‘Vichinjio’ vinavyobeba uhalali, haki


 
Wakati Uchaguzi Mkuu ukitarajiwa kufanyika Oktoba 25, ukiwa   ni wa tano tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini mwaka 1992, safari hii Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC), imetoa vitambulisho vya mpiga kura vyenye alama za utambulisho za kibaiolojia.
Licha ya hatua hiyo, kuna madai ya kusambaa na kukamatwa kwa vitambulisho bandia vya kupigia kura.
Vitambulisho hivyo vilitolewa wakati wa uandikishaji wananchi kwenye daftari hilo ulioanza Machi 23 mwaka huu mkoani Njombe na kuhitimishwa Dar es Salaam, Agosti 4.
Kupitia mfumo huo, Watanzania 22,751,292 wenye sifa wameandikishwa kwa ajili ya kupiga kura siku tisa zijazo kwa ajili ya kumchagua rais, wabunge na madiwani. Katika uchaguzi unaohusisha ya vyama vya siasa 22.
Walioandikishwa ni wale waliokuwapo kwenye daftari lililotumika katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2010, wapigakura wenye sifa ambao hawakuandikishwa awali na wote waliotimiza umri wa miaka 18 mpaka siku ya uchaguzi.
Baada ya NEC kufanikisha hatua hiyo ukafuata mchakato wa kuhakiki na kuhamisha taarifa kwa wananchi waliobadilisha makazi na maeneo ya kupigia kura na ulitengwa mwezi mmoja kwa ajili ya kazi hiyo.
Muda huo ulimalizika Septemba, hivyo kutoa fursa kwa wataalamu wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) kutoka tume hiyo kuendelea na uchakataji wa taarifa za wapiga kura zilizokusanywa.
NEC licha ya kukiri ugumu katika utekelezaji jukumu hilo, uliochangiwa na sababu mbalimbali ikiwamo za kiutawala na uwezeshaji kitambulisho cha mpigakura ndicho kithibitisho kinachobeba haki ya Mtanzania kuwa mpigakura halali.
Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mstaafu Damian Lubuva anasema walijifunga kibwebwe kuhakikisha wanakamilisha uandikishaji kwa BVR, huku akiainisha baadhi ya changamoto walizokumbana nazo.
Anataja changamoto zilizoibuka wakati wa uboreshaji wa daftari hilo kuwa ni pamoja na ugumu wa kuchukua alama za vidole kutoka kwa baadhi ya wananchi, hali iliyosababishwa na kazi za kiuchumi wanazozifanya kila siku.
Nyingine ni mashine za uchapaji kuhitaji kusafishwa mara kwa mara kutokana na mazingira ya vumbi kwenye vituo vya uandikishaji na maombi mengi ya kuanzishwa vituo vingine vya kazi hiyo wakati kazi hiyo imekwisha kuanza, pamoja na dhana potofu kwamba mfumo wa BVR utasaidia kuchakachua matokeo.
“Pamoja na changamoto hizo Tume imefanikisha uandikishaji kwa muda mfupi. Tulikuwa na mashine 8,000 pekee, lakini tukaandikisha watu wengi zaidi kuliko nchini nyingi zilizowahi kutumia teknolojia hiyo. Tumepongezwa kwa hili…Umoja wa Tume za Uchaguzi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), wamevutiwa na ufanisi wetu,” anasema Jaji Lubuva.
Kadi feki
Lubuva anasema licha ya kuzaga uvumi wa kuwapo kwa kadi za kughushi miongoni mwa wapigakura wanaotarajiwa kujitokeza siku ya uchaguzi, tishio linalotokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, lakini NEC wenye dhamana na kusimamia Uchaguzi Mkuu imejipanga kukabiliana nalo.
Tangu kuundwa kwake Januari 1993, NEC imepewa mamlaka ya kusimamia na kuendesha uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani ni. Imefanya kazi hiyo pia tangu kuanzishwa tena kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 na uchaguzi wa kwanza kwa mfumo huo kufanyika mwaka 1995.
Mkurugenzi wa Tehama wa NEC, Dk Modestus Kipilimba anasema hakuna yeyote asiye na utambulisho halali atakayepiga kura na atakayekamatwa, atachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Hairuhusiwi kutumia kadi isiyo ya NEC. Orodha ya wanaostahili kupiga kura tunayo na elimu imeshatolewa kwa wananchi kujiepusha na suala hilo, yeyote atakayekaidi atachukuliwa hatua za kisheria. Lakini kwa uhakika, hakuna uwezekano kwa mtu yeyote wa nje kufanikisha azma hiyo,” anasema Dk Kipilimba.
Katika uandikishaji huo, NEC ilitumia teknolojia ya kisasa ya BVR na kila mapigakura alipatiwa kadi mpya aina ya PVC yenye alama za kiusalama, kuongeza uwezekano wa kukamatwa kwa atakayejaribu kughushi.
Licha ya tume hiyo kukabidhi kwa Jeshi la Polisi majina ya watu 52,078 waliojiandikisha zaidi ya mara moja kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura ili hatua stahiki zifuate, NEC imebainisha pia maofisa watakaojihusisha na udanganyifu aina yoyote, nao watasombwa na dhoruba hiyo.
Wakati wa ziara ya waandishi wa habari katika Kituo cha Taarifa za Wapigakura cha NEC, ilielezwa kwamba mtumishi yeyote atakayejihusisha na uchakachuaji wa daftari hilo, atahukumiwa kifungo kisichopungua miaka saba jela.
Sheria hiyo imewekwa ili kuondoa uwezekano kwa watumishi 74,502 waliotumika katika uandikishaji nchini kujihusisha na vitendo hivyo.
“Si rahisi kuingiza maelezo ya mtu ambaye hakuwapo kituoni kwenye taarifa za NEC. Licha ya kulindwa, utaratibu uliopo unashirikisha zaidi ya mtu mmoja. Endapo kutakuwa na ‘mjanja’ yeyote, lazima tutambaini na sheria itamalizana naye,” anasema Mkurugenzi wa Uchaguzi NEC, Kailima Ramadhan.
Haki ya mpigakura
Siku tisa zimebaki Watanzania kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuchagua rais, wabunge na madiwani watakaongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Ibara ya 5 (1) ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzanania katika Kifungu cha 61(3)(a) na (b) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, vinampa kila mpigakura haki ya kupata elimu na taarifa sahihi kwa wakati, kuhusu mchakato wa uchaguzi ikiwa pamoja na kushiriki mikutano ya kampeni bila woga na kutoa maoni kwa uhuru na amani.
Sheria pia, inamruhusu kumpigia kura kwa siri mgombea anayemtaka bila bugudha, vitisho au woga na kulalamika juu ya mwenendo mbaya wa uchaguzi.
Kwa watu wenye ulemavu, wagonjwa au wazee, sheria hiyo inatoa haki ya kusaidiwa kupiga kura. Vilevile, NEC imeandaa vifaa ili kuwawezesha walemavu hasa wasioona kutimiza wajibu huo wa kidemokrasia bila msaada wowote.
Hata hivyo, ni vema mpigakura akajilinda dhidi ya matukio ya uvunjifu wa sheria, taratibu na kanuni siku ya uchaguzi huo.
Matukio hayo ni pamoja na kufanya kampeni ya aina yoyote siku hiyo na kupokea rushwa kwa ajili ya kupiga au kuacha kupiga kura. Wananchi pia wanakumbushwa kuepuka kupokea chakula, vinywaji au takrima kwa ajili ya kupiga au kutopiga kura.
“Ni kosa kupiga au kujaribu kupiga kura zaidi ya mara moja, kununua, kuuza, kutoa kadi kwa mtu mwingine au kumshawishi mtu asiye na sifa kupiga kura. Haitoruhusiwa kutumia jina la aliyefariki au jina la uongo na kufanya kampeni au kuvaa alama za chama cha siasa ndani ya mita 200 kutoka kituo cha kupigia kura,” anasema Ramadhan na kuongeza:
“Tuliandikisha watu zaidi ya watu milioni 23.7 na baada ya uhakiki na uchakataji wa taarifa zote wamebaki milioni 22.75, hao ndiyo watakaoshiriki uchaguzi huu. Mtu asiyependa matatizo ni vema akajiepusha na watu wenye dhamira mbaya kama kughushi kadi.”
Ni jinai
Ili ufurahie ushindi wa mgombea utakayemchagua na kuendelea kuwa salama hata baada ya Oktoba 25 ni busara na hekima kuepuka kuvunja sheria kwani ulinzi utakuwa wa kutosha maeneo yote wakati mchakato wa upigaji kura ukitekelezwa.
Maelekezo ya NEC kuhusu upigaji kura kila mpiga kura kukumbuka kituo alichopangiwa kupigia kura kulingana na alikojiandikisha, ni mahali ambako jina lake litabandikwa na kuruhusiwa kupiga kura.
Ikiwa siku ya kupiga kura jina halitaonekani katika orodha iliyobandikwa kituoni, kuna uwezekano mpigakura huyo amekwenda kituo ambacho hakujiandikisha wakati wa uboreshaji wa BVR, hivyo ndiyo sababu NEC hubandika orodha kituoni kabla ya uchaguzi ili kuondoa utata huo na kila mwananchi kujihakikishia yumo kwenye orodha ya wapigakura.
-chanzo;Mwananchi mobile
Powered by Blogger.