SEC-LUGHA-TAFSIRI NA UKALIMANI

 


TAFSIRI NA UKALIMANI

Tafsiri ni zoezi la uhawilishaji wa  mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa bila kubadilisha maana ya ujumbe.

 

DHANA MBALIMBALI

Ø  Uhawilishaji – ni uhawilishaji wa ujumbe au mawazo kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine kwa njia ya maandishi au mazungumzo.

Ø  Mfasiri – ni mtu yeyote anayejishughulisha au kufanya tafsiri. Ni mtu mwenye taaluma au ujuzi wa kutafsiri na ambaye anajishughulisha na shughuli hizo.

Ø  Matini – ni wazo au mfululizo wa mawazo wenye utoshelevu wa kimaana na unaohitaji kutafsiriwa. Matini yanaweza kuwa neno, kirai, kishazi, sentensi au aya.

 

      AINA ZA MATINI.

a)      Matini Chanzi (M.C) – ni matini iliyo katika lugha yake ya awali kabla ya haijatafsiriwa.

b)      Matini Lengwa (M.L) – ni matini iliyo tafsiriwa kutoka lugha yake ya awali.

c)      Mtini Elezi – ni matini ambayo huegemea upande wa mwandishi.Mfano matini za kisheria,

                               maandishi binafsi kama vile shajara (diary),wasia, nk.

d)     Matini Arifu – ni matini ambayo hulenga kutoa taarifa au maarifa kuhusu jambo fulani.   

                                    Mfano vitabu vya taaluma na masomo mbalimbali. Nk.

(e) Matini Amili – ni matini ambazo huegemea upande wa hadhira,mwandishi huchoochea hisia

    za wasomaji na kuwafanya watende kama ambavyo yeye mwandishi anataka wafanye au watende. Mfano kadi au barua za mwaliko, matangazo mbalimbali kama vile ya vipodozi, jeshi nk.

 

DHANA MBALIMBALI

Ø  Lugha Chanzi – ni lugha iliyotumika kuandika matini chanzi.

Ø  Lugha lengwa – ni lugha inayotumika kufanyia tafsiri au ni lugha inayotumika kuandikia matni lengwa.

Ø  Kutathmini tafsiri – ni kitendo cha kusoma kwa matini iliyo tafsiriwa na kuitolea hukuuamu juu ya ubora na udhaifu wake. Wakati mwingine hujulikana kama kuhakiki tafsiri.

Ø  Tafsiri pana - -ni tafsiri inayozingatia maana na mtazamo wa kiujumla kuhusu jambo au dhana inayozungumziwa wakati katika matini chanzi jambo au dhana hiyo imeelezwa katika umahususi wake. Mfano kutafsiri neno “kisamvu” kama vegetable ni tafsiri pana kwani imetazama katika ujumla ikiwa kisamvu ni aina fulani tu ya vegetable.

Ø  Tafsiri Finyu – ni tafsiri ambayo jambo au dhana hufafanuliwa katika misingi ya umahususi wake wakati katika matini chanzi imeelezwa kiujumla jumla. Au ni tafsiri inayotoa maana finyu zaidi kutoka maana inayolingana na matini chanzi. Mfano kutafsiri neno ‘filling station” kama “sheli” ni tafsiri finyu kwa sababu  Sheli ni aina moja tu ya kituo cha mafuta.

Ø  Tafsiri mbovu/ tenge -ni tafsiri ambayo imepotoshwa kiasi kwamba maana inayokusudiwa katika matini chanzi ni tofauti kabisa na maana inayotolewa katika matini hiyo. Tafsiri tenge huweza kusababishwa na mambo kadhaa kama vile ;-

·         Kutojua maana halisi ya neno lililo tumika katika matini chanzi.

·         Tofauti za kiutamaduni kati ya lugha chanzi na lugha lengwa.Mfano kutafsiri neno “Rarely” badala ya often ni tafsiri. Kutafsiri neno corporal punishment kama adhabu ya viboko badala ya adhabu ya kifo kisheria ni tafsiri tenge.

Ø Tafsiri rejeshi – ni mchakato wa kutafsiri matini ambayo tayari imeshatafsiriwa kutoka lugha fulani na kuirejesha tena katika lugha chanzi kwa lengo la kuitathmini tafsiri hiyo. Mfano Ikiwa tafsiri ilifanywa kutoka Kiswahili kwenda kiingereza basi tunapoitathmini tafsiri hiyo kwa kutumia tafsiri rejeshi tunaitafsiri tena toka Kiingereza kwenda lugha ya kswahili.

Ø Tafsiri sahihi – ni tafsiri ambayo kwa kiasi kikubwa ina kubalika na kuvumilika kwa sababu muundo na maudhui ya matini chanzi vimezingatiwa katika matini lengwa.

 

UMUHIMU/ DHIMA YA TAFSIRI

Ø Ni njia ya mawasiliano inayofanya kazi kati ya watu au jamii mbili zinazotumia lugha tofauti. Mfano Kiswahili na Kiingereza.

Ø Ni nyenzo ya kueneza utamaduni. Mfano kupitia dini,vitabu vimetafsiriwa kwa lugha mbalimbali.Mfano I will mery when I want – Kiingereza Nitaoa nitakapotaka – Kiswahili

Ø Ni mbinu ya kujifunza lugha – mfasiri anapofanya kazi ya kutafsiri matini mbalimbali hukutana na changamoto mbalimbali na anapofaya jitihada za kutatua matatizo hayo hujikuta anajifunza lugha.

Ø Tafsiri ni kiliwazo cha mfasiri – tafsiri humfanya mfasiri afurahi,aridhike na aburudike hasa anapopata suluhisho la changamoto za kutafsiri zilizokuwa zinamkabiri.

Ø Tafsiri ni kazi au ajira kwani umpatia mtu kipato.

 

SIFA ZA MFASIRI  BORA

Ø Awe mahari wa lugha husika yaani azifahamu  lugha zote mbili.

Ø Awe mjuzi wa tekinolojia habari na mawasiliano (Tehama) kwasababu baadhi ya kazi                              atalamika kutumia vifaa mbalimbali kama vile Tanakilishi (kompyuta).

Ø Afahamu vizuri watu jamii na utamaduni wao.

Ø Apende kujisomea na ajiendeleze kulingana na mabadiliko ya jamii yaani ajue vitu vingi.

Ø Afahamiane na watu wengi wa fani au sekta mbalimbali kwa kazi atakazofanya ni za watu mbalimbali na tofauti tofauti.

Ø Ajue misingi ya tafsiri.

Ø Awe na misamiati ya kutosha na ajue kanuni au sheria za lugha husika.

 

MAADILI YA MFASIRI

Ø Awe mwaminifu kwa wateja wake na matini aliyopewa.Mfano katika itikadi.Mfano mfasiri si mlevi kabisa lakini analetewa matini inayosifia pombe,hapaswi kubadili chochote kutokana nayeye kutopenda pombe bali anapaswa kuitasiri kama ilivyo,huo ndo uaminifu wa mfasiri.

Ø Awe na bidii katika kazi yake ili afanye kazi kwa wakati na awarudishie wateja wake kwa wakati bila kwazo au mgogoro wowote na wateja wake,Hii itamsaidia mfasiri aendelee kuaminiwa na kuletewa kazi za kutafsiri.

Ø Awe nadhifu wa moyo na muonekano yaani katika mavazi,kauli kwa wateja n.k ili aendelee kuaminiwa na wateja wake.

Ø Anapaswa kuzingatia taratibu za kazi yake.Mfano makubaliano na mteja wake yanapaswa yawe kimaandishi na mkataba utaje jina la mteja,jina la mfasiri, aina ya kazi nk.

Ø Awe na ushirikiano na watafasiri wenzake pamoja na watu mbalimbali wa sekta nyingine.

Ø Aepuke vishawishi au asiwe na tamaa.Anapaswa kuwa na msimamo yaani asijipendekeze kwa mteja wala asijishushe Mfano kupunguza bei.

 

MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA UCHAMBUZI WA MATINI.

Uchambuzi wa matini -  ni kusoma matini husika na kuielewa kabla ya kuanza kuitafsiri.Mambo ya kuzingatia wakati wa uchambuzi wa matini ni kama yafuatayo;-

Ø  Kubaini lengo la matini yaani mfasiri anapaswa abaini lengo la matini chanzi.

Ø  Kubaini lengo la kufasiri.Mfasiri ni lazima ajue lengo mahususi la tafsiri yake.Je anataka msomaji apate athari inayolingana na ile ya wasomaji wa matini chanzi.

Ø  Kubaini wasomaji na umbo la matini lengwa -  mfasri hana budi kufahamu hadhira ya matiini chanzi na abaini hadhira mahususi ya matini lengwa yake.Mfano elimu,umri na tabia nk. Kwa upande wa umbo mfasiri afahamu tafsiri hiyo itasomwa kama kitabu, jarida ama gazeti n.k.

Ø  Kubaini mtindo wa matini chanzi-mfasiri anapaswa abaini mtindo wa matini chanzi kwani mtindo wa matini chanzi unapaswa ulingane na ule wa matini chanzi mfano ikiwa matini chanzi ni shairi basi hata matini lengwa inapaswa iwe shairi n.k.

Ø  Kubaini ubora na mamlaka ya matini chanzi–ubora na mamlaka ya matini chanzi hubainika kwa kuangalia lengo la maadhishi na mahitaji ya matini aliyoandika.Mamlaka ya matini chanzi hudhihirika kwa kangalia iwapo matini chanzi imeandikwa vizuri pamoja na hadhi ya mwandishi wake.Mfano ikiwa ni matini ya Kiswahili basi iandikwe na mwanasheria gwiji.

Ø  Usomaji wa matini mara yamwisho -  mfasiri asome mala ya mwisho matini chanzi huku akipigia mstari istilahi na maneno muhimu ya matini hiyo ili yasisahaulike kuzingatiwa kwa umakini wakati wa kutafsiri.

 

VIPENGELE VYA UCHAMBUZI WA MATINI.

Kuna vipengele vikuu vitatu ambapo kila kipengele kina hatua kadhaa ndogondogo kama ifuatavyo:-

( a ) Kusoma matini nzima au yoe -faida au vipengele vyake vidogovidogo ni kama vile

Ø  Husaidia kuandaa marejeleo muafaka kama vile kamusi ya lugha ya kwanza na yapili.

Ø  Husaidia kuandaa orodha ya istilahi na visawe

Ø  Kugawa Sehemu au vipengele miongoni mwa wafasiri hasa kama matini ni kubwa.

( b ) Kuchambua matini yenyewe – uchambuzi wa matini hulenga kupata sifa bunifu za matini

               husika.Kipengele hiki kina hatua tano kama vile:-

Ø  Kubaini lengo la mwandishi, kama vile kubeza,kusifu,kukweza,kukashifu au kutoegemea upande wowote katika uandishi,mwandishi anaweza kuwa na mitazamo miwili au zaidi.

·         Mtazamo chanya kwa mtendwa. Mfano yanga yaichabanga simba.Mwandishi huyu ametumia neno chabanga ni mtazamo hasi yaani au kwani amefurahia samba kufungwa.

·         Mtazamo chanya kwa mtenda.Mfano yanga yafuta uteja  kwa Simba. Mwandishi  huyu anaonesha anafurahia yanga kuifunga simba.

·         Mtazamo wa kati– mfano yanga yaifunga simba 3 kwa 0 (sifuri),Mwandishi huyu haoneshi kuegemea upande wowote.

Ø  Kubaini lengo la mfasiri au mteja– mfasiri ajiulize kwanini anataka kutafsiri matini husika?.Na kwanini mteja wake anataka itafsiriwe?.Hivyo mfasiri anapaswa kuepuka upendeleo au kuegemea upande mmoja badala yake awe na msimamo au mtazamo wa katikati.

Ø  Kubaini hadhira na umbo la matini – mfasiri ajiulize maswali kama vile: hii ni aina gani ya matini? Aina hii ya matini hutafsirika vizuri kwa njia ya aina gani?, Hadhira lengwa ya zao la tafsiri ni ipi? Na  inalengo  gani?,Mfano Elimu, Umri, Mahali wanapo ishi nk. Zao la tafsiri iwe katika  umbo gani? Mfano Ripoti, tasirifu, kiatabu nk.

Ø  Kubaini mtindo wa matini – ni muhimu sana mtindo wa  matini  chanzi ujitokeze kwenye matini lengwa yaani tafsiri yake. Mfano monolojia, Dayalojia, Hadithi, lugha za mitaani,  mitindo ya kidini nk. Mitindo  hii ikiwa umetumiwa katika matini chanzi inapaswa ijitokeze pia katika matini lengwa.

Ø  Kubaini ubora na mamlaka ya matini chanzi –ubora wa matini chanzi hutokana na kuzingatia vipengele mbalimbali vya kiisimu vya lugha.Mamlaka ya matini chanzi hutokana na hadhi na ubobevu wa maadishi katika taaluma husika.Mfano matini ya kisheria ni vyema iandikwe na mwanasheria gwiji maana yake mwanasheria mbobevu.

( c).    Kusoma matini kwa mara ya mwisho – katika kipengele hiki mfasiri asome tena matini chanzi kutoa taswira au kuweka alama maneno au mambo muhimu katika matini hiyo, baadhi ya mambo ay maneno muhimu yanayo paswa kuwekewa alama ni  :- Majina mahususi ya watu, Sehemu, mwaka nk. Maneno, virai au sentensi ambazo hazitafsiriki kiurahisi.

 

HATUA/ MCHAKATO WA KUTAFSIRI MATINI

Ili kupata matini lengwa inayoeleweka na kukubalika kwa hadhira ni lazima mfasiri apitie hatua mbalimbali katika kutafsiri. Hatua hizo ni kama zifuatazo:-

1.Maandalizi – katika hatua hii mfasiri anapaswa kusoma matini chanzi mara kadhaa ili kujilidhisha kuhusu maudhui yake,mtindo wake na kuziwekea alama maalum Sehemu au vipengele vinavyopaswa kupewa kipaumbele.Vilevile chunguza usuri wa matini chanzi, historia ya mwandishi,utamaduni wake,mazingira ya uandishi ,malengo yake na hadhira ya matini hiyo kama mfasiri ni mgeni zaidi katika utamaduni huo inapaswa kujisomea zaidi kuhusu utamaduni huo.Usuri huendana na uchambuzi wa vipengele vya kiisimu ambapo mfasiri huandika msamiati na istilahi, maneno ya kiutamaduni na Sehemu ngumu kueleweka ili azifanyie kazi.

 

2.Uchambuzi – katika hatua hii mfasiri hufanyia kazi yale aliyobaini ktika hatua ya Maandalizi. Hatafuta visawe vya msamiati na istirai ngumu au ngeni kwa kutumia marejeo mbalimbali kama vile Ensaikolopidia na kamusi. Inashauliwa kuwa mfasiri awe na kompyuta au daftari au faili kwa ajili ya kutunzia msamiati au istirahi zitakazo tumika

.

3.Uhawilishaji – katika hatua hii mfasiri huhawilisha taarifa kutoka kwenye matini chanzi kwenda kwenye matini lengwa.Mfasiri anatakiwa kuzingatia sarufi ya lugha lengwa isipokuwa anapotumia tafsiri ya neno kwa neno.

 

4.Kusawidi rasimu ya kwanza –Baada ya kazi ya tafsiri inayo patikana baada ya uhawishaji wa visawe kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa kukamilika ni rasmu ya kwanza ya tafsiri. Rasimu ya kwanza ya tafsiri iliyo sawidiwa inaweza kuwa na dosari kadhaa kwa hiyo haifai kupelekwa kwa mteja au hadhira lengwa kama ilivyo,hivyo basi mfasiri hulazimika kuidurusu rasimu hiyo ili kuondoa dosari

 

5.Udurusu wa rasimu ya kwanza – Baada ya rasimu ya kwanza kukamilika lazima ipitiwe tena na kurekebishwa au kudurusiwa na mfasiri hupata fursa ya kwanza ya kuitathimini na kuifanyia marekebisho tafsiri yake mwenyewe. Kazi ya kudurusu haipaswi kufanya haraka.Hatua hii ya kudurusu huhusisha shughuli zifuatazo:-

Ø  Kusahihisha makosa ya kisarufi na miundo isyoeleweka vizuri.

Ø  Kuonesha sehemu zenye tafsiri ya mzunguko na zenye matumizi

Ø  Kurekebisha sehemu zenye muunganiko mbaya au tafsiri tenge zinazozuia mtiririko mzuri wa matini.

Ø  Kuhakiki usahihi na kukubalika kwa maana zinazowasilishwa katika matini lengwa.Katika shughuli hii tunaangalia kama kuna mambo yameongezwa, yamepunguzwa,yamepotoshwa au kubadilishwa.

Ø  Kuhakiki kukubalika kwa lugha iliyotumika katika tafsiri kwa kuzingatia umbo lililo tumika kuwasilisha matini lengwa na mada ya matini chanzi.

Ø  Kama iwapo mada au ujumbe mkuu wa matini chanzi unajitokeza waziwazi katika matini lengwa.

 

6.  Kusomwa kwa rasimu ya pili na mtu mwingine -Msomaji wa rasimu ya pili anaweza kuwa mfasiri mwingine au mhakiki au muhariri wa tafsiri,pia anaweza kuwa mteja wa tafsiri inayohusika au mtu mwingine yeyote mwenye uwanja uliotafsiriwa.

 

7.Kusawiri rasimu ya mwisho–katika hatua hii mfasiri hufanyia kazi maana na mapendekezo ya msomaji ambaye amempa kazi yake matokeo ya kufanyia kazi maoni hayo humwezesha kuandhika rasimu nzuri ya mwisho ambayo ndio humfikia hadhira.

 

MBINU / AINA/ NJIA ZA KUTAFSIRI

Katika kutafsiri matini kuna njia, aina, au mbinu nne kama zifuatazo:-

A. TAFSIRI YA NENO KWA NENO –Ni mbinu ya tafsiri ambayo maneno yake hutafsiriwa kiupeke upeke kwa kuzingatia maana za msingi za lugha chanzi lakini kwa kufuata sarufi hasa sintaksia ya lugha lengwa.Mfano

i)     Kiingereza => pull             up        your                  socks

                           Vuta              juu       yako                 soksi

   Kiswahili => vuta    socks   zako    juu

ii)   Kiswahili => mtoto wa nyoka ni nyoka, Kiingereza => A child of snake is snake.

 

FAIDA YA MBINU HII

Ø  Husaidia kujua muundo wa kisarufi wa lugha chanzi

Ø  Hutumiwa na wanaisimu katika kuchambua sarufi ya lugha mbalimbali.

 

UDHAIFU WA MBINU HII

Ø  Mbinu hii inashindwa kufikisha ujumbe wa lugha chanzi katika lugha lengwa ya sarufi kwa sababu kunakuwa na upotoshaji wa maana ya lugha chanzi latika lugha lengwa.

Ø  Misemo hutafsiriwa kwa makosa.

 

B.     TAFSIRI YA KISEMANTIKI

Ni mbinu au njia ya tafsiri ambayo huegemea zaidi kwa mwandishi wa matini chanzi ambapo maana na vipengele vidogovidogo hutiliwa maanani. Aina hii ya tafsiri hufanya kazi ya tafsiri iwe na taarifa nyingi.Mara nyingi tafsiri ya kisemantiki hujali zaidi maana na muundo wa matini chanzi. Mfano:

Kiingereza :Tanzania electric suppy company ltd,

Kiswahili :Shirika la ugavi wa umeme Tanzania.

 

 

Kiingereza: where is a purpose, there is no failure.

Kiswahili:  palipo na nia, hapana kushindwa.

 

Kiswahili:  hapa kazi tu.

Kiingereza: here job only

 

Mifano hiyo hapo juu inaonesha kwamba kila neno katika matini chanzi limetafsiriwa katika lugha lengwa hivyo basi matini lengwa zimekuwa na taarifa nyingi ambazo sio sahihi,mbinu hii ina uwezo mkubwa wa kuendeleza lugha lengwa kwa kuingiza miundo ya maneno toka lugha chanzi kwenda lugha lengwa . mfano:-

Ladies and gentlemen: Mabibi na mabwana.

At the end of the day – mwisho wa siku

Under the chair manship of – chini ya uwenyekiti wa

 

C.    TAFSIRI  YA KIMAWASILIANO.

Ni tafsiri ambayo huzingatia kueleweka kwa ujumbe kwa hadhira lengwa.Huzingatia historia, muktadha, utamaduni na itikadi ya mzungumzaji wa lugha lengwa.Hivyo ni tafsiri inayoilenga hadhira kwani humjali zaidi msomaji wa matini lengwa. Ni tafsiri iliyowazi, huru, na inayoeleweka kwa urahisi na wakati mwingine hujulikana kama tafsiri huru. Hii ndio aina ya tafsiri au mbinu inayoonekana kuwa na mashiko zaidi kwasababu haina utata wowote kwa hadhira ya lugha lengwa. Mfasiri hapaswi kufungwa na miundo ya lugha chanzi kwani kinacho lengwa ni kueleweka kwa ujumbe kwa hadhira. Mfasiri hufuata sarufi ya lugha lengwa na yuko huru kutafuta maneno au mafungu ya maneno na nahau,misemo,methali,tamaduni na mazingira ya lugha lengwa katika kueleza ujumbe unaotolewa na matini chanzi.Mfano;

Kiingereza: Tanzania Electric supply campany limited

Kiswahili: shirika la umeme Tanzania.

 

Kiingereza: there is a purpose, there is no failure

Kiswahili: penye nia pana njia

 

Tafsiri zilizotolewa katika mifano hapo juu zimefanyika kwa kuzingatia miundo na maana zake katika lugha lengwa ndio maana hatuoni kila neno lililokuwa limetafsiriwa pwekepweke.Aidha misemo katika mfano wa pili umetafutiwa msemo unao fanana nao katika lugha lengwa badala ya kutafsiri kisisisi.

 

 

 

FAIDA ZA MBINU HII

Ø  Mbinu hii hutumiwa kutafsiri matini nyingi duniani.

 

UMUHIMU WA MCHAKATO WA KUTAFSIRI

Ø  Husaidia mfasiri kufanya maandalizi yote muhimu ya kutafsiri yanayohitajika.Hii inapelekea kupata maana sahihi za istilahi mbalimbali.

Ø  Humsaidia mfasiri kutoa tafsiri sahihi ya matini chanzi kwenda kuwa matini lengwa.

Ø  Humfanya mfasiri hutafsiri kwa kuzingatia mazingira na utamaduni wa hadhira lengwa, n.k.

Ø  Hufanya kazi ya tafsiri isiwe na makosa madogomadogo ya kimaana na kimuundo.

Ø  Hurahisisha kazi ya kutafsiri na kuifanya iwe nyepesi zaidi isiyo na shida.

 

UMUHIMU WA TAFSIRI KATIKA JAMII.

Ø  Husaidia kuleta istilahi za kufundishia. Mfano Kiingereza kimetafsiri maneno mengi toka lugha ya kigiriki na kiratini.

             Mfano Kigiriki                                   kiingereza

                        Physics                                    physics

                        Chemia                                    Chemistry

Ø  Husaidia kutafsiri istilahi mbalimbali za kimataifa toka lugha chanzi kwenda lugha lengwa.

           Mfano Kiingereza                                Kiswahili

                      Asprin                                        Aspirini

                       Tyre                                          Tairi

                      Globalization                             Utandawazi

                         E-mail                                     Barua pepe

                           Fax                                        Nukushi

Ø  Husaidia katika kubuni na kuunda majina ya biashara katika lugha ya Kiswahili.

                  Mfano Sabuni chapa foma inatokana na foam.

                 Sabuni chapa Kodrai – inatokana na Codray

                 Kileo chapa Konyagi – inatoka na Cognac

Ø  Husaidia kutafsiri vitabu mbalimbali vinavyosomwa na watu wote.

Ø  Husaidia kuleta istilahi za kisayansi na kitekinolojia katika lugha ya Kiswahili.

              Mfano:Kiingereza                             Kiswahili

                         Radio                                     Redio

                        Television                                Televisheni

                         Computer                               kompyuta/Tanakilishi

Ø  Husaidia kuleta uhai wa lugha yaani kubadilika kimsamiati kulingana na wakati hasa kuakisi matukio mablimbali. Mfano

                 Mfano  Kiingereza                         Kiswahili

                             Stakeholder                      - mwanzo – washika dau

                                                                       - sasa – wadau

                                                                                                                

                              Globalization                  - Mwanzo – udandazi

                                                                        -Sasa - utandawazi

Ø  Husaidia sana katika vyombo vya habari, mfano redio, runinga na magazeti.

 

HASARA ZA TAFSIRI KATIKA UTAMADUNI

Ø  Tafsiri zimesababisha jamii za Afrika kuiga utamaduni wa nje.

Ø  Tafsiri imesababisha mivutano ya makundi ya kidini kati ya nchi kwa nchi na jamii kwa jamii.

Ø  Baadhi ya njia za tafsiri husababisha kwenda kinyume na sarufi ya lugha lengwa au utamaduni wa lugha lengwa.Mfano I like banana more than orange-Mimi penda ndizi zaidi  kuliko chungwa.

Ø  Husababisha matumizi mabaya ya lugha ya Kiswahili hasa pale ambapo mzungumzaji anaamua kuzungumza lugha mbili katika uzungumzaji wake.

 

 

 

UKALIMANI

Ni  uhawilishaji wa ujumbe ulio katika mazungumzo kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa. Au ni uhawishaji wa mawazo moja kwa moja kutoka lugha moja ya mazungumzo kwenda lugha nyingine ya mazungumzo bila kubadili maana.

 

Mkalimani – ni mtu anayefanya kazi ya kuhawilisha ujumbe ulio katika mazungumzo toka lugha chanzi kwenda lugha lengwa.

 

SIFA ZA MAKALIMANI BORA.

Ø  Awe mjuzi wa hali ya juu wa lugha husika na utamaduni wake.

Ø  Ajue lugha zaidi ya mbili hasa za kimataifa.

Ø  Awe na ujuzi au maarifa ya kutosha ya mada au taaluma husika.

Ø  Awe na ujuzi wa taaaluma ya ukalimani.

Ø  Awe machapakazi,mdadisi na we mpenda kujienedeleza kupata habari.

Ø  Awe na kipaji katika kutunza kumbukumbu kuteua msamiati sahihi haraka, kuunda istilahi zinazo kubalika na awe na ulumbi yaani uwezo wa kushawishi na mvuto wa kiuzungumzaji.

 

MAMBO YA MSINGI KATIKA UKALIMANI.

Kuna mambo mbalimbali ya msingi ya kuelewa kuhusu ukalimani.Baadhi ya mambo hayo ni kama yafuatayo:-

Ø  Ukalimani ni mchakato wa uhawilishaji wa ujumbe wa mazungumzo ya papo kwa papo.

Ø  Ukalimani unahusu lugha ya mazungumzo au alama.

Ø  Katika ukalimani kuna wahusika watatu ambao ni mzungumzaji, mtalijumani na msikilizaji.

Ø  Ukalimani huzingatia sarufi, utamaduni, muktadha wa tukio na mada.

Ø  Ukalimani unahusu lugha mbili tofauti ambazo ni lugha chanzi na lugha lengwa.

 

UMUHIMU WA UKALIMANI.

Ø  Ni daraja linalounganisha watu au jamii zinazozungumza lugha tofauti.Mfano kimakonde kwenda Kiswahili.

Ø  Husaidia katika masuala ya kidiplomasia na uhusiano wa kimataifa.Mfano katika utatuzi wa migogoro, n.k.

Ø  Husaidia kufanikisha vikao,mikutano na makongamano ya kimataifa na kitaifa.

Ø  Hutumika kama mbinu ya kufundishia lugha ya pili.

 

STADI ZA UKALIMANI.

Mkalimani anapaswa kuwa na stadi kuu nne (4) mbali na ujuzi wake wa hali ya juu wa lugha. Stadi hizo ni;

1.      Stadi ya kusikiliza.Mfano matamshi,lugha,maneno na kuwa makini na kile kinacho semwa.

2.      Stadi ya kuzungumza mbele za watu.Stadi hii huambatana na mavazi,usijipambe sana na punguza maelezo yasiyo na msingi.

3.      Stadi ya kujenga kumbukumbu.

4        Stadi ya kufupisha.

 

AINA ZA UKALIMANI

Kuna aina mbili za ukalimani ambazo ni:-

1.      Ukalimani fuatizi –Ni ukalimani ambao mkalimani huzungumza kisha humpa nafasi mkalimani ili akalimani.Mkalimani akimaliza humpisha mzungumzaji  na zoezi hili huendelea hadi mwisho.Ukalimani wa aina hii hufaa katika mijadala yaani kunapokuwa na mazungumzo ya maswali na majibu kama vile mkalimani atahitaji kuchukua nukuu na kumbukumbu.Ukalimani huu hufanyika katika mikutano ya wanahabari,mikutano ya kisheria ya pande mbili na kwenye kundi dogo la watu,mikutano ya kidini na hospitalini.Njia hii hutumika zaidi kwa vile haina gharama kubwa kutokana na gharama za vifaa vinavyotumika  kuwa ndogo na urahisi  wa kuvimudu.

Ø  Udhaifu wa  aina hii ni kuwa hutumia muda mrefu zaidi kwani hoja moja husemwa mara mbili kwa lugha mbili tofauti na kwa kusubiriana.

 

2.      Ukalimani sawia au sambamba – Ni aina ya ukalimani unaoshughulika na uhawilishaji wa ujumbe kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa,ambao hufanyika papo kwa papo wakati mzungumzaji anaendelea kuzungumza.Mzungumzaji na mkalimani huwasilisha ujumbe kwa pamoja bila kusubiriana na wakati mwingine mzungumzaji humwacha mkalimani nyuma kwa sekunde mbili au tatu.Mzungumzaji hasitishi mazungumzo kumpisha mkalimani na mkalimani hamsubiri mzungumzaji kama ilivyo katika ukalimani fautizi.

 

ZANA ZA UKALIMANI

Maendeleo ya sayansi na teknolojia yameibua zana mbalimbali ambazo husaidia katika zoezi zima la ukalimani hata hivyo zana za ukalimani hutegemea aina ya ukalimani wenyewe na muktadha unaohusika katika ukalimani huo.

 

BAADHI  YA ZANA AMBAZO HUTUMIKA KATIKA UKALIMANI.

1.      Kituturi.

2.      Paneli pokezi na tolezi ya sauti.

3.      Maikrofoni.

4.      Kompyuta.

5.      Jozi ya visikizo

 

Vilevile kituturi huwa kinapaswa kuwa kisicho ruhusu sauti nyingine kusikika ndani zaidi ya ile ya mzungumzaji,hii husaidia mkalimani kusikiliza sauti ya lugha chanzi kwa utulivu mkubwa. Mkalimani humuona mzungumzaji wa lugha chanzi kupitia dirisha lenye kioo angavu la chumba hicho na wakati mwingine mkalimani huweza kumuona mzungumzaji wa matini chanzi kupitia kompyuta.

 

DHANA MBALIMBALI ZA UKALIMANI

1.      Ukalimani wa kijamii – ni ukalimanni unaofanywa katika muktadha unaohusu jamii. Mfanii huduma za afya, ujenzi wa shule n.k.

2.      Ukalimani wa mahakamani – ni ukalimani ambao hufanywa na wanasheria katika mahakama mbalimbali za kisheria.

3.      Ukalimani wa mikutanoni – ni ukalimani ambao hufanywa katika mikutano ya kitaifa na mataifa.Aghalabu hufanywa ndani ya jengo au ukumbi maalumu.

4.      Ukalimani wa kitabibu – ni ukalimani ambao hufanywa katika sekta ya afya kwaajili ya kuchunguza maradhi pamoja na kutoa tiba au ushauri kwa wahusika.

5.      Ukalimani wa habari – ni ukalimani amabao hufanywa katika vyombo mbalimbali vya habari hususani ambapo lengo lake ni kufanya maudhui au taarifa ya habari iweze kuwafikia walengwa.

6.      Ukalimani sindikizi –ni ukalimani ambao mkalimani huambatana na jopo la uongozi au wataalamu katika ziara Fulani.Mfano kuongoza watalii.

7.      Ukalimani wa lugha ya alama – katika dhana hii ya ukalimani wa lugha ya alama huwa ndio lugha chanzi kwa ajili ya viziwi (wasio sikia/bubu) kama kundi moja la watu ambapo mkalimani huweza kutoa ujumbe kutoka lugha ya kusemwa kwenda lugha ya alama au kutoka kwenye lugha ya alama kwenda ujumbe wa kusemwa.

 

MAMBO YA KUZINGATIA KATIKA UKALIMANI.

Mkalimani anatakiwa kuzingatia mambo mbalimbali kama vile;

1.      Lugha – makalimani anatakiwa ajue lugha chanzi na lugha lengwa ikiwa ni pamoja na lafudhi ya mzungumzaji ayasikie vizuri mazungumzo na kuielewa vizuri habari anayo zungumza kisha aihawilishe bila tatizo lolote.

2.      Mazungumzo – mkalimani anatakiwa ajue aina ya mazungumzo atakayo kalimani ili aweze kuteua msamiati mwafaka katika mada na mazungumzo hayo.Mazungumzo hayo yanaweza kuwa ya kitaaluma,kidini au kisiasa.

3.      Hadhira – mkalimani lazima ajue hadhira inayopokea ujumbe na hana budi kuifanya hadhira iwe na ari na utayari wa kumsikiliza ili iweze kupata ujumbe.Kuijua hadhira kunamsaidia mkalimani kuchagua maneno na mtindo wa mazungumzo ili kuiwezesha hadhira kuelewa kinachosemwa.

4.      Muktadha – mkalimani anatakiwa azingatie muktadha  husika wa tukio.

5.      Ujumbe – Mkalimani azingatie ujumbe unaowasilishwa na mzungumazaji.Katika kukalimani kuzingatia zaidi ujumbe na kuvaa uhusika zaidi kuliko muundo na mtindo wa lugha chanzi.

6.      Lengo la mazungumzo–mkalimani anatakiwa kuzingatia lengo la mazungumzo na aoneshe hisia za mzungumzaji.Mfano huzuni, au furaha.

 

 

 

DHIMA ZA UKALIMANI

Ø  Ni kiungo cha mawasiliano kati ya jamii ya lugha moja na nyingine – mawasiliano hayo yanaweza kuwa ya kitaaluma,kidini au kisasa.

Ø  Husaidia kueneza utamaduni husika katika jamii tofauti–kupitia ukalimani jamii hupata kujua tamaduni za jamii nyingine hususani mazungumzo yanayohusu utamaduni,vyakula na michezo mbalimbali.

Ø  Husaidia katika shughuli za kidiplomasia–ambapo kunakuwa na watumiaji wa lugha tofauti mfano kuhusu  migogoro.

Ø  Hadhira au wasikilizaji wamazungumzo huweza kujifunza lugha nyingine kwa kujua maana ya maneno na hata muundo wa lugha ngeni.

 

 

TOFAUTI KATI YA TAFSIRI NA UKALIMANI

1.   Kimaana

Ø  Tofauti katika uwasilishaji–tofauti uwasilishaji kwa njia ya maandishi lakini ukalimani inawakilishwa kwa njia ya mazungumzo.

Ø  Muda wa maandalizi–tafsiri hupewa muda wa kuandaa kabla ya kuanza kutafsiri lakini ukalimani hauna muda wa kujiandaa.

Ø  Tofauti katika hadhira–ukalimani hadhira yake ni ya papo kwa papo, lakini tafsiri haina hadhira ya papo kwa papo.

Ø  Vifaa ambatani katika utendaji–ukalimani hutumia vifaa kama vile visikizi, vya masikioni,vituturi n.k lakini tafsiri vifaa vyake ni kama vile karatasi na kalaamu, kompyuta n.k.

Ø  Tofauti katika gharama – katika ukalimani gharama hulipwa kwa saa lakini katika tafsiri hunalipwa kwa ukurasa.

Ø  Ukongwe na umri – ukalimani ni mkongwe zaidi kwani ulianza kabla ya kugunduliwa kwa maandhishi lakini tafsiri ilianza baada ya kugunduliwa kwa maandishi.

 

UFANANO KATI YA TAFSIRI NA UKALIMANI

Ø  Zote ni njia au daraja la kuunganisha pande mbili–yaani lugha chanzi na lugha lengwa na matini chanzi na matini lengwa.

Ø  Zote huwa na dhima au lengo la kurahisisha mawaslilano.

Ø  Zote zinahusisha vijenzi katika utendaji wake – kama vile matini chanzi na matini lengwa, lugha chanzi na lugha lengwa.

Ø  Taaluma zote mbili huendeshwa kwa namana mbili – yaani kwa kutumia mashine na kwa kutumia mtu.

Ø  Taaluma zote mbili huhusisha wataalamu na namna mbili – yaani wataalamu wa lugha na wataalamu wa uwanja wa lugha husika yaani mkalimani na mfasiri  watambue watu wanao wafanyia  tafsiri na ukalimani.

 

MATATIZO KATIKA TAFSIRI.

1.      Tofauti za kiisimu– tofauti za maumbo,muundo na maana kati ya lugha ya Kiswahili na lugha za kigeni husababisha upungufu katika kutafsiri.Maumbo ya Kiingereza huruhusu kauli nyingine ili  kuonyessha wingi na umoja wa wahusika.Mfano wa maumbo hayo huweza kutoa tafsiri pana zaidi na wakati mwingine linapo tafsiriwa katika matini lengwa hasa katika lugha ya Kiswahili hulazimika kubadili matini. Mfano

                        Kiingereza                                                      Kiswahili

                        No enterance                                                   usiingie ndani

                        Quite please                                                    usipige kelele

Katika mifano hapo juu ni kwamba tafsiri ya Kiswahili hujibana zaidi kwani ukisema usipige kelele ina maana mimi sio wewe na kwa upande mwingine katika baadhi ya muundo wafasiri huhawilisha ruwaza na kisintaksia za Kiingereza katika Kiswahili na kufanya tafsiri kuwa tenge.

Mfano                         Kiingereza                              Kiswahili

                       Nine thouthands                      tisa elfu

                       Five million                              tano milioni

2.      Tofauti za kiitikadi–katika tafsiri za vitabu na magazeti itikadi na hisia za wafasiri zinaweza kuathiri matokeo ya tafsiri zao.Mfano matini inasifu pombe,unaambiwa utafsiri na wewe hupendi pombe kabisa,hii ni tofauti za kiitikadi kwani kutokana na mfasiri kutopenda pombe anaweza kuibadili matini hiyo badala ya kusifia pombe ikaonesha kuchukia pombe.

      Mfano                   Kiingereza                              Kiswahili

                                   Merchant of venice                  mbepari wa venisi

Katika jina la kitabu hicho nyerere alitafsiri kama mabepari wa venisi badala ya wafanya biashara wa venisi ambayo ndio tafsiri sahihi ya merchant.Mfasiri huyu alisema hivyo kutokana na itikadi alizo nazo kuhusiana na wafanyabiashara kuwa ni mabepari hivyo ni wanyonyaji

3.      Tofauti za mitindo – maranyingi ni vigumu kueleza dhana au taarifa kwa kufuata mtindo unaotokiwa katika uwanja huo hivi inamaana kwamba Kiswahili kama zilivyo lugha nyingine za kiafrika hazijawa na tofauti dhahiri za mitindo. Mfano

                                        Kiingereza                                                  Kiswahili

                                      Lend me your ears                                        naomba mnisikilize

                                      May I have your attention                           

Taarifa ya kingereza inaonekana kuwa pana zaidi kuliko ya kiswahili kwasababu kuna maana nyingi za kuzungumza jambo moja.

4.      Tofauti za mazingira na mila – kwa kawaida mazingira,mila na desturi kati ya watumiaji wa lugha chanzi na lugha lengwa maranyingi hufanya tafsiri kuwa ngumu. Mfano maneno kama “karibu tena” yanapotumiwa na mswahili anapomuaga mgeni wake hayana maana ya moja kwa moja na yale ya Kiingereza “welcome again” bali humaanisha “goodbye”

5.      Toafauti za misemo vitendawili na nahau –maneno haya huendana na watu wa utamadunu fulani unaotofautiana kati ya jamii moja na nyingine.Mfano funga vilago (msemo),enda joshi (nahau),popo mbili zavuka mto (kitendawili), mwenda pole hajikwai (methali) kwa kuwa vitendawili, nahau, misemo na methali huendana na utamaduni wa watu fulani hivyo tafsiri ya maneno kama hayo huweza kukumbwa na matatizo kama vile kutopatikana kwa visawe katika lugha lengwa.

6.      Tofauti za kifasihi –taarifa zilizomo katika fasihi huandaliwa kusanii hivyo huhitaji wasomaji wafanye bidii katika uchambuzi ili wapate maudhui ya fasihi husika kwani bila kusoma kwa makini hawataweza kupata maudhui ya fasihi husika.Mfano katika mashairi ya shaban Robert kuna shairi lenye kichwa “ua” mfasiri anaanza kujiuliza je ua linalozungumziwa hapa ni lipi? Ua kama pambo, mpenzi au muuwaji. Je mfasili  atatoa fasili ipi katika lugha lengwa bila kpoteza maana katika matini chanzi,hili pia ni tatizo  katika tafsiri.

 

UTOSHELEVU KATIKA TAFSIRI

Katika kuangalia utoshelevu katika tafsiri hutazama mambo mbalimbali kama vile;

1.   Kupata msaada wa vitabu mbalimbali. Mfano kamusi.

2.   Kutumia mbinu mbalimbali za tafsiri. Mfano tafsiri ya neno kwa neno mawasiliano nk

3.   Kuzingatia kanuni, sheria na taratibu za matini asli ya au matini chanzi.

4.   Mfasiri azingatie sana utamaduni wa lugha lengwa.

 

MBINU ZA KUTATHMINI/ KUHAKIKI TAFSIRI

Kutathimini au kuhakiki tafsiri  ni kitendo cha kitendo kuisoma kwa makini iliyotafsiriwa na kisha kuitolea hukumu juu ya ubora na udhaifu wake.Kuhakiki au kutathimini  tafsiri hulenga kubaini iwapo tafsiri hiyo ni Tafsiri pana,Tafsiri tenge (mbovu),tafsiri finyu aua Tafsiri sahihi.

 

MBINU MBALIMBALI ZA KUTATHIMINI/ KUHAKIKI MATINI

Katika kuhakiki au kutathimini matini kuna mbinu sita zinazotumiwa,nazo ni;

1.      Ulinganishaji wa matini,Ni mbinu ambayo ni kongwe na ndiyo mbinu ambayo hutumiwa zaidi na wafasiri au wataalamu wengi wanapotathimini au kuhakiki matini mbalimbali.Hapa kinachofanyika ni kwamba matitini iliyotafsiriwa yaani tafsiri huchukuliwa na kulinganishwa na matini chanzi yake ili kuona iwapo vipengele vyote muhimu vya kimuundo na vya kidhima vimezingatiwa katika tafsiri hiyo.Kazi hii ya kutathimini huweza kufanywa na mfasiri mwenyewe au mtu mwingine.

Mfano: Matini chanzi – The chairperson had spoken for almost a hour

              Matini Lengwa-Mwenyekiti alikuwa akihutubia kwa takribuni saa moja

Je kama ni wewe unafanya tathmini ya hizo tungo ungezitathminije kwa kutumia mbinu ya ulinganishaji matini?

2.      Kutumia tafsiri Rejeshi,Ni mchakato wa kutafsiri matini ambayo tayari imeshatafsiriwa katika lugha Fulani (lugha lengwa) na kuirejesha tena katika lugha chanzi kwa lengo la kuitathmini matini hiyo.

Mfano: Kama tafsiri ilifanywa kutoka Kiswahili kwenda kiingereza basi inapofanyiwa tathmini kwa kutumia tafsiri rejeshi basi tafsiri hiyo itatafsiriwa tena kutoka katika lugha ya kiingereza kwenda katika lugha ya Kiswahili

Tafsiri rejeshi inachangamoto kwani inawezekana makosa yapo katika tafsiri ya mtu wa pili anayetathmini na wala si katika tafsiri ya awali iliyofanywa.Hivyo upo uwezekano wa kusema tafsiri iliyofanyika ni mbaya ati tu kwasababu matokeo ya tafsiri rejeshi hayalingani na matini chanzi halisi lakini upo uwezekano wa kuonesha ubora wa tafsiri husika pia.

 

3.      Kupima uasili,Tafsiri bora haipaswi kusomeka kama tafsiri.Hii ina maana kwamba mtu anaposoma tafsiri yako asijue kama ni kazi iliyotafsiriwa badala yake inatakiwa isomeke kama vile imeandikwa katika lugha lengwa hiyohiyo.Hivyo hali ambapo tafsiri husomeka kama vile imeandikwa katika lugha lengwa hiyo hiyo ndio ambayo huitwa uasili.Inashauriwa mfasiri mwenyewe au mtu mwingine anaisoma kazi hiyo,pia hasa inashauriwa apewe mtu mwingine tena bila kuambiwa kwamba kazi hiyo ni tafsiri.

4.      Kupima uelewekaji,Katika mbinu hii kinachoangaliwa ni kueleweka kwa maudhui yanayotolewa katika tafsiri hiyo.Mtu anayepima uelewekaji atajiuliza yeye mwenyewe,je maudhui katika kazi hii yataeleweka kwa wasomaji au kazi hii inazungumzia nini?.Hivyo inashauriwa kwamba mfasiri ampe mtu mwingine ili kuepuka kujipendelea.Ni muhimu kuzingatia kuwa mtu anayepelekewa kazi hiyo inashauriwa awe mfasiri.

5.      Kupima usomekaji,katika mbinu hii ya kupima usomekaji mfasiri au mhakiki atapima tafsiri husika ili kuona iwapo inasikika vizuri masikioni mwa msikilizaji na kama ina mtiririko unaokubalika katika lugha lengwa.Hapa kunakuwa na watu wawili mmoja anasikiliza na mwingine anasoma kwa sauti.

6.      Kupima ulinganifu,Hapa mhakiki anaangalia umakini wa mfasiri katika kutumia kwa namna inayofuata vipengele vyote muhimu vya matini kama vile msamiati,istilahi,maudhui au maneno muhimu yanayobeba maudhui.Maana yake ni kwamba kama neon limejirudia rudia katika tafsiri usibadilishe,mfano;Aim-nia,lengo,madhumuni,kusudi,azma,shabaha n.k.Hivyo kama neon ‘’Aim’’ umelitafsiri kama lengo basi popote litakapojitokeza kwa mara nyingine katika matini basi libaki hivyo hivyo bila kubadili badili.

Powered by Blogger.