Kwa kutoa mifano kutoka katika jamii yako, jadili dhima mbalimbali za fasihi simulizi huku ukirejelea vipera mbalimbali vya utanzu huu wa fasihi.

 
 
Kwa kutoa mifano kutoka katika jamii yako, jadili dhima mbalimbali za fasihi simulizi huku ukirejelea vipera mbalimbali vya utanzu huu wa fasihi.

Kwa kutoa mifano kutoka katika jamii yako, jadili dhima mbalimbali za fasihi simulizi huku ukirejelea vipera mbalimbali vya utanzu huu wa fasihi.

Fasihi simulizi ni utanzu mmoja wapo kati ya tanzu za fasihi ambao una dhima mbalimbali kwa kwa jamii husika. Hata hivyo kabla ya kuangalia dhima za fasihi simulizi ni vyema kwanza kutalii fasili ya fasihi simulizi.
Mulokozi, M.M (1996) anasema, Fasihi Simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi.
TUKI (2004) wanasema Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili. 
Hivyo basi Fasihi Simulizi ni fasihi inayotokana na maneno ambayo huzungumzwa, hutolewa au kuimbwa ambapo mtungaji na mwasilishaji hutumia sanaa. Baada ya kuangalia maana ya fasihi simulizi sasa tuangazie dhima mbalimbali za fasihi simulizi kwa jamii.
KIINI

Kuburudisha; tanzu mbalimbali za fasihi simulizi hutumika kama nyenzo ya burudani katika nyanja mbalimbali za kijamii. Mfano wa tanzu hizo ni kama vile hadithi, ushairi (nyimbo mbalimbali),  semi (methali, vitendawili).  Tanzu hizi hutoa burudani katika sehemu mbalimbali, mfano nyimbo, zipo nyimbo ambazo hutumika kutoa burudani katika sehemu mbalimbali kama vile harusini-nyimbo za harusi, nyimbo za nyiso hutoa burudani jandoni na unyagoni. Vilevile katika siasa zipo nyimbo ambazo hutumika kutolea burudani na uhamasishaji wakati wa kampeni za kisiasa kwa mfano wimbo wa tumejipanga,mwaka huu wataisoma (ccm). Hivyo basi kutokana na utanzu huu wa nyimbo kutumika kama chombo cha burudani katika nyanja mbalimbali huonesha dhahiri kuwa ni kwa namna gani fasihi simulizi inatimiza wajibu wake kwa jamii.

Kuelimisha; kupitia fasihi simulizi jamii hujipatia elimu ambayo huwasaidia kuijua vizuri historia yao, utamaduni, siasa ya nchi yao pamoja na itikadi. Mfano katika historia zipo kazi za fasihi simulizi ambazo huonesha historia, kazi kama utendi wa Fumo Lyongo kuhusu historia ya jamii ya Wangozi, utendi wa Shaka Zulu ambao hutupatia historia na utamaduni wa watu wa Afrika kusini. Pia ndani ya tendi hizo kuna masuala ya uongozi pamoja na siasa. Vilevile zipo methali ambazo huelimisha watu kufanya kazi kwa bidii ili kujiongezea nafasi yao kiuchumi, kwa mfano; “mgaagaa na upwa hali wali mkavu”. Kadhalika katika upande wa afya zipo methali zinazotoa elimu mfano “kinga ni bora kuliko tiba”. Hivyo basi utoaji huo wa elimu katika nyanja tofauti tofauti huonesha ni kwa namna gani fasihi simulizi ilivyo na dhima kubwa kwa jamii.

Kuhifadhi historia na utamaduni wa jamii; katika suala hili pia fasihi simulizi haikuwa nyuma kwani zipo kazi mbalimbali ambazo hutumika kama nyenzo kuu na muhimu za kuhifadhia amali za jamii kwa mfano visasili na visakale hutunza historia na utamaduni wa jamii husika, mfano; kisasili cha kibo na mawenzi hutunza historia ya Tanzania kuhusu mlima Kilimanjaro. Pia zipo methali ambazo hutunza utamaduni wa waafrika hususani Tanzania mfano; “Asiyesikia la mkuu huvunjika guu”, methali hii hutunza utamaduni wa kiafrika kuwa wadogo lazima wawasikilize na kuwaheshimu wakubwa. Kadhalika katika siasa kupitia kipera cha lakabu ya baba wa taifa huonesha historia ya kiongozi wa Taifa la Tanzania.

Kuhamasisha umoja na mshikamano; suala hili pia hufanywa na aina hii ya fasihi simulizi katika jamii na hujidhihirisha katika Nyanja mbalimbali kama vile siasa, zipo methali ambazo uhamasisha suala hili:- “Umoja ni nguvu utengano ni udhaifu”, “Kidole kimoja hakivunji chawa”. Kwa upande wa nyimbo zipo pia ambazo huhamasisha suala hili kama vile nyimbo za chapuzo mfano; wawe-kilimo, kimai-uvuvi. Vileveli zipo nyimbo ambazo huhamasisha umoja na mshikamano wakati wa michezo.

Kukuza lugha; fasihi simulizi hujikita pia katika suala hili la ukuzaji lugha kupitia vipera mbalimbali ambavyo hufanyika katika nyanja mbalimbali kwa mfano nyanja ya elimu, vipo vipindi mbalimbali redioni na hata kwenye luninga ambavyo hutumika kufundishia lugha hasa kwa watoto kwa kupitia vipera vya fasihi simulizi kama vile vitendawili na methali, zipo pia chemshabongo na hadithi mbalimbali. Vilevile ipo michezo ya watoto ambayo hukuza lugha kama vile kauli tauria, mfano; “Katibu kata wa kata ya mkata alikataa katakata kukata miti katika kata ya mkata”. katika siasa uibukaji wa misimu mfano, chakachua, ngangari nk. pamoja na nyimbo hasa wakati wa kampeni husaidia kukuza lugha. Pia shughuli mbalimbali za kijamii mfano harusi, misiba kupitia nyimbo za watani pia hutoa mchango mkubwa katika kukuza lugha.

Kuonya na kukosoa jamii; zipo tanzu na vipera mbalimbali vya fasihi simulizi ambavyo hujihusisha zaidi na kuiweka jamii katika nafasi iliyobora zaidi. Mfano; kimaadili kuna methali zinazoonesha maadili mema katika jamii mfano; “Samaki mkunje angali mbichi”, “Mkaidi hafaidi mpaka siku ya iddi”. Vilevile kiuchumi zipo methali ambazo huonya na kukosoa wale wote wenye tabia za kivivu katika kujitafutia maisha mfano, “Mtegemea cha ndugu hufa masikini”, “Fanyakazi kama mtumwa uishi kama mfalme”.

Vilevile kuongeza kipato; kupitia fasihi simulizi watu hujiajiri na kujipatia kipato. Kwa mfano; watu hujishughulisha na utanzi wa nyimbo mbalimbali kama vile nyimbo za kisiasa, kiuchumi pamoja na nyimbo za kiutamaduni ambapo kwa namna moja au nyingine huwasaidia katika suala zima la kujipatia kipato na kusukuma mbele gurudumu la maisha kwa ujumla.

HITIMISHO

Hivyo basi, kutokana na fasihi simulizi kujihusisha na masuala mtambuko katika jamii ya leo ni dhahiri kuwa maendeleo ya sanaa jadi yanapiga hatua na kamwe hayawezi kupotea kabisa, ila tu, upo uwezekano wa kubadilika kulingana na maendeleo ya jamii husika.
Powered by Blogger.