Misingi ya Uhakiki katika Fasihi ya Kiswahili


Cover Image East African Development Library
 Fasihi, Uandishi na Uchapishaji (Dar Es Salaam University Press, 1993, 260 p.)
close this folder
SEHEMU YA TATU: UHAKIKI
View the document
11. Mhakiki, Uandishi na Jamii
View the document
12. Misingi ya Uhakiki katika Fasihi ya Kiswahili
View the document
13. Mchango wa Wanawake Katika Maendeleo ya Ushairi wa Kiswahili Katika Kipindi cha Urasimi (1600 - 1900)
View the document
14. Mwanamke ni Ibilisi?
View the document
15. Hisia Katika Fasihi Andishi
View the document
16. Mwandishi wa Riwaya ya Kiswahili na Suala la Ukweli wa Maisha
View the document
17. Uchawi katika Riwaya za Kiswahili
View the document
18. Mchango wa Waandishi wa Riwaya
View the document
19. Matumizi ya Dhana na Sanaa za Maonyesho za Jadi katika Tamthiliya za Leo

11. Mhakiki, Uandishi na Jamii


J.L. Mbele
Tumezoea kumfikiria mhakild kama mtu anayehusika sana na ukuaji, ustawi, na ueneaji wa fasihi na kazi zingine za sanaa. Lengo la makala haya ni kuichunguza fikra hiyo, ili kujaribu kuielewa zaidi nafasi ya mhakiki katika uandishi na jamii.
Njia moja ya kuielewa nafasi ya mhakiki katika uandishi ni kuitafiti historia ya uhakiki, kujaribu kuelewa jinsi mhakiki alivyojitokeza kama mtaalamu wa fasihi, tofauti na msanii mwenyewe. Swali muhimu hapa ni, je, wahakiki walikuwepo tangu fasihi ilipoanza? Yaelekea kuwa wahakiki kama kundi la watu tofauti na wasanii wenyewe hawakutokea wakati ule fasihi ilipoanza. Walitokea baadaye. Kabla ya wahakiki kuwepo, wasanii wenyewe ndio waliokuwa wahakiki. Hadi leo, wasanii hawajaacha kuwa wahakiki. Katika kuitunga kazi ya sanaa, msanii hujiuliza maswali, hujikosoa, na hivyo kuirekebisha kazi yake, mpaka anaporidhika nayo. Mara kwa mara msanii huishia kutoridhika na kazi yake, akaizuia isionekane na jamii, na pengine huiharibu kabisa na kuitupilia mbali. Kwa upande mwingine, jamii nayo daima imekuwa ni mhakiki wa kazi za sanaa. Wanajamii huihakiki kazi ya sanaa kulingana na viwango vyao mbalimbali. Ni wazi, basi, kuwa wadhifa wa mhakiki umeshikiliwa tangu zamani na watu wote wahusikao na kazi ya sanaa, na sio wahakiki peke yao. Msanii na jamii nao ni wahakiki; jambo hilo lafaa kuzingatiwa, maana linapuuzwa au kusahauliwa.
Kutokea kwa kundi la wahakiki ambao walikuwa tofauti na wasanii lilikuwa ni zao moja la maendeleo ya mgawanyiko wa kazi katika jamii. Historia ya mgawanyiko huu ni ndefu, na hatuwezi kuijadili hapa, lakini ndiyo iliyosababisha kuwepo kwa wanasayansi, wanafalsafa, wahunzi, waandishi, wahakiki na kadhalika. Mgawanyiko huu bado unaendelea. Hata katika uwanja wa uhakiki wenyewe tunaona maendeleo ya mgawanyiko huu; leo tunao sio tu wahakiki, bali pia wahakiki wa wahakiki. Hata wakati mwingine husemekana kuwa wahakiki ni wengi kuliko waandishi.
Kundi la wahakiki lilitokea likiwa na shughuli ya kuichambua kazi ya sanaa na kutoa nadharia ya sanaa yeyewe. Kwa kuwa watu hao walipata uzoefu mkubwa katika kazi hiyo, walifanikiwa kutoa mawazo mengi muhimu kuhusu kazi za sanaa, na pia kuitajirisha nadharia ya sanaa. Mhakiki wa kale wa Kigiriki, Aristotle, alifanikiwa kutoa nadharia kuhusu sanaa za ushairi na tamthilia kwa kuzichunguza kazi za sanaa za wakati wake. Kwa mfano, kwa kuzichunguza tendi za msanii maarufu Homer, aliweza kutoa nadharia juu ya tendi - muundo wake, namna zinavyowasilisha mawazo, hisia na dhamira zake, na namna zinavyowaathiri watazamaji.1
Hata hivyo, kuzuka kwa wahakiki, watu ambao si wasanii, watu waliojiweka baina ya msanii na jamii kwa madhumuni ya kuieleza kazi ya sanaa kwa jamii, kulizua masuala ya kutatanisha. Tatizo moja lilikuwa lile la kujihalalisha. Je, mhakiki ni mtu anayehitajika kweli, au amejipachika tu hapo alipo? Ni kweli kuwa anamsaidia msomaji? Kama jibu ni ndiyo, kwa kiwango gani? Wahakiki wanasema kuwa wanamsaidia pia mwandishi. Je kuna ukweli katika rai hiyo? Wahakiki wanasema kuwa wao ni kiungo kati ya mwandishi na jamii. Swali ni, je, bila kuwepo hao wahakiki, uhusiano kati ya mwandishi na msomaji ungezorota au kupotea kabisa? Maswali kama haya yamewakera wahakiki, na kuwafanya wajaribu kujihalalisha. Hata kule kujiuliza au kuyajadili maswali kama hayo sio jambo la kawaida kwa wahakiki. Kimya hiki nacho ni mbinu ya kujipatia nafasi ya heshima, maana kuyajadili maswali hayo kungeweza kutoa mambo hadharani juu ya nafasi ya wahakiki ambayo wahakiki wenyewe hawangependa yatoke.
Juhudi za kujihalalisha zimewafanya wahakiki wafikie hatua ya kudai kuwa wao ni muhimu au wajuzi zaidi kuliko hata waandishi najamii. Wahakiki wamefikia hatua ya kujisema kuwa wao ni waalimu wa msanii na msomaj Mawazo ya aina hiyo yametolewa na mhakiki maarufu wa Kirusi, Lunacharsky, ambaye anasema kuwa mhakiki bora zaidi ni yule wa ki-Marx. Anasema kuwa mhakiki wa ki-Marx "kwa kiasi kikubwa ni mwalimu... katika kujaribu kumfundisha mwandishi ifaavyo, mhakiki wa ki-Marx lazima pia amfundishe msomaji. Naam, msomaji lazima afundishwe kusoma."2
Lunacharsky anamwona mhakiki kama huyu kuwa ni mtu anayetuta hadharisha kuhusu sumu inayonoga, anayetuvumbulia vito vilivyofichika, na kadhalika.3 Kwa misingi hiyohiyo Fikeni Senkoro, mhakiki anaveonekana kuathiriwa na mawazo ya Lunacharsky. anasema:
Mhakiki huifunza jamii namna ya kupokea na kuifurahia kazi ya sanaa na uandishi. Kazi ya sanaa ya uandishi ni kama chakula kilichokwishapikwa na kuungwa vizuri. Uhakiki ni sehemu mbalimbali za ulimi zenye kuifanya jamii iukubali utamu wa chakula hicho, iuchukie uchungu wa chakula hicho au ukali, na iugundue utepetepe wa chakula hicho4
Maoni hayo ya Lunacharsky na Senkoro ni ya kuwatukuza wahakiki kupita kiasi. Mtu anaposikia maneno hayo anaweza kudhani kuwa mwananchi wa kawaida akishanunua riwaya au kazi nyingine ya fasihi huzunguka au hupaswa azunguke huko na huko akimtafuta mhakiki wa kumsomesha kazi hiyo. Ukweli ni kwamba yeyote anayenunua riwaya kama hiyo hujikalia chini akajisomea. Kila msomaji ana uwezo wa kuielewa kazi ya fasihi, ingawa namna ya kuielewa huwa ni tofauti kwa wasomaji mbalimbali. Wananchi wa kawaida hawasomi tahakiki zetu. Aghalabu tahakiki hizo hazina ladha kama kazi zenyewe za fasihi. Kutokana na hali hii, sisi wahakiki tunalazimika kutumia mabavu kuwafanya raia wasome tahakiki zetu. Raia hao ni wanafunzi wa fasihi, a'mbao hawana njia ya kukwepa balaa hilo, maana wanatarajia kufaulu mitihani ili wasonge mbele kijamii katika mfumo huu wa kibepari tunamoishi. Hata kama mhakiki binafsi hatumii mabavu, mfumo wa elimu unatekeleza jukumu hilo barabara.
Wazo la kuwa mhakiki humfundisha msomaji kuielewa na kuifurahia kazi ya fasihi linaleta picha ya kuwa maana ya kazi ya fasihi imejificha ndani ya kazi hiyo, na kuwa mhakiki ndiye bingwa wa kuitoa maana hiyo humo ilimojificha ili watu wa kawaida waweze kuiona. Kumbe maana ya kazi ya fasihi sio kitu kilichokwisha kutengenezwa na kufungiwa katika kazi hiyo ya fasihi. Maana ya kazi ya fasihi hutokea pale msomaji anapoisoma, ni zao la juhudi ambayo msomaji huifanya wakati anaposoma kazi hiyo. Ndio maana kazi moja ya fasihi huwa na maana mbalimbali kwa wasomaji mbalimbali. Kila msomaji huweza kupata maana fulani kutokana na upeo wa mawazo yake, uzoefu wake wa kusoma kazi za fasihi, itikadi yake, hisia zake, na kadhalika. Kusema kuwa kazi ya fasihi ni kama chakula kilichokwishapikwa ni kuitweza dhana ya fasihi. Kazi ya kuisoma fasihi sio kazi ya kula tu, bali ni ya kupika pia. Kutokana na mambo hayo, tunaweza kuona kuwa maana anayoiona mhakiki katika kazi ya fasihi ni moja tu kati ya maana zinazoweza kuonekana. Wala hatuwezi kusema kuwa anachokiona mhakiki ni sahihi au bora zaidi kuliko yale yote ambayo jamii huona. Kimsingi, mhakiki ni mmoja tu kati ya wasomaji.
Wazo la kuwa wahakiki ni muhimu sana na waalimu wa mwandishi na msomaji limeota mizizi sana. Waandishi wengi mashuhuri hukubali kuwa ni wahakiki ni waalimu wa waandisni. Abdilatif Abdalla, mshairi maarufu wa Kiswahili, anakubaliana na Senkoro kuwa mhakiki ni mwalimu wa mwaiidishi na wa msomaji. Anasema kuwa ingawa mshairi anafahamu sana katika nafsi yake taratibu anazofuata katika kuandika shairi lake, anaweza kushindwa kabisa kuzieleza taratibu hizo; bali "mhakiki aliye mwelewa wa kazi yake ataweza kuziona bila ya taabu kubwa; pengine hata aweze kumtoa kombo mtunzi mwenyewe."5 Abdilatif Abdalla anakubaliana na Senkoro pia kuwa kazi ya sanaa ni kama chakula, na kuwa jukumu la mhakiki ni kumsaidia msomaji kukila chakula hicho.6
Wasanii wengi hawana wazo la kuwa mhakiki ni mwalimu wao. Wengi hujitambua kuwa wao ndio waalimu. Wazo hilo limeelezwa vizuri na msanii wa fasihi simulizi, yeli Mamoudou Kouyate wakati wa kusimulia utendi wa Shujaa Sundiata.
Mimi ni yeli. Ni mimi, Yeli Mamoudou Kouyate, mwana wa Bintou Kouyate na Yeli Kedian Kouyate, bingwa katika sanaa ya kusema... Nilipata ujuzi wangu kutoka kwa baba yangu Yeli Kedian, ambaye aliupata toka kwa baba yake; historia haina kisichojulikana kwetu; twawafundisha wajinga kiasi kile tu tunachoamua kuwafundisha. kwani ni sisi tunaotunza funguo za milango kumi na mbili ya Mali7
Mwanahistoria D.T. Niane anatueleza kuwa "milango kumi na mbili ya Mali" anayoitaja msanii huyu ni majimbo ya mwanzo kabisa ya himaya ya Mali.8 Maneno hayo ya Yeli Kouyate yanatuonyesha msanii anayejitambua kuwa yeye ndiye mwalimu. Ni maneno yanayoonyesha kujiamini kwa msanii na kujivunia ujuzi wake. Hatusikii lolote kuhusu mhakiki hapo. Uhusiano uliopo ni ule tu baina ya msanii na wasikilizaji wake.
Naye Chinua Achebe, mwandishi wa Nigeria, anasema kuwa anaiona kazi yake ya uandishi kuwa ni ile ya kuwa mwalimu wa jamii yake, jamu iliyodunishwa na kupotoshwa na ukoloni. Lengo lake ni kuifanya jamii hiyo ijitambue tena na kujiamini.9
Wahakiki kama Lunacharsky na Senkoro wanakubali kuwa mwandishi ni mwalimu, lakini bado wanampa umuhimu zaidi mhakiki. Senkoro anasema: "Japo mwandishi ni mwalimu pia, lakini yeye ni mwalimu wa jamii tu. Mhakiki anao ualimu kwa jamii na pia kwa mwandishi".10
Tatizoni kuelewa kwa nini au kwa vipi wahakiki wamejitukuza kiasi hicho, hata kuwateka mawazo baadhi ya waandishi ili nao waukubali utukufu huo wa wahakiki. Yawezekana kuwa kujitukuza huko kwa wahakiki kumetokana na hali ya kisaikolojia ya kujitambua kuwa wao ni tasa, hawazalishi fasihi; kuwa wao ni duni wakilinganishwa na waandishi ambao ndio wanaosababisha fasihi kuwepo. Haikosi kuwa wahakiki hujitambua kuwa wao humtegemea mwandishi kama kupe amtegemeavyo kiumbe mwingine. Bila waandishi, kuwepo kwa wahakiki kungekuwa mashakani, lakini waandishi wanastawi hata bila wahakiki kuwepo. Kisaikolojia, hali hii ya kujitambua kuwa ni duni au dhaifu yaweza kusababisha tabia ya ugomvi au kujitukuza kwa huyo anayejiona duni. Kujitukuza kwa wahakiki kunaweza kuwa na misingi hiyo.
Kujitukuza kwa wahakiki kunaweza kuelezwa kwa namna nyingine pia. Ninamwunga mkono Anthony Cronin aliyesema kuwa kazi ya uhakiki lu namna ya kujitafutia madaraka. Cronin anasema pia kuwa kazi bora za fasihi hazisababishwi na mawaidha ya wahakiki. Kwa maneno yake mwenyewe,
criticism is of course...a kind of politics, an attempt to escercise power. It is impossible to remember an important instance where what apoet did was a result of what a critic (who was not also a poet and usually a friend) said.11
Katika juhudi hizo za kujihalalisha, kujitukuza, na kujitatutia madaraka, wahakiki wametunika mambo ambayo yanaweza kuwapunguzia hadhi. Kama nilivyodokeza, sio kawaida kwa wahakiki kujadili suala la umuhimu wao katika uandishi kinaganaga. Hawakuthubutu kukubali kuwa hata bila wao kuwepo, fasihi ingendelea kustawi. Kukubali ukweli huo ni kujimwagia unga wao.
Kama nilivyodokeza pia, kimsingi mhakiki ni mmoja tu kati ya wasomaji. Hatuna ushahidi wa kuwa lile analosema mhakiki kuhusu kazi ya fasihi ndilo pekee sahihi, au ndilo sahihi kuliko wanayosema wengine. Hatukatai kuwa mhakiki mwenye uzoefu anaweza kuwa na upeo mpana sana kuhusu kazi ya fasihi, hasa kwa kuwa anaweza kuilinganisha kazi hiyo na kazi zingine za fasihi. Lakini hata hao wahakiki maarufu wanakuwa na upungufu wa namna fulani. Kwa mfano, mhakiki maarufu wa ki-Marx, Georg Lukacs, alizipenda kazi fulani tu za fasihi, za wakati uliopka, na wala sio zile za kimajaribio za wakati wake. Alizithamini zile alizoziona zina uhalisi wa kihistoria na kijamii. Jambo hilo lilisababisha kutokubaliana kati yake na mhakiki mwingine, ambaye pia ni msanii maarufu, Bertolt Brecht. Brecht alikuwa na fikra za kuzithamini hata zile kazi zenye fani na miundo ya kimajaribio. Tunaona kuwa Lukacs alikuwa na upeo finyu kuhusu fasihi. Mhakiki mwingme mashuhuri, F. Leavis, naye alikuwa na ufinyu huo, alizithamini kazi za fasihi za watu fulani tu, akaziona ndio fasihi halisi ya Kiingereza. Waandisbi wengi wa Kiingereza hakuwathamini.
Yawezekana pia kuwa wakati mwingine wahakiki hawazitambui au kuzisoma kazi fulani za fasihi. Huu nao ni upungufu. Kushindwa huku kwa wahakiki kuzihakiki kazi zake za fasihi kulimfanya mwandishi maarufu wa Ireland, George Bemard Shaw, aamue kuchapisha tahakiki alizoziandika yeye mwenyewe juu ya kazi zake.12
Ingawa wanadai kuwa wao ni waalimu wa mwandishi na msomaji, wahakiki mara kwa mara huwa na mawazo yaliyopotoka. Chinua Aehebe amewashutumu sana wahakiki wenye mawazo ya kikoloni, ambao wanawabughudhi waandishi.13 Naye Wole Soyinka amewashutumu wahakiki wanaopiga kelele kuwa mwandishi aiandikie jamii wakati wao wenyewe hawajiulizi wanamwandikia nani. Soyinka anadokeza kuwa mara kwa mara wahakiki hao huwaandikia watu wa kiwango chao ili wapate umaarufu na kupandishwa vyeo katika vyuo vikuu.14
Mamboyote hayo yanatuonyesha kuwa wahakiki sio miungu. Mhakiki Tigiti Sengo amewahi kusema kuwa:
Mhakiki si Mungu wa kusema kila kitu ili wengine wafuate. Hata Mungu katuheshimu sisi binadamu kwa kutuacha huru kuchagua na kujua baya na zuri. Hivyo, lazima pia ajue jinsi anavyoweza kuzungumza katika uhakiki wake na wasomaji wake. Haja na kusudi ni kupanua na mawazo wala si juu ya mtu mmoja kuwatawala kimawazo wengine.15
Katika mazingira ya leo, ambayo ni ya mfumo wa kibepari, mhakiki anajikuta katika hali ambayo hairidhishi, ingawa yeye mwenyewe anaweza asiitambue. Karl Marx na Frederick Engels walisema kuwa ubepari ulipojiimarisha umeangusha hadhi ya aina mbalimbali za kazi. Himaya ya fedha, ambao ndio ubepari, imewafanya watu wanaofanya kazi mbalimbali kuwa ni vibarua tu wa kulipwa. Hata mambo kama ndoa, ambayo twayaona yana heshima sana, yamegeuzwa na kuwa mambo yanayotawaliwa na fedha.16 Wazo hilo limejadiliwa namna hiyohiyo na wanafalsafa kama Georg Lukacs 17 na Theodor Adorno.18 Akizungumzia uhakiki, Adorno anasema kuwa katika mazingira ya ubepari, kazi ya mhakiki imekuwa ni ile ya kutangaza bidhaa, maana kazi za fasihi zimegeuzwa na ubepari kuwa ni bidhaa. Mhakiki amekuwa ni mchuuzi wa hizo bidhaa, hali ambayo imeangusha hadhi yake.19 Kwa kuzingatia hoja hiyo, tunaona kuwa kuna jukumu la kuikwamua kazi ya uhakiki na uandishi kutoka katika mfumo wa kibepari, ili waandishi waweze kupumua kwa raha na kuandika kufuatana na uhalisi wa hisi zao badala ya kuvutwa na soko la bidhaa kama ilivyo sasa, ili pia wahakiki waweze kurudia hali yao ya kuwa watafiti wenye kuipenda fasihi na wenye lengo la kushirikiana na waandishi na jamii ili wote tuweze kuifahamu na kuifurahia zaidi fasihi.
Marejeo
1. Aristotle (1985) On Poetry and Style, kimefasiriwa na G.M.A. Grube. The Bobbs - Merrilt Company, Inc., Indianapolis.
2. Anatoly Lunacharsky (1973) On Literature and Art. Progress Publishers, Moscow, uk. 18 - 19.
3. Lunacharsky, uk. 19.
4. F. Senkoro (1973) "Ndimi na Hisi za Wahakiki", Kioo cha Lugha, 3 uk. 5.
5. Abdilatif Abdalla (1975) "Utangulizi" kwa T.S. Sengo, Shaaban Robert: Uhakiki wa Maandishi Yake. Longman, Dar es Salaam, uk. xxiii.
6. AbdilatifAbdalla, uk. xxiii.
7. Angalia D.T. Niane (1960) Soundjata, ou l'epopee mandingue. Presence Africaine, Paris, uk. 9 (Tafsiri ni yangu).
8. Niane, uk. 9.
9. Chinua Achebe, (1576) "The Novelist as Teacher" katika Morning Yet on Creation Day. Anchor Books, New York, kur. 55-60.
10. Senkoro, uk. 5.
11. Anthony Cronin (1976) "A Massacre of Authors." Encounter (April 1956), uk. 25.
12. Angalia D.H. Lawrence (1965) (Mh) Selected Non - Dramatic Writings of Bernard Shaw. Houghton, Boston, uk. 309
13. Chinua Achebe (1976) "Colonialist Criticism," m.y.k., kur. 3-24.
14. Wole Soyinka (1984) "The Critic and Society: Barthes, Leftocracy and other Mythologies," katika Black Literature and Literary Theory, kimehaririwa na Henry Louis Gate, Jr. Methuen, New York, kur. 27-57.
15. T.S.Y. Sengo (1973) "Uwanjawa Uhakiki", Kioo cha Lugha, 3, uk. 11.
16. Karl Marx na Frederick Engels (1988) Manifesto of the Communist Party. William Reeves Booksellers Ltd., London, uk. 9.
17. Angalia, kwa mfano, Georg Lukacs, (1978) "The Writer and the Critic," katika Writerand Critic, kimefasiriwa na Professor Barthur Kahn, Merlin Press, London, uk. 198-226.
18. Angalia Theodor Adomo, (1982) "Cultural Criticism and Society", katika Prisms, kimefasiriwa na Samuel na Shierry Weber, The MIT Press, Cambridge, Massachusetts, kur. 17-34.
19. Adomo, k.h.j., uk. 20.
to previous section
Powered by Blogger.