Ukawa wavutana mgombea ubunge Nzega Vijijini

Mgombea Mwenza wa Ukawa kupitia Chadema, Juma Haji Duni akihutubia wananchi .
Tabora. Ziara ya Mgombea mwenza urais kwa tiketi ya Chadema kupitia Ukawa, Juma Duni Haji imeingia dosari baada ya viongozi na wafuasi wa vyama hivyo ndani ya jimbo la Nzenga Vijijini kutoridhiana mgombea atakayewakilisha jimbo hilo.
Hivi karibuni, Ukawa ilipitisha jina la Khamis Katuga(CUF), kuwakilisha jimbo hilo kwa umoja wa Ukawa lakini mgombea wa Chadema, Joseph Malongo alikataa uamuzi huo.
Kabla ya kutambulishwa Katuga mbele ya wafuasi hao, Duni alimwomba apande jukwaani na ndipo kundi la wafuasi wengi lilianza kupinga utambulisho huo.
Duni aliwataka wafuasi hao wampokee na kumpigia kura ili Kumshinda mgombea kutoka CCM,Dk Khamis Kigwangalla.
Kila alipojaribu kuwaomba utulivu vijana wengi walikataa na hata alipowasalimia kwa lugha ya vyama hivyo walipiga kelele za kumtaka mgombea wa Chadema.
"Naomba mumchague huyu ndiye aliyepitishwa na vikao vya Ukawa, tunatakiwa umoja wetu na lengo ni maslahi ya kuiondoa CCM madarakani,"alisema Duni.
Licha ya kutumia muda mwingi kufafanua uamuzi huo, bado haikusaidia hatua iliyomkwaza Duni na kushuka juu ya jukwaa hilo.
Tukio hilo limetokea jana majira ya saa 9:30 jioni katika Uwanja wa taifa,uliopo Kata ya Ndalla, Nzenga vijijini.
Baada ya kushuka Duni, mgombea huyo wa Chadema alipanda jukwaani huku akishangiliwa na wafuasi wengi uwanjani hapo.
Baadhi yao walisema wako tayari Ukawa ivunjike katika jimbo hilo lakini hawatakubali kuunga mkono mgombea wa Cuf.
"Uamuzi uliopitishwa na viongozi hatuwezi kukubaliana nao, haujatenda haki, sisi tunamtaka Malongo basi, Ukawa wamchukue mgombea wao waliyetuletea,"alisema Bernard Samwel ambaye ni mkazi wa jimbo hilo.
-
Powered by Blogger.