Uhusiano wa Sintaksia na Matawi mengine ya Isimu

 

Uhusiano wa Sintaksia na Matawi mengine ya Isimu



Dhana ya sintaksia imejadiliwa na wanazuoni mbalimbali ;
            Massamba na wenzake (1999:34) anasema “sintaksia ni utanzu wa sarufi unaojihusisha na uchunguzi wa mpangilio wa maneno katika sentensi na uhusiano wa vipasho vyake”. Wanaendelea kusema, utanzu huu huchunguza sheria  au kanuni zinazofuatwa katika kuyapanga maneno ili yalete maana inayokubalika na kueleweka katika lugha husika.
           Habwe na Karanja (2004) wanasema “sintaksia ni utanzu wa isimu unaoshughulikia muundo wa sentensi na elementi nyingine zinazounda sentensi kama vile kategoria za maneno, vikundi na vishazi”
        TUKI (2004)anasema “sintaksia ni tawi la isimu linaloshughulikia uchanganuzi wa taratibu na kanuni za mahusiano baina ya maneno katika tungo” kwa ufupi sintaksia ni tawi la isimu ambalo linachunguza muundo wa tungo pamoja na uhusiano wa vipashio hivyo vinavyounda tungo ambayo ni nukta pacha, neno, kirai na kishazi.
           Kwa ujumla sintaksia ni tawi la isimu ambalo linahusu namna maneno yanavyoungana na kuhusiana kirai, kishazi na sentensi. Sintaksia inachunguza namna maneno yanavyojipanga katika sentensi kwa kuzingatia kanuni za sarufi ya lugha husika.
         Kwa hiyo kutokana na kwamba sintaksia pia ni kitengo mojawapo kinachounda maarifa ya lugha, kwamba, sintaksia haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Vitengo hivi hutegemena na kuathiriana. Hivyo basi tunaweza kuonesha jinsi sintaksia isivyoweza kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha yaani fonolojia, mofolojia na semantiki kama ifuatavyo:
Uhusisno uliopo kati ya sintaksia na fonolojia.
          Massamba na wenzake (1999:34) wanasema “fonolojia ni uchambuzi wa mfumo wa sauti katika lugha mahususi” Ni jinsi ambavyo vitamkwa au sauti za lugha zinavyoungana ili kujenga maneno yanayokubalika katika lugha. Ni dhahiri kwamba kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na fonolojia kwa sababu hatuwezi kuwa na miuundo mikubwa bila kuwa na mpangilio sahihi wa sauti katika lugha.
Mfano 1. ‘anacheza’ hili ni neno lakini pia ni sentensi, hivyo linaweza kuchanganuliwa            kifonolojia kama, /a/n/a/ch/e/z/a/. kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti hizo ndizo zinazounda neno ‘anacheza’.
Mfano 2 (a). neno “debe” neno hili limeundwa na konsonanti irabu konsonanti irabu (KIKI).
           2. (b). “edbe” hili limeundwa na irabu konsonanti konsonanti irabu (IKKI).
Katika mfano 2a, neno “debe” lina maana na limefuata kanuni na mpangilio unaokubalika katika lugha ya Kiswahili, lakini katika mfano 2b neno “edbe” halina maana katika lugha ya Kiswahili kwa sababu halina mpangilio sahihi wa vitamkwa au fonimu.
Kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti katika maneno ndio husaidia kupata vipashio vikubwa zaidi katika lugha kama vile kirai, kishazi na sentnsi. Kwa hiyo sintaksia na fonolojia haviwezi kuenganishwa.
Uhusiano uliopo kati ya sintaksia na semantiki.
        Habwe na Karanja wakimnukuu Richard na Wenzake (1985) wanasema “Semantiki ni stadi ya maana. Semantiki ni utanzu unaochunguza maana katika lugha ya mwandamu”. Wanaendelea kusema semantiki hutafiti maana za fonimu, mofimu, maneno na tungo. Hivyo kutokana na fasili hii maana hushughulikiwa katika vitengo au viwango vyote vya lugha ambavyo ni fonolojia, mofolojia na sintaksia. Kwa mfano,
1               Mtoto mtiifu amefaulu mtihani.
2                Mtihani mtoto amefaulu mtiifu.
3              Mtiifu mtoto mtihani amefaulu.
Katika mifano hii sentensi (1) ina maana kutokana na kwamba imefuata mpangilio sahihi wa maneno katika tungo na sentesi zilizobaki hazina maana kutokana na sababu kwamba hazijafuata mpangilio ulio sahihi wa kimuundo katika lugha ya Kiswahili. Kwa mantiki hii, kwa kuwa semantiki hushughulikia viwango vyote vya lugha, basi hushughulikia pia kiwango cha sintaksia ambapo huangalia maana za tungo, kwani tungo lazima ikubalike kwa wazungumzaji wa lugha husika, pia tungo lazima ilete maana. Kwa mantiki hiyo kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na semantiki kwa sababu mpangilio sahihi wa maneno katika sentensi ndiyo huleta maana na bila mpangilio sahihi wa maneno maana hupotea.
Uhusiano uliopo kati sintaksia na mofolojia.
        Besha (2007:49) anasema “mofolojia ni taaluma inayojishughulisha na kuchambua muundo wa maneno katika lugha’.Pia Rubanza (1996:1) anasema “mofolojia ni taaluma inayoshughulikia vipashio vya lugha katika kuunda maneno”. Maumbo ya kimofolojia huathiri vipengele vingine vya kisintaksia kama vile kipengele cha umoja na wingi, katika maumbo ya kimofolojia ndicho kinachoathiri umbo linalofuata jina na kuathiri muundo wa sentensi nzima. Kwa mfano,
1                        Mtoto alikuwa anajifunza kusoma.
2                        Watoto walikuwa wanajifunza kusoma.
Katika mifano hii kiambishi m- na wa- katika upande wa kiima vimeathiri utokeaji wa viambishi a- na wa- katika upande wa kiarifu. Hivyo taaluma ya sintaksia na mofolojia haziwezi kutenganishwa.
            Kwa ujumla sintaksia kama tawi mojawapo la isimu linauhusiano wa moja kwa moja na matawi mengine kwani haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Hutegemeana na kuathiriana kwa kiasi kikubwa, mfano huwezi kupata mofolojia bila kupitia ngazi ya fonolojia na pai huwezi kuwa na ngazi ya sintaksia bila kupitia ngazi ya fonolojia na mofolojia lakini vitengo vyote hivi hutawaliwa na kitengo cha semantiki ili kuleta mawasiliano miongoni mwa wazungumzaji.
                                          MAREJEO
Besha, R.M. (2007). Utangulizi wa Lugha na Isimu. Dar es Salaam: Mackmillan Aidan
Habwe, J na P. Karanja (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd.
Massamba, D.P.B na wenzake (1999). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu: Sekondari na Vyuo.          Dar essalaam: TUKI.
Rubanza, Y.I (1996). Mofolojia ya Kiswahili. Dar es salaam: Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.
TUKI (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es salaam: TUKI.
Powered by Blogger.