NEC: Wanasiasa acheni kutumia majukwaa vibaya

Kamishna wa Tume  Jaji mstaafu, Mary Longway
Iringa. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imewataka viongozi wa vyama vya siasa kuacha kutumia majukwaa vibaya katika muda uliobaki badala yake wanadi sera zao.
Kamishna wa Tume hiyo, Jaji mstaafu Mary Longway alisema hayo kwenye mkutano uliowakutanisha maofisa wa NEC na viongozi wa vyama vya siasa mkoani hapa juzi.
“Tume imekuwa ikifuatilia kampeni za vyama vyenu vya siasa, tumieni nafasi zenu kueleza sera ili kuwasaidia wananchi kufanya uamuzi sahihi,” alisema Longway.
Aliwaasa viongozi hao kuwasilisha malalamiko yao katika kamati za maadili zilizopo kisheria pindi wanapoona maadili na kanuni za uchaguzi zinakiukwa.
Alisema hatua hiyo itasaidia Tume kushughulikia changamoto zinazojitokeza katika kampeni kwa wakati.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Iringa, Mustapher Msowela aliitaka Tume kukutana na viongozi wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), ili kujadiliana kuhusu wananchi kukaa umbali wa mita 200.
Mwakilishi wa Chama cha SAU Iringa, Selemani Rajabu alisema katika suala la watu kulinda kura busara inapaswa kutumika ili kuepuka vurugu.
“Watu wanaosimama umbali wa mita 200 baada ya kupiga kura waachwe wasubiri endapo hawatafanya vurugu ,” alisema Rajabu.

Powered by Blogger.