Kikwete aongoza mamia kumzika Kigoda

Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakari Zuberi (mbele) akiongoza swala ya mazishi ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda mjini Handeni, mkoani Tanga jana. Picha na Burhani Yakub
Handeni/Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete na mkewe Mama Salma Kikwete jana, waliwaongoza mamia ya wananchi kwenye mazishi ya aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda.
Dk Kigoda alifariki dunia Oktoba 12, kwenye Hospitali ya Apollo, India alikokuwa akitibiwa.
Akisoma wasifu wa marehemu, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mussa Uledi alisema Dk Kigoda alijikita zaidi katika kazi na ndicho chanzo cha kuchelewa kwenda kupata matibabu India.
Katika salamu zake kwa wafiwa na wakazi wa Tanga, Spika Anne Makinda alisema Bunge limepoteza mshauri mzuri wa mambo ya uchumi ambaye alikuwa hasukumwi kufanya kazi tangu alipokuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge hadi alipoteuliwa na Rais Kikwete kuwa waziri.
Viongozi wa kada tofauti walitoa salamu za rambirambi akiwamo Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Salum Mwalimu aliyesema wanasiasa wamepoteza mpambanaji na mtu ambaye hakujikweza katika nafasi zote alizozishika.
Mtoto wa Kigoda, Omar Kigoda pamoja na kutoa shukran kwa Serikali, pia aliwashukuru wakazi wa Handeni kuifariji familia hiyo.
Kabla ya mazishi hayo, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal aliwaongoza mamia ya waombolezaji kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa mwanasiasa huyo katika Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Sambamba na Makamu wa Rais, viongozi mbalimbali wa Serikali akiwamo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, mawaziri, wabunge na marais wa wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa walishiriki kuaga mwili huo.
Akisoma salamu kwa niaba ya Serikali, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe alisema kifo cha Dk Kigoda kimeacha pengo kubwa serikalini kutokana na umahiri aliokuwa nao katika masuala ya uchumi. “Daima tutamkumbuka Kigoda kwa utumishi wake uliotukuka, alijitoa kwa dhati kutumia taaluma yake katika kuliletea maendeleo taifa,”alisema.
Shughuli ya kuaga mwili huo ilimalizika saa 3,30 asubuhi na safari ya kwenda Handeni kwa mazishi ilianza. Imeandikwa na Elizabeth Edward, Rajabu Athuman na Burhani Yakub.

Powered by Blogger.