Mbegu za kiume huhifadhi virusi vya ebola


Freetown, Sierra Leone. Utafiti umeonyesha virusi vya ebola vinaweza kudumu kwenye mbegu za kiume kwa baadhi ya watu waliopona ugonjwa huo kwa takriban miezi tisa.
Hayo yamo kwenye utafiti wa awali uliofanywa kwa pamoja na Wizara ya Afya na Usafi wa Mazingira ya Sierra Leone, Wizara ya Ulinzi ya nchi hiyo, Shirika la Afya Duniani (WHO) na Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Marekani.
Matokeo ya ufatifi huo yalitangazwa juzi nchini humo baada ya kukamilika kwake na kubaini siyo kila mbegu za mwanaume zinaambukiza bali ni baadhi ya watu waliopona ugonjwa huo kwa takriban miezi tisa.
Taarifa hiyo ilisema, awali virusi vilionekana kwenye mbegu za uzazi za wanaume baada ya kupona, hata hivyo kuna taarifa chache tu kuhusu muda wa virusi hivyo kudumu katika mbegu hizo.
Kwa mujibu wa utafiti wanaume wanapaswa kujizuia na aina zozote za ngono au kutumia mipira hadi wapimwe mara mbili na kuonekana hawana virusi vya ebola.
Wakati huohuo, China na Umoja wa Mataifa wamesaini makubaliano kuhusu China kuchangia Dola 5 milioni za Marekani kusaidia mapambano dhidi ya ebola.
Mchango huo utaingizwa kwenye mfuko wa fedha wa kushughulikia ebola ili kusaidia Tume ya Umoja wa Mataifa ya Kudhibiti na Ebola.
Ugonjwa huo ni miongoni mwa magonjwa yajulikanayo kwa ujumla kama homa za virusi zinaazosababisha kutokwa na damu mwilini (Viral Haemorrhagic Fevers). Chanzo kamili cha virusi vya ugonjwa huo hakijulikani.
Tafiti zinaonyesha kwamba katika orodha ya watu 10 waliopata kirusi cha ebola, wastani kati ya watu watano au tisa hufariki dunia.
-
Powered by Blogger.