Mbinu za uundaji wa istilahi katika Kiswahili


 LUGHA huundiwa istilahi ili utamaduni wake ukidhi dhana ambazo hapo awali zilikuwa hazimo katika utamaduni huo.
Aidha, maendeleo ya kasi ya sayansi na teknolojia ndiyo kichocheo cha kimsingi katika uundaji wa istilahi – ingawa sicho kiini cha pekee.
Katika makala ya leo, tutajadili mbinu ambazo wanaleksikoni hutumia katika kuunda istilahi za lugha.
Mwandishi Enock Nyariki alitaja baadhi ya mbinu hizo (Taifa Leo, Desemba 30, 2015).
Wanaleksikoni wa Kiswahili kama vile Patricia Mbughuni, Zubeida –Tumbo Masabo, Hermans Mwansoko na John Gongwe Kiango (wote kutoka Tanzania), Mzee Sheikh Ahmad Nabhany, Rocha Mzungu Chimerah na Kyallo Wadi Wamitila (wa Kenya) wametumia mbinu zifuatazo katika kukiundia Kiswahili istilahi na msamiati mpya.
Hizi ni pamoja na takriri au uradidi, upanuzi wa maana, utohozi, tafsiri, ufupishaji, uhulutishaji, uambatanishaji, ubunifu na uingizaji wa maneno ya lahaja ya lugha za Kibantu katika Kiswahili.
Mwandishi Enock Nyariki alitaja mbinu za uradidi na upanuzi wa maana.
Neno 'nyokonyoko’ alivyosema Bw Nyariki limetokana na uradidi wa neno 'nyoko’ ambalo maana yake ni mzazi wa kike au nina.
Katika Kiswahili, kuna misemo ya 'kumanyoko’ na 'kumanina’ ambayo aghalabu ni matusi.
Mzee Jomo Kenyatta alipenda sana kutumia neno 'nyokonyoko’ kwa maana iliyozua fahiwa ya kuwakomesha watu wasilete mchezo au wasithubutu - au kitu kama hicho.
Kuna msamiati kama vile 'kimbelembele’ 'kijingajinga’ na kadhalika ambao umetokana na uradidi.
Katika mbinu ya upanuzi wa maana, maana ya awali ya neno hupanuliwa na kuhusishwa na maana nyingine.
Maana ya kileksika ya neno 'sakata’ kwa mfano: ni kufanya jambo kwa umahiri au hali ya mgogoro au ghasia.
Hata hivyo nchini Kenya, vyombo vya habari vimepanua maana ya neno hili na kulitumia kutajia kashfa kama vile Goldenberg, Anglo-Leasing au hata Eurobond.
Mbinu ya utohozi huhusisha kuyapatia maneno yaliyokopwa kutoka kwa lugha nyingine matamshi na maandishi ya lugha inayokopa.
Kwa mfano 'wakti (Kiarabu) huwa 'wakati’ (Kiswahili); 'Television’ (Kiingereza) huwa 'televisheni’ (Kiswahili) na kadhalika.
Mbinu ya kutafsiri
Katika mbinu ya kutafsiri, neno lililokopwa huelezwa kwa lugha nyingine; kwa mfano. 'secondary school’ huwa 'shule ya upili’.
Katika mbinu ya ufupishaji, wanaleksikoni hutumia akronimu za sehemu ya kwanza ya maneno mawili au zaidi na kuziunganisha ili kupata neno jingine.
Mfano mzuri ni: Upungufu wa Kinga Mwilini (Ukimwi).
Nayo mbinu ya uhulutishaji (hybdidisation) huhusisha uunganishaji wa visehemu mbalimbali vya maneno mawili au zaidi ili kubuni neno moja mahuluti.
Mzee Sheikh Nabhany wa Mombasa amebuni neno 'runinga’ kutokana na maneno Rununu + Maninga.
Katika Kiswahili cha zamani kwa mujibu wa Mzee Nabhany, 'Rununu’ ni sauti inayosikika kutoka mbali’ ilhali 'Maninga’ ni macho.
Aidha wanaleksikoni huambatanisha maneno mawili ili kuunda neno moja.
Kwa mfano 'isimu’ + 'Jamii’ tunapata 'isimujamii’.
Kiswahili na lugha nyingine za Kibantu ni lugha 'ambishibainishi’ (agglutinative language).
Kwa sabababu hiyo, viambishi huweza kupachikwa mwanzoni au mwishoni mwa mizizi ya maneno ili kuunda maneno tofauti.
Kutokana na neno 'utandawazi’ tunaweza kupata maneno kama vile 'tandawazisha’, 'utandawazishaji’ miongoni mwa mengine.
Katika mbinu ya kubuni, wataalamu wa istilahi huangalia sifa za kimaumbile, sifa za kitabia na sifa za kimatumizi ambazo huwaongoza katika kubuni maneno na istilahi mpya.
Mwandishi Enock Nyariki anaonekana kuwa na tatizo na mbinu hii – ingawa sababu alizotoa katika makala yake kutoridhishwa na mbinu hii hazikuwa za kitaalamu.
Mwisho, tuna mbinu ya uingizaji wa maneno ya lugha nyingine za Kiantu katika Kiswahili.
Maneno yafuatayo yemeingizwa katika Kiswahili kutoka kwa lahaja za Kiswahili pamoja na lugha nyingine za Kibantu: 'njeo’ (Kiamu, Kenya), 'ngeli’ (Kihaya, Tanzania), 'kitivo’ (Kipare, Tanzania), 'Bunge’ (Ha, Tanzania), 'githeri’ (Kikuyu, Kenya) na kadhalika.
Mzee Sheikh Ahmad Nabhany ni mmoja wa wataalamu wa Kiswahili wanaounga mkono mbinu hii.
Enock Matundura ni mhadhiri wa Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Chuka
Powered by Blogger.