchi. Kuna kila dalili kuwa Watanzania tuna matatizo makubwa ambayo hayahitaji rais mpya kuyatatua kama kuilinda Shilingi. Pia, hii ni ishara kuwa mamlaka zinazohusika kusimamia sheria kama BOT hazifanyi kazi ipasavyo.
Kwa elimu yangu ndogo ya uchumi kinachofanywa na maduka hayo ya kubadilishia fedha ni hatari kwa uchumi wa nchi yetu, hasa katika kipindi hiki ambacho Shilingi inazidi kushuka thamani dhidi ya fedha za kigeni, hususan Dola.
Pamoja na ukweli kuwa kuna sababu kubwa za kushusha thamani ya Shilingi yetu kama kuongezeka kwa thamani ya Dola ya Marekani ulimwenguni na kupungua kwa uuzaji bidhaa nje ya nchi, bado maduka hayo yanaweza yakafanya uovu wa makusudi kuingamiza Shilingi yetu.
Hii itatokana na ukweli kuwa, tabia ya kutokutoa risiti kwa wateja kunaficha taarifa za ukweli juu ya mzunguko wa fedha za kigeni ambazo wakati mwingine BOT huziingiza sokoni nje ya viashiria vya kisoko
Mtindo huo unaweza kusababisha mahitaji bandia ya fedha za kigeni hasa Dola na kusababisha Shilingi yetu kushuka thamani na kupandisha bei ya bidhaa na huduma kutokana na kuongezeka kwa gharama za uingizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi.
Iwapo hakuna kumbukumbu ya mauzo ya fedha hizo katika maduka ya fedha kwenda BOT, itafahamika vipi kuwa kiwango cha fedha za kigeni zinazouzwa na kununuliwa kila siku nchini? Mamlaka ya Mapato Tanzania itafahamu vipi kiasi cha kodi inayopatikana katika biashara hiyo?
Ni wazi kuwa kitendo cha maduka hayo kutotoa risiti na wananchi kutodai kunasababisha Serikali ipoteze mapato yake kwani katika kila biashara inayofanyika kuna kodi inayotakiwa kulipwa.
Kuendelea kuwakumbatia wafanyabiashara hao kutaifanya nchi iendelee kupoteza mapato ambayo yangesaidia kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo ya kijamii.
Pia, jitihada za kuzuia uvunjaji huo sheria zikawabane na wafanyabiashara wanaolazimisha wananchi kupata huduma zao kwa kutumia Dola ya Marekani kinyume na sheria hasa katika sekta ya nyumba na makazi.
Nuzulack Dausen ni mwandishi wa gazeti hili. Anapatikana kwenye mtandao wa Twitter @nuzulack

Powered by Blogger.