MALENGO YA ISIMU JAMII




Malengo ya isimujamii

Isimujamii ina malengo makubwa matatu yafuatayo:-
Kuchunguza tofauti za wazungumzaji wa lugha katika jamii.
Wanaisimujamii hufanya uchunguzi na kufafanua tofauti zilizopo za watumiaji wa lugha katika jamii na kueleza tofauti hizo za wazungumzaji husababishwa na nini. Kuelewa lugha ya jamii kunaendana na kuielewa jamii yenyewe ikiwa ni pamoja na kuyaelewa matabaka na makundi mbalimbali yaliyomo ndani ya jamii hiyo. Jamii imeundwa na matabaka na makundi mbalimbali ya watu. Kuna matabaka ya watawala na watawaliwa, wakulima na wasiowakulima, wafanyakazi wa kuajiriwa na wasiowakuajiriwa, waliosoma na wasiosoma, wafanyabiashara na wasio wafanyabiashara n.k. Pia kuna makundi ya vijana, wazee, wanawake, wanaume, wanafunzi, wanachuo, wanamichezo n.k. Ukichunguza kwa makini utabaini kuwa kila tabaka au kundi la watu katika jamii hutumia lugha inayotambulisha tabaka au kundi hilo. Kuchunguza na kufafanua tofauti za wazungumzaji wa lugha katika jamii kunasaidia watumiaji wa lugha kufahamu watumie lugha ipi katika mazingira rasmi na yasiyo rasmi miongoni mwa wanajamii wenyewe. Lugha rasmi ni ile lugha iliyokubalika na kutangazwa na chombo chenye mamlaka ili lugha hiyo itumike katika shughuli za serikali, bunge, mahakama, elimu nakadhalika. Pia umuhimu mwingine wa kuchunguza tofauti za wazungumzaji wa lugha ni kusaidia wazungumzaji kufahamu namna bora ya kutumia lugha katika mawasiliano ya jamii baina ya wazungumzaji na msikilizaji.
 
Kufanya uchunguzi na kufafanua uhusiano uliopo baina ya lugha na wazungumzaji wake. 
Lengo hili pia linalenga kuifahamu jamii kwa kuchambua lugha ya wazungumzaji wanayoitumia. Kwa kuchambua lugha wanayoitumia wazungumzaji, tunaweza kuitambua jamii inayohusika kama ina dini ua imani ipi, iko maeneo gani ya nchi (pwani, bara, kusini/kaskazini n.k), watu wake wanafanya kazi gani,  wanaume au  wanawake, vijana au wazee, wasomi au wasiowasomi n.k

Kuangalia uhusiano wa lugha moja na lugha nyingine
Mwanaisimujamii anapaswa kuchunguza na kutolea ufafanuzi uhusiano uliopo baina ya lugha moja na lugha nyingine zinazotumika. Katika jamii au taifa kuna lugha zaidi ya moja zinazotumiwa na watu. Nchini Tanzania, kwa mfano, kuna lugha zaidi ya 120 zinazotumiwa na watu mbalimbali. Kidhima lugha hizi zimegawanywa katika makundi matatu. Lugha ya Kiingereza, lugha ya Kiswahili na lugha za kijamii. Ni kazi ya mwanaisimu kufanya uchunguzi na ufafanuzi wa mambo ya msingi yanayohusu uhusiano wa lugha hizi na wazungumzaji wake kwa kuzingatia mahitaji ya jamii ya wakati huo.
 
Isimujamii ya mawandafinyu
Huu ni makabala wa kiisimu unaozingatia lengo la kwanza na la pili la isimujamii katika uchunguzi na uchanganuzi wake. Ni makabala unaochunguza uhusiano wa tofauti za wazungumzaji wa lugha na kubainisha vitambulisho vya usemaji au utamkaji wa wazungumzaji au wazungumzaji ili kuhusisha na kundi la aina ya watu au matabaka ndani ya jamii. Mwanaisimu Labov (1972) katika utafiti wake alioufanya katika jiji la New York, Marekani ameonyesha kuwa, watu wa tabaka la chini hutamka sauti [r] kwa mkwaruzo zaidi katika maneno yenye fonimu /r/ kuliko watu wa matabaka mengine (tabaka la juu). Trughdill (1874), katika uchunguzi alioufanya nchini Uingereza, ameonyesha kuwa mbali na kuwepo kwa lahaja la kijiografia, pia kuna lahaja za kijamii yaani zinazoonyesha hadhi mbalimbali za watumiaji wa lugha ya Kiingereza. Kwa maneno mengine Trudgill anaeleza kwamba unaweza kupata lahaja za wazungumzaji wa hadhi ya juu na lahaja za wazungumzaji wa hadhi ya chini. 
 Isimujamii ya mawandamapana
 
Huu ni mkabala unaozingatia lengo la tatu la isimujamii ambalo linachunguza na kufafanua uhusiano wa lugha moja na lugha nyingine zinazotumika katika jamii. Kwa mujibuwa mkabala huu, mambo yanayozingatiwa ni yale yote yanahohusu utumiaji wa lugha kwa jumla. Kujua lugha zilizopo katika jamii na uhusiano wake kidhima na lugha nyingine ni moja ya mambo ya msingi ya mkabala huu. Kwa mfano mwanaisimujamii katika mkabala huu, hupenda kujua sababu za msingi zinazofanya lugha moja iteuliwe kuwa lugha ya taifa, lugha rasmi au lugha ya kufundis hia katika mfumo wa elimu. Sababu zinazotumika kuteua lugha kuwa na dhima kitaifa mara nyingi huwa hazina budi zitokane na sababu za msingi za kiisimu na kijamii. Kimsingi, hata zile lugha ambazo haziteuliwi kuchukua dhima yoyote kitaifa bado kwa mujibu wa mkabala huu, ni muhimu lugha hizo kufanyiwa uchunguzi ili kuona hali halisi ilivyo, kwa lengo la kutaka kujua hatma ya lugha hizo, hasa kule zinakotumika na pia kutaka kujua maendeleo ya lugha hizo ili kuweza kutoa mapendekezo ya nini kifanyike. Uhusiano huu wa lugha mbalimbali katika jamii hutegemea sana sera ya lugha ya nchi husika. Mkabala huu huhusisha watu wengi kijiografia. Mathalani, mkabala huu unaweza kuhusisha wazungumzaji wa nchi moja, nchi zilizoungana, jumuia ya nchi kadhaa, kanda za nchi mbalimbali na hata huweza kuhusisha wazungumzaji wa bara zima. Kimsingi, mkabala huu wa mawanda mapana ni mkabala ambao kusema ukweli, uchunguzi wake unalenga kutatua matatizo mbambali yahusuyo utumiaji wa lugha kitaifa na kimataifa kwa ujumla.
Powered by Blogger.