ACT waahidi kuzalisha umeme wa upepo

Mgombea urais wa ACT- Wazalendo Anna Mghwira akihutubia wananchi katika mkutano wa kampeni .

Singida. Mgombea urais wa ACT- Wazalendo Anna Mghwira, ameahidi kuutumia upepo wa Mkoa wa Singida kuzalisha umeme wa uhakika.
Mghwira alisema hayo jana alipozungumza na wakazi wa Singida Mjini na kuongeza kuwa ni ndoto kuwa na nchi ya viwanda bila ya umeme na maji ya uhakika.
Alisema badala ya kutegemea umeme wa maji ambao umeonyesha kushindwa, inahitajika nguvu ya ziada kuhakikisha nishati hiyo inapatikana kwa kutumia vitu mbadala ukiwamo upepo wa Singida unaopotea bure.
“Nakumbuka miaka ya 1980, kulikuwa na mradi wa umeme wa upepo, kutokana na kutokuwa na mipango endelevu ya maendeleo, ilikufa. Sasa ACT- Wazalendo itahakikisha inaifufua ili iende sambamba na upatikanaji wa umeme wa uhakika,” alisema Mghwira.
Alisema mbali ya viwanda watahakikisha kunakuwa na kilimo shirikishi kwa maana ya kusaidia maendeleo na siyo kwa ajili ya chakula pekee.
Mghwira alisema kilimo hicho kitamuhusisha mkulima wa kawaida na Serikali kwa utaratibu maalumu kupitia sera na kanuni za ACT -Wazalendo.
“Kinachowatesa na kuwapa hasira wananchi ni uwazi, vitu vingi vinafanywa kwa siri na kuwanufaisha wachache. Serikali ya itaweka kila kitu bayana ili kuondoa ukakasi huo unaokatisha tamaa kwa kuwakandamiza wengi,” alisema Mghwira.
Kuhusu elimu, alisema wamejipanga kuwajali zaidi walimu kwa sababu wao ndiyo chimbuko la kuwapo shule na wasomi wanaoisaidia nchi katika masuala mbalimbali. Alisema bila kuwajali walimu kwa kuzingatia madai yao ikiwamo nyumba, kulipwa kwa wakati na kupata vitendea kazi, haitakuwa rahisi kuwa na wahitimu wanaoweza kupambana katika soko la ajira.
“Walimu watakuwa na nafasi nzuri ya kujadili, kuwasilisha maoni yao na kusikilizwa, huku mahitaji yao muhimu yakipewa kipaumbele,” alisema Mghwira.
Mgombea mwenza wa ACT-Wazalendo, Hamad Yusuph aliwaomba wananchi kumpigia kura Mghwira ili alete mabadiliko ya kweli. Alisema wananchi wamechoka kudanganywa na huu ndiyo wakati wa kufanya uamuzi sahihi.
-
Powered by Blogger.