Ufeministi, itikadi na misingi yake (8)

Ufeministi, itikadi na misingi yake (8)
Ufeministi, itikadi na misingi yake (8)
Karibuni kuwa nasi tena katika sehemu ya 8 ya kipindi cha Ufeministi, Itikadi na Misingi Yake. Katika kipindi cha wiki iliyopita tulizungumzia baadhi ya misingi ya kifikra ya ufeministi ikiwa ni pamoja na kupuuza tofauti za kimaumbile ya kibiolojia za mwanamke na mwanaume na vilevile itikadi ya kuwapiga vita wanaume. Tulisema baadhi ya mafeministi wanaokana suala la kuwepo tofauti za kimaumbile kati ya mwanamke na mwanaume wanamtambua mwanaume kuwa ni adui mkuu wa mwanamke na wanasisitiza juu ya udharura wa kupambana naye. Tulisisitiza kuwa fikra hii inapingana na itikadi na mafundisho ya Uislamu unaomtambua mwanamke na mwanaume kuwa wanakamilishana ndani ya familia na katika jamii. Kipindi chetu cha leo kitaendelea kuzungumzia itikadi za kifeministi na kukosoa misingi ya mrengo huo katika mtazamo wa dini ya Uislamu.  >>>>>  <
Miongoni mwa misingi ya kifikra ya ufeministi ni kupinga na kutupilia mbali mafundisho ya dini. Mafemenisti wanayaona mafundisho ya dini kuwa yanachangia katika kuimarisha utamaduni wa mfumo dume, kwa msingi huo wanaamini na kufuata thamani za kimaada na kupinga thamani za kidini. Wanasema thamani na mafundisho ya dini ndiyo kizuizi kikuu katika njia ya kufikiwa malengo yao kwani wanaamini kuwa dini za Mwenyezi Mungu zinathamini na kutukuza sana familia na nafasi ya mama, na ili kulinda nafasi hiyo zinamzuia mwanamke kushiriki katika baadhi ya mambo ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kadhalika. Vilevile wanasema dini zinashajiisha na kuhamasisha uzazi na kuzaa, na zinakataza kuavya mimba na kuwalazimisha watu kuzilinda na kulitambua suala hilo kuwa ni sawa na kulinda nafsi ya mwanadamu mzima. Suala hili- wanasema mafeministi- linawaelekeza wanawake katika kuzaa na kujizuia kuavya na kutoa mimba. Hata hivyo kwa mtazamo wa mafeministi, kulindwa thamani na mambo kama haya ndiyo kizuizi kikuu cha uhuru wa mwanamke katika suala la maingiliano ya ngono na kupata burudani na anasa; hivyo basi kuna haja ya kufanyika jitihada za kujiweka mbali na thamani na mafundisho ya dini!
Inasikitisha kwamba, mafeministi wanaghafilika kwamba, kadiri unavyojiweka mbali na kujitenga na dini na masuala ya kiroho ndivyo unavyopata hasara zaidi. Hii leo mfumo wa familia umekumbwa na mgogoro katika jamii ya Magharibi. Wanafikra na wasomi wengi wanaamini kuwa, miongoni mwa sababu za mgogoro huo ni kujitenga na kuwa mbali na mafundisho ya dini na masuala yaa kiroho. Mwandishi wa Marekani, Patrick J. Buchanan, anasema waziwazi katika kitabu alichokipa jina la “Kifo cha Magharibi” kwamba: Magharibi imo katika hali ya kugawanyika, kutoweka na kufa. Anasema ubinafsi, kutojenga na kuanzisha familia, kutozaa watoto, kuongezeka kiwango cha utoaji wa mimba, talaka, vitendo vya kuingiliana kinyume na maumbile na kujamiiana watu wenye jinsia moja, utumiaji uliokithiri wa dawa za kulevya, jinai za kutisha zinazohusiana na masuala ya ngono na kadhalika katika nchi za Magharibi vinatokana na kusambaratika mfumo wa familia na masuala ya kiroho. Kwa mfano tu, mwandishi Buchanan anasema kuhusiana na suala la kuzaa kwamba: Kuanza kuzama na kutoweka Ukristo katika nchi za Magharibi kulifuatiwa na tukio jingine. Watu wa Magharibi waliacha kuzaa watoto kwa sababu kuna mfungamano baina ya imani ya dini na kuwa na familia zenye jamii kubwa, na kadiri watu wanavyoshikamana na dini ndivyo kiwango cha kuzaa watoto kinavyoongezeka”, mwisho wa kunukuu.
Mafemenisti wamefanya jitihada za kueneza na kuhubiri misingi yao ya kifikra katika jamii kupitia nadharia za malezi ya kimaada. Wanaamini kuwa mtazamo jumla wa jamii nyingi unawadunisha wanawake na kuwafanya watu wa daraja la pili. Kwa msingi huo wanasisitiza juu ya kubadilishwa mtazamo wa jamii kuhusu wanawake na kufutwa ubaguzi unaolenga jamii hiyo. Hapa inatupasa kusema kuwa, kila mtu mwenye insafu anajua kwamba, mijadala inayohusiana na haki za wanawake na mafeministi na wito wa kufanyika mabadiliko katika mtazamo unaowaona wanawake kuwa ni wanadamu wa daraja la pili katika nchi za Magharibi na vilevile juhudi za mafeministi za kupigania haki zao za kisiasa, kijamii na kichumi vimepelekea kupatikana baadhi ya mafanikio kwa maslahi ya wanawake hususan katika nchi za Magharibi. Hata hivyo suala la kupigania haki za wanawake na kupambana na ubaguzi halipasi kuwa kisingizio cha kutokomeza na kuua maana ya maisha, kumdunisha mwanaume katika jamii na kulazimisha haki na majukumu sawa na yanazofanana licha ya tofauti za kimaumbile baina ya jinsia mbili za wanadamu.     >>
Kinyume na dhana za mafeministi, thamani, matukufu na majukumu ya kimaumbile na kaida zilizokubalika na mwanaume na mwanamke zinasaidia sana katika kuimarisha zaidi mfungamano wa ndoa. Kwa sababu hiyo katika familia ambazo wanaume hukosa hadhi na thamani, uwezekano wa wanaume kukimbia majukumu yao ya kusimamia familia pia huwa mkubwa zaidi. Vilevile kila majmui na kundi lenye uongozi na utaratibu mzuri linaweza kufikia malengo yake vizuri na vyema zaidi. Uongozi ndani ya familia pia ni sehemu ya dharura ya uongozi wa jamii yenye malengo ambayo wanachama wa familia husika wanapaswa kushikamana nayo ili kuweza kupiga hatua za maendeleo ya kimaada na kiroho. Iwapo nyumba na familia haitakuwa na mudiri na kiongozi, na mke na mume wakawa sawa katika kuongoza maswala ya familia, hapana shaka kwamba watalazimika kwenda mahakamani mara kwa mara kwa ajili ya kusuluhisha hitilafu zao au kutoka nje ya familia kutafuta utatuzi, suala ambalo si rahisi kuwezekana wakati wote. Suala hilo huwa sababu ya kuzorota uhusiano wa kifamilia. Msingi wa mantiki na akili ni kuwepo mudiri na mwendeshaji wa masuala ya nyumba na familia mwenye ustahili. Na kwa kuwa aghlabu na kwa ujumla mwanaume huwa na uwezo mkubwa wa kusimamia masuala mbalimbali ya familia na vilevile kukabiliana na mikikimikiki na changamoto za aina mbalimbali, huwa ndiye kiongozi na msimamizi wa masuala ya familia kiujumla. Suala hili linaashiriwa katika aya ya 34 ya Suratul Nisaa inayosema: Wanaume ni wasimamizi wa wanawake, kutokana na fadhila alizowapa Mwenyezi Mungu baadhi yao juu ya baadhi…”. Ni wazi kwamba, wanaume kwa ujumla ni bora zaidi kuliko wanawake katika masuala ya uendeshaji wa masuala ya kiuchumi, kijamii, uwezo wa kulinda familia na kadhalika. Hata hivyo ubora huu wa kiujumla hauna maana ya ubora wa kidhati wa mwanaume juu ya mwanamke kwa sababu mwanamke na mwaname wanashirikiana katika dhati ya ubinadamu na katika uwezo wa kufanya jitihada za kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu, suala ambalo halihusu jinsia ya mtu. Katika upande mwingine tunapaswa kuelewa kwamba, Uislamu umemlazimisha mwanaume kudhamini mahitaji yote ya mwanamke na familia na mkabala wake amepewa pia majukumu ya kusimamia na kuendesha masuala ya familia yake.
Katika mtazamo wa Uislamu maslahi ni kumwepusha mwanamke kadiri ya uwezo kufanya kazi ngumu na nzito na kumbebesha mwanaume jukumu la kudhamini na kukidhi mahitaji ya kimaisha ili mwanamke aweze kutekeleza ipasavyo majukumu yake kama mke na mama. Hali hii huifanya familia kuwa kituo chenye utanashati, upendo na mahaba.
Miongoni mwa itikadi za kifemenisti ni kugeuza kabisa nafasi za wanaume na wanawake. Mafemenisti wanaamini kuwa, nafasi na mchango wa wanaume na wanawake katika jamii na familia zinapaswa kuarifishwa upya kwa mujibu wa usawa kamili baina ya jinsia hizo mbili kwa sababu -kwa mtazamo wao - hakuna tofauti yoyote kati ya wawili hao. Kwa mtazamo wao, itikadi kwamba kazi nzito na za kiufundi zinapaswa kufanywa na wanaume na kwamba wanawake wanapaswa kufanya kazi nyepesi na za kuvutia, inapaswa kubadilishwa. Hata hivyo katika mtazamo wa Uislamu mwanaume na mwanamke hawafanani katika pande nyingi kwa sababu wanatofautiana katika mambo mengi ya kimaumbile. Kwa msingi huo ni makosa kuwapa watu wanaotofautiana kimaumbile kazi sawa na majukumu yanayofanana. Kwa maana kwamba, kutofautiana katika sifa za kimaumbile kunapaswa kufuatiwa na kutofautiana katika majukumu na nafasi ya jinsia hizo mbili.     >
Kipindi chetu kinaishia hapa kwa leo. Msikose kufuatilia mfululizo wa kipindi hiki wiki ijayo.
                    
Powered by Blogger.