TAHAKIKI-KIMBUNGA

 

JINA LA DIWANI: KIMBUNGA

MWANDISHI: HAJI GORA HAJI

WACHAPISHAJI: TUKI

MWAKA: 1995

UTANGULIZI


Kimbunga ni diwani inayozungumza juu ya mawaidha mbali mbali katika maisha pamoja na suala zima la ujenzi wa jamii mpya.Katika diwani hii,mwandishi ametoa maadili na maonyo mbali mbali pamoja na mbinu mbalimbali za kufuata ili kufanikiwa katika suala zima la ujenzi wa jamii mpya hapa nchini.

MAUDHUI;

DHAMIRA KUU-Ujenzi wa jamii mpya

Mwandishi amejadili dhamira ya ujenzi wa jamii mpya katika kazi yake.Mwandishi ameonesha vikwazo mbali mbali vinavyokwamisha ujenzi wa jamii mpya hapa nchini, Vikwazo hivyo ni kama vile uongozi mbaya,rushwa,tamaa, ukosefu wa elimu, ukoloni mamboleo, n.k.

Katika kujadili dhamira hii mwandishi ameonesha mbinu/njia mbalimbali ambazo jamii inapaswa kuzitumia  katika suala  zima la ujenzi wa jamii mpya hapa nchini,hizo ndizo dhamira ndogo ndogo;

 

1.     Uongozi Mbaya

Mwandishi ameonesha kuwa Uongozi bora unahitajika kwa jamii yoyote ile ili kuleta ufanisi mzuri katika utendaji na utekelezaji wa majukumu mbalimbali kwani Uongozi mbaya unasababisha kushindwa kufikia malengo.Kutokana na uongozi mbaya ndiyo maana jamii hufikia kufanya mpinduzi ili kuuondoa uongozi uliopo na kusimika uongozi mpya ili kuijenga jamii kwa upya.

Katika shairi la “Kimbunga” (uk 1) mwandishi anaongelea juu ya mapinduzi yanayofanywa na tabaka la chini dhidi ya tabaka tawala.mwandishi anasema;

’kimbunga mji wa siyu,kilichowahi kufika,

Si kwa yule wal huyu,ilikuwa patashika,

Kimeing’owa mibuyu,minazi kunusurika,

Nyoyo zilifadhaika’’.

Mwandishi ametumia mji wa Siyu kama kielelezo kizuri kwa jamii yeyote inayotaka kufanya mapinduzi ili kuondoa viongozi wabaya/wabovu na kuleta viongozi bora.Katika mapinduzi hayo mwandishi amefafanua kuwa wananchi wengi ndio wanaoathirika na wachache hunusurika.

Shairi la Madanganyo” mwandishi anazungumzia jinsi uongozi mbaya unavyowadanganya wananchi na jinsi unavyowaathiri na kuwakera wananchi.Wananchi hushiriki katika shughuli za uzalishaji mali (miradi mblimbali) lakini matunda ya jasho lao huliwa na wachache.Wachache hao husahau wale waliosulubika katika uzalishajina na mtokeo yake wananchi wanaishia kuishi maisha ya taabu.Katika Ubeti wa 6,msanii/mwandishi anasema;

Mlitupigia mbiu, tulimeni ushirika,

Tukakatana miguu, kwa mapanga na mashoka,

Manufaa kwa wakuu, wadogo yetu mashaka,

Wezeni kutukumbuka, mjue nasi wenzenu.”

Shairi la Wenye Vyao Watubana mwandishi amejadili namna matajiri jinsi wanavyowagandamiza,kuwanyonya na kuwabana wale wasio na chochote yaani maskini.Mwandishi anawaomba viongozi wawatetee ili kuepukana na hali hii.Hii ni kutokana na uongozi mbaya ndiyo maana hali kama hii ipo nchini lakini viongozi hawachukui tahadhari yeyote ile.Katika ubeti wa 7,mwandishi anasema;

“Maji yamezidi unga,kwa lodi wa darajani,

Kujitolea mhanga,kwa bei hawezekani,

Mvao wake wa kanga,ni shilingi elifeni,

Wakubwa tuteteeni, wenye vyao watubana.”

Shairi la “Kibwangai”  linajadili dhana ya usaliti wa viongozi wetu kwa wananchi wanaowaongoza. Mwandishi ameonesha jinsi wananchi wanavyowachagua viongozi wao lakini viongozi hao wakishapata madaraka au wakishashika nyazfa wanageuka na  kuwasaliti wananchi waliowachagua.Katika ubeti wa 7,msanii anasema;

Kibwangai lipoona, ni mtu kakamilika,

Akaanza kujivuna,na dharau kuzidiya,

Wala hakujali tena,wenzake walowambiya,

Akahisi hawi nyani,umbo lile litadumu.”

Katika Shairi hili manii ametumia taswira ya Kibwangai kuwakilisha viongozi wasaliti na nyani kuwakilisha wananchi wanaoongozwa na akina Kibwangai yaani watawaliwa.

Katika shairi la “Hili Mnatutakiya,mwandishi anaonesha jinsi vyombo vya dola kama vile polisi ,jeshi n.k  namna  vinavyoshindwa kutekeleza wajibu wake wa kuwalinda raia na kuwashughulikia wahalifu.Katika ubeti wa  1,msanii anasema;

Twasema kinaganaga,tumechoka vumiliya,

Wenzetu mkatubwaga,hasa ukiangaliya,

Hao wezi mwafuga,wazidi kutuibiya,

Hakuna watendewalo,ndipo wakapamba moto.

Msanii ameonesha kuwa vyombo hivyo ndivyo  vinavyowalinda wezi,majambazi na matapeli.

Kwa ujumla  msanii wa  diwani hii anaona kuwa ili tujenge jamii mpya lazima tuwe na uongozi bora unaowajali wananchi wake.

2.     Kupiga vita rushwa

Rushwa ni kikwazo kimojawapo kinachokwamisha kujenga jamii kwa upya.Kutokana na rushwa kuota mizizi  katika jamii haki hupotea bali wachache wanafaidi matunda ya nchi  na wengine wanaendelea kuumia.Katika Shairi la “Rushwa mwandishi anasema;

Rushwa kajenga kambi,na kuondoka hataki,

Afanya kila vitimbi,mkaidi hashindiki,

Tumzushiyeni wimbi, isiwe kutuhiliki,

Tumchimbie handaki,rushwa tukamzikeni.”

Katika ubeti huu,mwandishi anatuonesha kuwa lazima jamii yetu ipinge rushwa ili haki na usawa vitawale kwani kupiga vita rushwa ni njia pekee itakayosaidia  kujenga jamii mpya ambayo mwandishi ameipendekeza.

3.     Umuhimu wa Elimu

Ili tuijenge jamii mpya ni lazima watu wapate elimu na waelimike bila kujali umri wala jinsia.Mwandishi anawahimiza wazee kujiunga na kisomo chenye manufaa ili wafute ujinga wa kutojua kusoma na kuandika.Katika shairi la “Kisomo cha Maarifa  ubeti wa 2,Msanii anasema;

Kisomo cha manufaa,tusomeni kwa haraka,

Isiwe tunakataa,kwa kuwa tumekongeka,

Roho si inochakaa,mwili ndio hupayuka,

Tusomeni kwa haraka,kisomo cha maarifa.

katika shairi hili mwandishi anawahimiza wazee wajiunge na kisomo cha elimu ya watu wazima kwa sababu wakishaelimika watakuwa na uwezo wa kupanga mipango yao ya maendeleo.

Mwandishi anaonesha kuwa elimu ni silaha madhubuti katika kufanikisha zoezi zima la ujenzi wa jamii mpya kwani  bila kuwa  na wasomi katika jamii kama hii yetu zoezi la ujenzi wa jamii mpya halitaweza kufanikiwa.

4.     Ukoloni mamboleo

Ukoloni mamboleo ni kitendo cha nchi kuwa na uhuru wa bendera lakini kimaamuzi inatawaliwa na nchi nyingine.Ukoloni mamboleo ni kikwazo kikubwa kinachokwamisha maendeleo ya uchumi hapa nchini.Na ili tuweze kufanikisha ujenzi wa jamii mpya hapa nchini hatuna budi kupiga vita ukoloni mamboleo.Katika shairi la “Chuwi Mwandishi anaonesha jinsi ukoloni mamboleo unavyoathiri maendeleo ya uchumi hapa nchini.Ukoloni mamboleo unawaathiri watu wa tabaka la chini wasio nachochote na kuwanufaisha matajiri au tabaka la juu. Katika ubeti wa 6 mwandishi anasema:-

Ambao ni matajiri, kwao anapowafikiya,

Huweza kujisitiri, salama kujipatiya,

Walokuwa mafakiri, huzidi kuwaoneya

Huyu ndiye Chuwi gani?

Mwandishi ameeleza kuwa ukoloni mamboleo huingia kwa njia mbali mbali katika nchi zinazoendelea.Hivyo mwandishi anatahadharisha kuwa tuepukane na mbinu (njia) hizo na tuupinge ukoloni mambo leo kwa nguvu zote ndipo tutaweza kujenga jamii mpya.

5.     Umuhimu wa kujitawala

Ili tuweze kujenga jamii mpya ni lazima tujitawale katika Nyanja zote za kifikra,kisiasa,kiutamaduni pamoja na kiuchumi. Katika shairi la “Afrika “Mwandishi anaeleza kuwa ili tuweze  kujitawala ni lazima tuepukane na unafiki,vibaraka (wasaliti),tusikate tama na tudumishe amani. Katika ubeti wa 3 msanii ansema:-

Wasaliti wazikishe, wasiwe wenye kuzuzuka,

Tamaa uwakatishe, yasiwe wanayotaka,

Katu wasiwawezeshe, wabakiye kuzuzuka,

Washindike mahusuda,wasopenda bara letu.”

Katika shairi la “Kujitawala Mwandishi anaeleza umuhimu wa kujitawala kwa jamii yoyote ile.Mwandishi anaonesha kuwa, kujitawala ni pale umma unapokuwa na mamlaka ya kuamua mambo yao wenyewe bila kuingiliwa au kuwekewa vikwazo vyovyote.Katika Ubeti wa 1 Msanii anasema:-

Kujitawala si kwema,kuliko kutawaliwa,

Kujitawala ni umma,kila yao kuamua,

Kujitawala si kama,ulanguzi na rushwa

Katika shairi hili la ‘kujitawala’ mwandishi anaonesha faida mbalimbali za kujitawala kama vile kuwepo kwa demokrasia, kuwepo umoja naushirikiano,kuwepo haki na usawa,amani hudumishwa,vile vile mila na desturiza nchi zinadumishwa.Hivyo mwandishi anatuasa kuwa ili tujenge jamii mpya ni lazima tujitawale kisiasa,kiuchumi,kiutamaduni na kifikra.

6.     Umuhimu wa kazi na kuwajibika

Kazi ni nguzo muhimu sana ya ujenzi wa jamii mpya.Mwandishi amesisitiza umuhimu wa kazi na kuwajibika.katika shairi la Kazi” Mwandishi anatuonesha kuwa kazi ndio msingi wa maendeleo. Anasisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii na tuepukane na njaa. Ubeti wa 1,mwandishi anasema;-

“Pesa huletwa na kazi, ni njia zipitiayo,

Hutopata matumizi,iwapo kazi hunayo,

Hata njaa hukuhizi,uvivu na angamiyo’’

Katika shairi la “Uokolewe”,mwandishi anasisitiza umuhimu wa kudumisha umoja na mshikamano ili kuinua uchumi wetu. Anasisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa  bidii na kutumia vyema  rasilimali zetu ili kuinua uchumi wetu.

Katika shairi la Dumizi  mwandishi anakemea  tabia ya baadhi ya watu kukaa bila kazi (uvivu) na kuanza  maisha ya kunyonya.Hivyo mwandishi anapiga vita unyonyaji unaofanywa na baadhi ya watu.

Hivyo msanii aniasa jamii kujihusisha na ukulima, uvuvi, utalii na viwanda ili kujenga jamii kwa upya.

7.     Mapenzi na ndoa

Katika diwani hii,mwandishi ameonesha kuwa mapenzi yamegawanyika katika pande kuu mbili ambazo ni;Kuna mapenzi ya kweli na mapenzi ya udanganyifu.

Katika shairi la “Usimpige Mkeo mwandishi anasema kuwa haifai mwanaume kumpiga mke wake na vile vile  mwanaume hatakiwi kumwekea mkewe masharti magumu.

Shairi la “Hongera” mwandishi anawaonya wanandoa (bibi na bwana) wasiwe na tabia ya kufukuzana wawapo nyumbani. Amewapa kila mmoja maadili yake kwa mwenzake. Beti za  (4-5) mwandishi anasema:-

4- “Bi arusi yangu shika, uyatie akilini.

Muumeo akifika, anapotoka kazini,

Mpe mema mamlaka, aliwazike moyo,

Hongera!

5- “Bwana arusi sikia, ukiwa kwako nyumbani,

Maneno ya kutupia,hayafai asilani,

Kauli njema tumia, na lugha iwe laini,

Hongera”

Katika shairi la “Sifa ya Mke” msanii  anaonesha kuwa sifa kubwa ya mwanamke ni tabia na wala  si sura.Sifa ya tabia njema humpa mwanamke taadhima,huruma,utiifu na hata uhodari. Anaeleza kuwa  mwanamke anapaswa kuwa  mtulivu,asiwe kiruka njia, asiwe na ufedhuli wa aina yoyote,uovu, n.k.

Katika shairi la Sitakimwandishi anakemea mapenzi ya udanganyifu yaliyoshamiri katika jamii zetu kwa wakati huu. Mwandishi anasema:-

Rabi sinipe mapenzi,hakuna wa kuamini,

Wapendwa wenye ujuzi,ni wachache duniani,

Penzi la siku hizi,kuhadaana nyoyoni,

Mapenzi yamepotea, sasa ni adimu sana,”

Ni kweli mapenzi ya siku hizi hutawaliwa na pesa na yamejaa ulaghai wa kila aina pamoja na udanganyifu.Mwandishi anaitaka jamii kutambua kuwa mapenzi ya pesa si mapenzi ya kweli hivyo ni vyema yapigwe vita.

 

8.     Maonyo na maadili mema katika maisha

Mwandishi amekuwa mwalimu mzuri wa walimwengu kuhusiana na harakati mbali mbali za maisha.Mawaidha aliyoyatoa mwandishi ni kielelezo kizuri kinachofaa kufuatwa na kizazi hiki.Maadili na maonyo haya ni ya muhimu sana katika maisha.Maadili hayo ni kama vile:-

(a)Malezi bora katika jamii ni njia pekee ya kuiweka jamii katika msingi bora wa maisha.Katika shairi la“Vijana wa Zanzibar” Mwandishi ameonesha matendo ambayo vijana wa siku hizi  wanayatenda ambayo si mazuri pia  ni ya kusikitisha.vijana wa siku hizi hawana utii,ni wajeuri, ni wadanganyifu,ni majambazi na pia hudharau mila na desturi zetu za asili na kukimbilia tamaduni za kigeni.Katika  ubeti wa 2 msanii anasema:-

Mwawacha yenu ya hapa,ambayo yako mazuri,

Kutii na kuogopa,mwaona hakuna kheri,

Mwayavamia kwa pupa,kwa kedi na ujeuri,

Mila zetu za fakhari,wacheni kuzipotosha.”

Kulingana na ubeti huu mwandishi anaonesha kuwa suala la malezi bora ni muhimu sana katika jamii ili kuwaandaa vijana wetu kuendana na mazingira wanamoishi.

Kwa ujumla, katika suala la malezi mwandishi anaifundisha jamii kuwa,samaki mkunje angali mbichi.

b)Umuhimu wa kuwathamini wazazi

Mwandishi ameonesha kuwa kuna umuhimu wa kuwaheshimu na kuwathamini wazazi.Katika shairi la “Wazazi  msanii ameonesha kuwa wazazi ndiyo ngao ya mtoto; hivyo mtoto hatakiwi kuwakasirikia,kuwaudhi wala kuwachikiza bali anatakiwa kuwa na mapenzi nao.Wajibu wa wazazi kwa mtoto ni  kumpa chakula, mavazi,malezi mema pamoja na elimu.Katika ubeti wa 4 msanii anasema;

Wakatafuta walimu,kukupatia ujuzi,

Wakakufunza elimu,pamoja na matumizi,

Sasa ni mtu timamu,waendelea na kazi,

Usiwaudhi wazazi,hiyo ndiyo yako ngao

Katika shairi la “Ulezi KaziMwandishi ameonesha jinsi mama (wazazi) wanavyohangaika kubeba mimba hatimye kuzaa na kuanza kazi ya ulezi wa mtoto hadi anapofikia umri wa kujitegemea. Mwandishi anaonesha kuwa wazazi hupata taabu na shida mbalimbali katika ulezi wao.Hivyo mwandishi anashauri wazazi wathaminiwe na wapewe heshima zote wanazostahili.

c)Kuepukana na umbea

Umbea ni ile tabia ya kutoa maneno au habari bila kutumwa. Mwandishi anaona tabia hii si nzuri,kwani huweza kutenganisha marafiki au ndugu kwa njia ya uchonganishi.

Katika shairi la “Wacha Hayo” mwandishi anaishauri jamii iepukane na umbea na badala yake ijishughulishe na shughuli za uzalishaji mali.Madhara ya umbea ni kama vile majungu,uchochezi,n.k. Umbea pia husababisha utengano baina ya ndugu au marafiki.Ubeti wa 1 mwandishi anasema;

Wacha kupika majungu,na kuleta uchochezi,

Kuwajaza walimwengu,kasumba zile na hizi,

Hicho kimoja kifungu,huletesha ubaguzi,

Tuacheni ubaguzi,huvunja mafanikiyo.”

Katika shairi la “Hayafai Mitaani  mwandishi anaionya jamii kuwa si jambo la busara au zuri kusambaza au kupeleka taarifa ya jambo fulani sehemu ambayo haihusiki.Anaona kuwa ni busara sana endapo jambo fulani limefanyikia sehemu fulani liishie huko huko lilikotokea na haifai kulipeleka sehemu isiyohusika.Si tabia nzuri kupeleka mitaani kwa watu wasiohusika. Katika ubeti wa 2 unasema:-

Yanayosemwa kunini, huko huwa yamekisha,

Haifai asilani, mitaani kufikisha,

Kwani siri ya mwituni, si vyema kuelewesha,

Ya kunini huishia kunini.”

Hivyo mwandishi anatushauri kuwa jambo moja likitendeka sehemu moja ni bora liishie katika sehemu hiyo na hakuna haja ya kulipeleka sehemu nyingine.

(d)Kuepukana na udokozi (tabia ya wizi)

Udokozi ni ile hali ya kunyemelea vitu visivyo vyako kwa lengo la kuiba au kunyang’anya.Katka shairi la ‘Paka’mwandishi anakemea tabia hii kwani  si nzuri.Tabia hii ipo miongoni mwa wanajamii.Mwandishi anaonya kuwa tabia hii huhatarisha maisha ya wahusika yaani wenye tabia hii.Mwandishi amemtumia paka kuwakilisha watu wenye tabia hiyo.Aidha mwandishi anaendelea kuelezea  kuwa tabia hii husababisha uchokozi,ugomvi  pamoja na chuki katika maisha.

(e)Umuhimu wa shukrani katika maisha

Mwandishi anaieleza jamii umuhimu wa kutoa shukrani pale mtu anapofanyiwa hisani na mtu mwingine. Katika shiri la “Punda”  mwandishi ameonesha jinsi baadhi ya watu wasivyo na shukrani kwa wenzao ple wanapotendewa mema.Mwandishi ameonesha kuwa mwandamu asiye na shukrani hata umfanyie wema kiasi gani hawezi kutoa shukrani.Ameelezea kuwa mtu asiye na shukrani ni vyema kuachana naye au kumtenga (kutengana naye) kabisa. Anasema;

Punda hakumbuki wema,hata kwa mchunga wake,

Humpa mwingi mtama, na maji  anufaike,

Katu haiwi salama, shukrani zake mateke,

Ndiyo tabia ya punda,kurusha rusha mateke,

Kuchunga akikushinda, muwachiye ende zake.

Katika ubeti huu,mwandishi anasisitiza umuhimu wa kutoa shukrani pale tunapofanyiwa fadhila au jambo jema.

UJUMBE

Ø Dhana potofu ya kudhani bila ya kuwa na uhakika wa mambo haifai katika jamii kwa sababu hupotosha ukweli wa mambo.

Ø Mapenzi na ndoa ya dhati ni muhimu katika jamii zetu

Ø Ukoloni mamboleo, uongozi mbaya,rushwa na ukosefu wa elimu ni baadhi ya vikwazo vya ujenzi wa jamii mpya hapa nchini.

Ø Maadili mema na maonyo ni njia pekee ya kuiweka jamii katika misingi ya haki na usawa.

FALSAFA

Mwandishi anaamini kuwa maadili mema na maonyo ni njia pekee ya kuiweka jamii katika msimamo na  mwenendo bora wa maisha na anatetea misingi ya haki na utu katika jamii.

MSIMAMO

Msimamo wa mwandishi una hali ya udhanifu kwani amejadili baadhi ya mambo kwa kudhani tu bila kuwa na misingi ya kisayansi.

 

FANI

1. MITINDO

Mwandishi wa diwani ya KIMBUNGA ametumia mitindo ifuatayo:-

(a)  Mtindo wa kuhoji

 Ni mtindo Swa kuuliza maswali ambayo ama majibu yake yako wazi au hayako wazi.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kuhoji au kuuliza maswali katika diwani hii ni “Mnapata Kitu Gani?”  na “Nimuite Jina Gani” .

Katika shairi la “Mnapata Kitu Gani?” ,mshairi anasema;

“Wavutaji wa sigara, nauliza nijibuni,  

Ni ipi yake tijara, mwapata faida gani,  

Nipeni jawabu bora, ambayo ya kuamini, 

Ni ipi tijara yake, nambiyeni mvutao”

 

Katika shairi la “Nimuite Jina Gani” ,mshairi anasema:

Ninalo suali langu, wamalenga msikiye, 

Ilivyo na ndugu yangu, na mimi ndiye kakaye,  

Amemuowa mwanangu, aliye nihusu miye, 

Mke nimuite vipi, mwanangu au shemegi”

 

(b)  Mtindo wa msisitizo au takriri

Ni mtindo ambao neno moja linatokea mwanzoni na linarudiwa katika mishororo au mistari ya ubeti wa shairi.Shairi lililotumia mtindo wa msisitizo au takriri katika diwani hii ni “Kujitawala”.Mshairi anasema;

Kujitawala si kwema, kuliko kutawaliwa, 

Kujitawala ni umma, kila yao kuamuwa,  

Kujitawala si kama, ulanguzi na rushwa.  

 

 

Kujitawala ni mila, nchini kushikiliwa, 

Kujitawala aila, kufunzwa yanotakiwa,

Kujitawala si ila, kufanza yaso kuwa”.

( c )  Mtindo wa masimulizi

Ni mtindo ambao mshairi ama huamua kusimulia hadithi yeye mwenyewe au huwaumba wahusika wanaosimulia hadithi  au kisa fulani kwa wengine.Shairi lililotumia mtindo wa masimulizi katika diwani hii ni  “Kibwangai”. Mshairi anasema;

Kuna hadithi ya kale, kwa babu nimepokeya, 

Kwa manyani zama zile, mkasa ulotokeya,

Nilikuwa mwanakele, hayo nikazingatiya,  

Leo nawadokezeya kwa nilivyofahamu”

 

( d )  Mtindo wa kuto wasia

Ni mtindo ambao unonesha usia au maagizo ya mtu kwa watu wake ambayo anataka yatimizwe baada ya kifo chake au kuondoka kwake mahali fulani.Mashairi yaliyotumia mtindo wa kutoa wosia katika diwani hii ni”Wasia” na “Paka”.

 

Katika shairi la “Wasia”,mshairi anasema;

“Wasia wangu nakupa, mwanakwetu zingatiya,  

 Siingiliye kwa pupa, ina hatari duniya,  

 Itakuja kukutupa, usipopakusudiya,  

 Kaa kwa kuiogopa, katu haina shujaa”

 

Katika shairi la “Paka”, mshairi anasema;

“Kuna hadithi ya kale, kwa babu nimepokeya, 

Kwa manyani zama zile, mkasa ulitokeya,  

Nilikuwa mwanakele, hayo nikazingatiya, 

Leo nawadokezeya, kwa nilivyoyafahamu”

 

( e ) Mtindo wa majibizano

 Ni mtindo ambao mshairi anaamua kuwaumba wahusika wanaozungumza kwa kupokezana maongezi.Shairi lililotumia mtindo wa masimulizi katika diwani hii “kibwangai” . Mshairi anasema;

          “Pana mmoja kasema, kibwangai kumwambiya,

              Kama tutalokutumia, weza kututimiziya,

              Isiwe kurudi nyuma, ewe mwenzetu sikia,

              Wewe tumekuchagua, utumikie kaumu.

 

             “Kibwangai akasema, hayo nimezingatia,

              Kidete nitasimamia, jitihada kutimia,

              Kwa kusi na kulima, mpate jifaidia,

              Sitobadili mawazo, ilipwe yangu kaumu”

( F ) Mtindo wa kutoa amri

Ni mtindo ambao mshairi huonekana ama akiamrisha watu kufanya au kutofanya jambo Fulani au akitoa maelekezo fulani muhimu kwa wanajamii.Shairi lililotumia mtindo wa kutoa amri katika diwani hii ni “Usimpige mkeo” (uk. 12). Mshairi anasema:

“Mke hapigwi kwa fimbo,wala hapigwi mateke,

Hupigwa kwa mapambo, hilo ndilo pigo lake,

                      Usiyaharibu mambo, utajuta mwisho wake,

                       Kupiga piga si kwema, kaa nae kwa salama”

( g )Mtindo wa kidato

Ni mtindo ambao mshairi hutumia baadhi ya mistari iliyofupishwa maneno au silabi tofauti na mistari mingine ambayo huwa na silabi au maneno mengi. Mashairi yaliyotumia mtindo wa kidato katika diwani hii ni “Usimalize”,“Hongera”, “kimbunga”, “kazi”, “Dumuzi”,“chuwi”, na “Madereva”.

Katika shairi la “Usimalize”, mshairi anasema:

“Haifai kumaliza, kumi utumie tisa,

        Moja utudunduliza, kuna halafu na sasa,

Weza kujihakibiza, usijipige msasa,

                                      Akiba haichakai,

 

Katika shairi la “Hongera” ,mshairi anasema;

“Biarusi yangu shika,uyatie akilini,

Muumeo akifika,anapotoka kazini,

        Mpe mema mamlaka, aliwazike moyoni,

                                            Hongera”.

 

 

(h) Mtindo wa nafsi

Ni mtindo ambao mshairi anaweza kutumia nafsi umoja,nafsi wingi au nafsi kikundi kwa lengo la kufikisha ujumbe au maudhui fulani kwa jami.Kuna nafsi za aina tatu (3),yaani nafsi ya kwanza (umoja na uwingi),nafsi ya pili (umoja na uwingi, na nafsi ya tatu,(umoja na uwingi).Mwandishi wa diwani hii ametumia mtindo wa nafsi kama ifuatavyo:

 

       i.            Matumizi ya nafsi umoja (nafsi ya kwanza umoja na nafsi ya pili umoja):

Katika mtindo huu mshairi huzungumzia jambo ambalo linamuhusu mtu mmoja pekee.Hujumuisha ahadi,matamanio, sifa mawaiza na maonyo.Mashairi yaliyotumia nafsi ya kwanza umoja katika diwani hii ni “uchawi”, “kipaji” na “sitaki”. Kwa mfano katika shairi la “sitaki”, mshairi anasema:

“Wanaopenda nawapende, mimi siye asilani,

Nimejitenga upand, singie mwao kundini,

Moyo nimepiga konde, usiweze kutamani,

Mapenzi yamepotea, sasa ni adimu sana”.

 

Pia mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya pili umoja katika diwani hii ni “usimpige mkeo” , “kurumbizi” , “usimalize,“Paka”, “Dawa ya deni kulipa”, “ Sifa ya mke”  na “Wasia”.Kwa mfano katika shairi la “kurumbizi”, mshairi anasema;

“Siye wewe kurumbizi, wa kubughudhi kuichaka,

             Si mema mapendekezi, ukae ukikumbyuka,

             Kuponda haipendezi, ambacho kinakuweka,

              Usiwe mpopotozi, na hayo ukatamka,

             Mbona unaghafilika, nakuhasa kulumbizi”

     ii.            Matumizi ya nafsi wingi (nafsi ya kwanza wingi);

Katika mtindo huu mshairi huzungumzia jambo au suala linalohusu kundi fulani la watu,akiwemo na yeye mwenyewe. Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya kwanza wingi katika diwani hii ni “kisomo cah manufaa” , “Rushwa” , “Wenye vyao watubana” , “Usafi” , “Wacha hayo” ,“dhamana” .Kwa mfano katika shairi la “Rushwa” ,mshairi anasema:

         “Rushwa kajenga kambi, na kuondoka hataki,

               Afanya kila vitimbi, mkaidi hashindiki,

               Tumzushiyeni wimbi, isiwe kutuhiriki,

               Tumchimbie handaki, rushwa tukamzuikeni.”

 

  iii.            Matumizi ya nafsi kikundi (nafsi ya tatu wingi);

Katika mtindo huu mshairi huonekana ama akisimulia hadidhi, akitoa hotuba au akizungumzia kundi fulani la watu kuhusu suala au jambo muhimu.Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya tatu uwingi katika diwani hii ni “Hili mnatutakia”, “wazazi

“Dumuzi” . Kwa mfano katika shairi la “ Hili mnatutakia”,mshairi anasema;

Wakijua unapesa, nyumbani watakujia,

         Usiku wa saa tisa, ndani kukuingilia,

 Mara wakakukabasa, na vyako kuangamiya,

Hakuna watendewalo, ndipo wakapamba moto.”

 

 ( B ) MUUNDO

Mwandishi wa diwani ya hii ametumia miundo tofauti tofauti kwa kuzingatia vigezo mbalimbali kama ifuatavyo:-

Ø Kigezo cha idadi na mishororo:

Kwa kuzingatia kigezo cha idadi na mishororo kwa kira ubeti mshairi ametumia miundo ifuatayo;

(a) Muundo wa tathlitha

Ni muundo ambao kila ubeti unakuwa na mistari mitatu.Shairi lililotumia muundo wa tathlitha katika diwani hii ni “kujitawala”. Mshairi anasema;

“kujitawala si kwema, kuliko kutawaliwa,

Kujitawala ni umma, kila hayo kuamua,

                   Kujitawala si kama, ulanguzi na rushuwa.”

(b) Muundo wa tarbia:

Ni muundo ambao kila ubeti unakuwa na mistari minne. Mshairi ametumia muundo wa tarbia katika mashairi takrimu yote. Miongoni mwa mashairi hayo ni “Afrika” (uk. 1-2), “kisomo cha manufaa” , “vielezeo” , “kiswahili”, “ uokolewe”, “madanganyano” , “wenye vyao watubana” , “chaka”, “kibwangai” , “usimpige mkeo”, “Rushwa” , “usafi” ,“ vitendawili”,“beni” ,“Hili mnatutakia” , “Wazazi”, na “ si vyema”.Kwa mfano, katika shairi la “usafi”, mshairi anasema:

“kipindupindu twajua, maradhi yanohiliki,

Usafi ni yake dawa, kufanyiza hatutaki,

Hatua ikichukuwa, serikali twaichukia,

(c)  Muundo wa takhmisa

Ni muundo ambao kila ubeti unaundwa  kwa mistari mitano. Mashairi yaliyotumia muundo wa takhmisa katika diwani hii ni “kurumbizi,“Punda”, na “Bahati”. Kwa mfano katika shairi la “kirumbizi”, mshairi anasema:

    “siye wewe kirumbizi, wa kubughudhi kichaka,

     Si mema mapendekezi, ukae ukitumbuka,

     Kuponda haipendezi, ambacho kinakuweka,

    Usiwe mpopotozi,na hayo ukatamka,

    Mbona unaghafilika, nakuhasa kurumbizi,”

 

Ø Kigezo cha idadi ya vipande

Kwa kuzingatia idadi ya vipande kwa kila mchororo katika ubeti wa shairi mwandishi wa diwani hii ametumia muundo wa vipande viwili (ukwapi na utao).Huu ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na vipande viwili,yaani kipande cha kwanza (ukwapi) na kipande cha plili    ( utao).Mashairi yote ya diwani hii yametumia muundo wa vipande viwili.Kwa mfano katika shairi la “ulezi kazi”,mshairi anasema;

“kulea mwana ni kazi, natakan ifahamike,

 Hii tabu ya uzazi, hupita majir yake,

Hubakia kwa mlezi, mzigo kichwani mwake,

         Kazi kumlea mwana, uzazi ni uraufu,

 

Ø Kigezo chya aina ya vituo:

Kwa kuzingatia kigezo cha aina ya vituo,mwandishi wa diwani ya KIMBUNGA ametumia miundo ifuatayo:-

 

 

 

 

(a) Muundo wa kituo bahari

Kituo bahari ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao hujirudiarudia kwa kila ubeti. Mashairi yaliyotumia kituo bahari katika diwani hii ni “kimbunga” (uk. 8-10), “Afrika” , “Kiswahili”, “Uchawini” , “usimpige mkeo”, “usafi”, “Vitendawili” ( “mtu wa namna hiyo”, “hongera”,“kazi” , “Hili mnatutakia”, “ Wazazi”, “Sivyema” , “ karumbizi”, “Punda”,“Paka”, “ulezi kazi”, “ Dhamana” , “Vijana wa Zanzibar”, “wacha hayo “, “usimalinze” (, “ndiye avumaye”,“makarafuu” ,“Dawa ya deni kulipa”,“mpewa hapokonyeki” , “Bahati”, “Si uzito wa latili” ?, “Hayafiki mitaani” “Dumuzi” , “Chuwi”, “madereva” ?, na “Sitaki” .

Katika shairi la “wazazi”,mshairi anasema.

                  “wazazi ni yako ngao, udumu na kuwaenzi,

                 Usikasirike nao, kaa nao kwa mapenzi,

                 Wakifurahika hao, juwa huna pingamizi,

                  Usiwauzi wazazi, hiyo ndio yako ngao,

 

                  Baada ya kukuzaa, wakawa na kubwa kazi,

               Chakula cha kuvaa, kukuwekea simanzi,

               Wala hawakuzubaa, kukupa mema malenzi,

               Usiwauzi wazazi, hiyo ndiyo yako ngao.”

 

(b) Muundo wa kituo nusu bahari

Kituo nusu baharini ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao sehemu tu ya mshororo (mstari) hujirudia kwa kila ubeti wa shairi.Mara nyingi katika kituo nusu bahari, kipande kimoja tu cha mshororo wa mwisho wa ubeti hurudiwa katika beti za mashairi. Mashahiri yaliyotumia muundo wa kituo nusu bahari katika diwani hii ni “mnapata kitu gani?”, “ Wasia” , “Nimuite jina gani”, “kasa”, “ Sifa ya mke” .

Katika shairi la “ nimute jina gani” , mshairi anasema:-

“Ninalo suali langu, wamalenga msikie,

             Ilivyo na ndugu yangu, na mimi ndiye kakaye,

 Amemuowa mwanagu, aliye nihusu mie,

     Mke nimuite vipi, mwanangu au shemeji.

 

                Nimuite vipi mke, na hata ielekee,

                           Kwani ni mjomba wake, na mume ni kakae,

                Jina gani litumike, mkwe au shemejie,

           Lipi litaelekea, mwanangu au shemeji.”

 

(c)  Muundo wa kituo kimalizio

Kituo kimalizio ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao haujirudiirudii kwa kila ubeti.Hii inamaana kuwa kwa kila ubeti wa shairi kuna kuwa na mstari wa mwisho (kituo) na tofauti au usiofanana na beti nyingine.Mashairi yaliyotumia muundo wa kituo kimalizio katika diwani hii ni “kisomo cha manufaa”, “vielezeo” , “uokolewe” , “madanganyano” , “ kujitawala”, “kibwangai” , “Beni” , “minazi chotara” , “kipaji”  na “tenga” .katika shairi la “kibwangai”. Mshairi anasema;

“kibwangai lipoona, ni mtu kakamiliya,

Akaanza kujivuna, na dharau kuzidia,

         Wala hakujali tena, wenzake walimwambiya,

      Akahisi hawi nyani, umbo lile litadumu,

 

               Kawa na tabia moja, nyani walipomwendea,

               Akajifunga mkaja, mijiwe kuwalushia,

               Hakujali zao haja, wala kuwahurumia,

              Kapiga na kukemea, pia na kuwashutumu.”

 

Ø Kigezo cha muundo kwa kuzingatia mpangilio wa mashairi:

Katika kigezo au kipengele hiki kinachochungunzwa ni jinsi/malenga mshairi alivyoyapanga mashairi yake ndani ya diwani.Kinachoangaliwa kwa makini ni kama mashairi yamepangwa kwa utaratibu maalumu au mashairi yamechanganywa; mfano uchanganyaji wa  mashairi ya mapenzi, kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni. Je mshairi ameyapanga mashairi ya kimapenzi peke yake, akaja mashairi ya kisiasa baadae kuchumu, kiutamaduni,n.k?  Mwandishi wa diwani ya KIMBUNGA hajayapanga mashairi yake kwa usahihi au maalumu kwani amechanganya mashairi ya kimapenzi, kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni.

 

MANDHARI

Mshairi wa diwani ya KIMBUNGA ametumia mandhari yafuatayo:-

(a) Mandhari ya bara ya Afrika

Mshairi anazungumzia mambo,kero, shida au matatito mbalimbali yanayokabili bara la Afrika, ikiwemo nchi Tanzania kupitia mashairi ya “Afrika” , “Kiswahili” , “vijana wa Zanzibar”.Mshairi ametaja nchi moja wapo ya bara la afrika ambalo ni Tanzania, hasa Zanzibar.

 Pia, mshairi ametaja maeneo kama mji wa Siyu na pori la Bweleo, ambayo yamo ndani ya bara la Afrika.Mandhari ya bara la Afrika yanaibua dhamira za unafiki,usaliti,amani,chazo/asili ya Kiswahili, upotoshaji wa mila,mmomonyoko wa maadali wa maadili (uvutaji wa bangi na ujambazi/wizi),ukosefu wa uzalendo na utoaji wa wasia.

(b) Mandhari  ya  porini,baharin na shambani. Mandhari yote haya yanaibua dhamira za umaskini,unyonyaji,uongozi mbaya,dhuluma na usaliti.

 

Kwa kumalizia, diwani hii iliandikwa na Haji gora Haji mnamo mwaka 1994 akizungumzia kwa kiasi kikubwa matukio yanayohusu nchi za bara za Afrika, hasa katika visiwa vya Zanzibar nchini Tanzania ingawa maudhui yake yanasadifu wakati tulionao hivi sasa katika nchi zinaziendelea, ikiwemo nchi ya Tanzania.

 

WAHUSIKA

Mwandishi wa diwani ya kimbunga ametumia vikundi kama ifuatavyo:-

(a)   Wahusika wanasiasa na wabepari

Mshairi amewatumia wahusika wanasiasa na mabepari katika mashairi ya “kimbunga” , “Afrika” ,“Madanganyano”  na “wenye vyao watubana” . Wahusika hawa wanawakilisha tabaka la juu (tawala) linalonyonya, linalodhurumu, linaloonea na linalokandamiza tabaka la chini.Wahusika wanasiasa ni wabinafsi, waongo, wasaliti, wadhulumaji, waqnafiki na wasiowajibika katika kazi zao.

(b) Wahusika wakulima

Mshairi amewatumia wahusika wakulima katika shairi la”madanganyano”, wahusika hawa wanawakilisha watu wa tabaka la chini,maskini na wanaonyonywa na kukandamizwa na watu wa tabaka la juu (viongozi na mabepari au matajiri)

c)Matumizi ya Lugha

Mwandishi ametumia lugha rahisi iliyoshehenezwa lahaja ya Kiunguja yenye mafumbo na taswira mbali mbali pamoja na  tamathali za semi kidogo na misemo kwa kiasi.

d)TAMATHALI ZA SEMI

Tashibiha

Ø Kwenye shairi la “Sifa ya Mke” (uk 40)

·        Ufedhuli na uovu kama yake mazoea.

·        Awe kama malaika mzuri kupindukiya

Tafsida

Mwandishi ametumia mbinu ya kufumba kwa kusema maneno makali,machafu,matusi kwa kutumia tafsida.Mfano shairi la “Nyang’au”linahusu tamaa,Paka” linahusu wizi, shairi la “Dumuzi” linakemea uvivu,n.k.

Mbinu Nyingine za Kisanaa

Takriri

Mwandishi ametumia takriri ili kuweka msisitizo mfano shairi la “Kujitawala” (uk 7-8) neno kujitawala limerudiwarudiwa.

Matumizi ya Taswira

Mwandishi ametumia taswira nyingi kama vile;

Kimbunga …(uk 1)…..Kuashiria mapinduzi

Kibwangai…(uk 9)….Kuashiria viongozi wasaliti

Nyani…..(uk 9)…….Kuashiria wananchi waliosalitiwa

Chuwi…..(uk 42)…..Kuashiria ukoloni mamboleo, n.k.

Jina la Kitabu

Jina la Kitabu Kimbunga halisadifu yale yaliyomo ndani ya kitabu kwa sababu hatuyaoni mageuzi yoyote ambayo anayajadili katika kitabu hiki zaidi ya mashairi ya maadili mema na maonyo ya kimaisha.Asilimia kubwa ya mashairi katika diwani hii yamejadili juu ya maonyo na maadili katika maisha.

 

Kufaulu kwa Mwandishi

Kimaudhui

Mwandishi amefaulu ;

Ø Kutoa maadili mema na maonyo katika jamii

Ø Kujadili dhamira ya ujenzi wa jamii mpya

Ø Ameonesha mbinu mbalimbali za kufuata ili tufanikiwe katika ujenzi wa jamii mpya

Kifani

Ø Ametumia lugha rahisi, mafumbo, taswira, n.k.

KUTOFAULU KWA MWANDISHI

Kimaudhui

Ø Baadhi ya maadili aliyoyajadili katika diwani hii ameyajadili kidhanifu,ni sawa na yale tunayoyapata makanisani, ambayo yana nafasi ndogo sana katika ujenzi wa jamii mpya

Ø Vile vile amejadili masuala mbalimbali kidhanifu hasa anapomhusisha Mungu.Kama vile masuala ya kipaji (uk 38-39), bahati (uk 36), umaskini (uk 35).

Kifani

v Mwandishi ametumia  lahaja ya Unguja badala ya Kiswahili sanifu ivyo ni vigumu  kueleweka kwa watu wote.

v Diwani hii ni ya hali ya chini sana katika muundo,mtindo na baadhi ya vipengele vingine vya kisanaa.

 

 

 

Powered by Blogger.