TAHAKIKI- CHUNGU TAMU

 


DIWANI : CHUNGU TAMU

MWANDISHI: THEOBALD MVUNGI

WACHAPISHAJI: TPH

MWAKA: 1985

 

UTANGULIZI

Chungu Tamu ni diwani iliyoandikwa na  Theobald Mvungi  miaka ya 1980.Katika diwani hii mwandishi anaimulika jamii na kuichunguza kwa makini.Anakosoa na kutoa mapendekezo ili wananchi waondokane na machungu yanayowaandama na kuonja utamu ambao utawafikisha kwenye kheri.Katika diwani hii mwandishi ameonesha dhahiri jinsi Uchungu na Utamu vinayotangamana katika harakati zote za maisha ya mwanadamu.Kwa ufupi,diwani hii ni kipaza sauti  kinacholia kwa sauti kali kuujulisha ulimwengu juu ya uchungu unaoiandama jamii yetu ya Tanzania .

 

MAUDHUI

DHAMIRA KUU;  UJENZI YA JAMII MPYA

Suala la ujenzi wa jamii mpya limezishughulisha fikra  za wanafasihi wengi hapa   Tanzania .Jamii endelevu ni jamii mpya ambayo haina ubaguzi,matabaka,uongozi mbaya,yenye kufuata misingi ya haki na usawa.Jamii iliyojikomboa katika Nyanja zote yaani kiuchumi, kisiasa,kiutamaduni  na kifikra.Wanafasihi wa Afrika wanaitaka jamii hiyo ijengwe kwa kufuata misingi ya haki na usawa kwa kila mtu. Wanafasihi wa Afrika wameonesha dhahiri kuwa jamii iliyoachwa na wakoloni ilikua zimeoza na hivyo zinahitajika juhudi kubwa ili kuondoa uozo huo.

Nchini Tanzania suala la jamii  endelevu lilianza mara tu baada ya kupata uhuru na kuimarishwa zaidi wakati wa Azaimio la Arusha. Watanzania walitaka wajenge jamii yenye kufuata misingi ya haki na utu,jamii isiyokuwa na matabaka,jamii yenye viongozi waliotakasika, jamii yenye demokrasia ya kweli,jamii isiyo na unyonyaji wa  aina yoyote ile,jamii ambayo hatamu za uongozi zingekuwa mikononi mwa wakulima na wafanyakazi,jamii isiyo na dhuluma ya aina yoyote,n.k.Hadi mwandishi anaandika diwani hii anaonyesha kuwa  jamii bado haijafanikiwa kuifikia lengo la kujenga jamii mpya.

Mwandishi ameonesha vikwazo  mbali mbali vinavyokwamisha ujenzi wa jamii mpya na endelevu hapa nchini na mbinu za kujikwamua kutoka kwenye  vikwazo hivyo.Mwandishi  ametoa mapendekezo ambayo anaamini kuwa endapo jamii itayafuata  itafanikiwa kuijenga jamii  mpya na  endelevu.Mbinu hizo ndizo dhamira ndogo ndogo za diwani hii kama ifuatavyo;

 

1.     KUPINGA DHULUMA

Dhuluma  ni tendo lisilo la haki,tendo la uonevu,ukatili au uovu. Dhuluma hupingana na haki.Suala la dhuluma hurudisha nyuma maendeleo ya jamii na hivyo ni kikwazo kikubwa cha ujenzi wa jamii endelevu.Suala la dhuluma limemshughulisha sana mwandishi wa diwani hii,katika shairi la “Chatu na kuku” Katika ubeti wa mwisho mwandishi anasema;

 

Basi  babu akatua,

Funda akajimezea,

Mimi tama imejishikia,

Huzuni imenisaliti,

Kwa chatu kukosa dhati,

Ndipo nikapanga hizi beti,

Ziwe kama ndiyo  hati

Ukumbusho wa huyu dhulumati.

Katika shiri la “Chatu na Kuku”, mwandishi amelijenga kitaswira kuonesha jinsi wakoloni (chatu) walivyoingia Afrika na kuendeleza dhuluma.Chatu amewakilisha wakoloni na kuku anawakilisha wananchi (Waafrika) walioonyonywa na kudhulumiwa na wakoloni. Mayai ya kuku yanawakilisha mali ghafi waliyodhulumu wakoloni kutoka hapa Afrika.

Katika shairi la“Chanzo ni Wenye Kauli” mwandishi anaonesha jinsi ulanguzi unavyosababisha dhuluma katika jamii.Mwandishi ameonesha kuwa chanzo cha ulanguzi ni upungufu wa bidhaa muhimu,tamaa,pamoja na uzembe toka kwenye vyombo vya dola. Ulanguzi husababisha   rushwa,magendo na hivyo haki haitendeki katika jamii.

Mwandishi anasema;

“Mianzo tukiijua,

Mipango tujipangia,

Kamwe pasiwe na njia,

Ulanguzi kurudia,

Iwe tu twahadithia,

Mithili historia”.

Katika shairi la “Kademokrasia Katoweka”mwandishi anasema;

Ya msiba atayetamka,

Udikteta waja haraka,

Mtemi na walomzunguka,

Wawatia raia mashaka,

Dhuluma yatangazwa fanaka.

Mwandishi anaonesha jinsi wananchi wanavyodhulumiwa demokrasia yao ya kutoa maoni yao hadharani.Demokrasia inapokosekana,dhuluma ya kutawala kwa mabavu huendelezwa.

Katika shairi la “Wengine  Wabaki Taabuni”,mwandishi anajadili juu ya dhuluma wanayoiendesha wakubwa dhidi ya watu wa tabaka la chini.Ameonesha kuwa majambazi wanayo idhini ya kufanya kila jambo kwa wanyonge,kwani hayo majambazi hulindwa na wakubwa.Anaendelea kueleza kuwa dhuluma inayoendeshwa na majambazi hapa nchini ni njama za walinzi (vyombo vya dola).Mwandishi Anasema;

“Majambazi wanayo idhini,

Kufanya lijalo akilini,

Na hawataingia nguvuni,

Ma’na walinzi wamo njamani,

Tabu yaanzia kileleni.”

Mwandishi anaeleza  kuwa tabu inaanzia kileleni maana yake ni tabu au dhuluma inaanzia kwa wakubwa.Hivyo ili tufanikishe suala  la ujenzi wa jamii mpya ni lazima tujitoe mhanga kupambana na kila aina ya dhuluma katika jamii.

 

2. KUFANYA KAZI KWA BIDII

Uzembe na kutowajibika ni kikwazo kikubwa kinachokwamisha maendeleo ya jamii yoyote ile.Jamii yoyote ile yenye viongozi wazembe,viongozi wasiowajibika au wananchi wasiojua wajibu wao daima itabaki nyuma kimaendeleo.Mwandishi anaitaka jamii yetu ijue umuhimu wa kazi na kuwajibika katika suala zima la maendeleo. Mashairi kadhaa katika diwani hii yanasisitiza kuhusu umuhimu wa kufanya kazi ili kuleta maendeleo ya jamii.Katika shairi la “Daktari askari”.Mwandishi anasema;

Saa moja jioni Landova inaingia,

Majeruhi sita na waganga pia,

Majeruhi vibaya wanalalama,

Waganga wao na sisi kazi tukaanza,

Hakuna kuamkiana au sijui nini.la,

Wagonjwa wengi misuli walikatika,

Wengine risasi walichimbiwa ,

Tukawekea damu,

Wa kushonwa,tukawashona,

Wakupasua ,tukapasua.

Katika shairi la “Daktari Askari”,mwandishi anaonesha jinsi waganga wanavyojua umuhimu wa kuwajibika katika kazi yao ya utabibu. Ameonesha kuwa wale waganga waliwahudumia majeruhi kwa bidii wakati wa vita.Hivyo kila mtu anatakiwa kuwajibika kama wale waganga ndipo tutaweza kulisukuma mbele gurudumu letu la ujenzi wa jamii endelevu.

Katika shairi la “Chanzo ni Wenye Kauli” mwandishi anaonesha utekelezaji na uwajibikaji mbovu unavyosababisha rushwa, magendo na ulanguzi katika jamii yetu Katika shairi hili mwandishi ameonesha dhahiri kuwa uzembe toka kwenye vyombo vya dola ndio umechangia uwajibikaji kuwa mbovu.Mwandishi anasema;

“Chombo hiki kuzembea,

Chanzo kilichozidia,

Magendo kuyatetea,

Watu kuwasaidia,

Chombo kilididimia.”

Katika shairi la “Wimbo Wake Hotubani” wandishi anaonesha utekelezaji  mbaya wa maazimio unavyochangia kuzorota kwa maendeleo ya jamii yetu.Katika shairi hili,mwandishi ameonesha kuwa viongozi wetu wametuna ofisini na shambani hawaingii, wanatumia madaraka vibaya,maagizo ni midomoni bila utekelezaji, kila siku-mchana kutwa wanakunywa na kulewa, n.k.Utekeleaji wao uko kwenye hotuba,Mwandishi anasema;

Cheo kiko mkononi,

Agizo li mdomoni,

Mchana kutwa ndotoni,

Wimbo wake hotubani,

Raia kazi fanyeni.”

Katika shiri la “Wengine Wabaki Taabuni”,mwandishi anaonesha jinsi uzembe kazini,kutowajibika ipasavyo,usaliti pamoja na rushwa unavyorudisha nyuma utekelezaji mzuri wa maazimio tunayojiwekea.Mwandishi anaitaka  jamii ifahamu na kutambua umuhimu wa kazi na wajibu wa kila mmoja katika jamii ndipo tutaweza kufanikisha kuijenga jamii mpya.

 

3.     UONGOZI  MBAYA

Suala la uongozi mbaya limekuwa tatizo sugu kwa nchi nyingi  za Afrika.Waandishi wengi wameonesha jinsi ambavyo viongozi wengi walioshika madaraka baada ya mkoloni kuondoka walivyoteka nyara uhuru uliopatikana,kwa hiyo mabadiliko yakawa rangi ya ngozi tu,kwani wananchi wengi waliendelea kuteseka katika umasikini wao.Katika shairi la “Tishio la Binadamu”mwandishi anasema;

Mashindano ya silaha,yamekuwa ni mchezo,

Wakubwa waona raha,kwa silaha waundazo,

Mabomu yaso na siha,ndiyo yawapa uwezo,

Urusi na Marikani,dunia mwaipa  adha.

Mwandishi anakemea juu ya uongozi unaotumia mabavu, Mfano mzuri mwandishi anakemea nchi za Urusi na Marekani ambazo ni wanachama wenye kura ya VETO kwenye umoja wa Mataifa zinavyotumia mabavu kuzikandamiza nchi zisizo na nguvu kisilaha. Mwandish anasema;-

Kuyasujudu mabavu, mwadai tusilotaka,

Maoni yetu chakavu, sawa nguo ya miaka,

Ni pengi penye makovu, nchi zilivyopasuka,

Mabomu yateketeza,waundaji mwafurahi!”

Shairi la “Chini ya Mti Mkavu” mwandishi analaani uongozi unaoendeleza dhuluma katika jamii.Anakemea juu ya uongozi mbaya usiojali maslahi ya wengi,uongozi usiopiga vita umaskini hapa nchini, n.k.

Katika shairi la “Wanajua Kuvumilia”,mwandishi analaani ahadi za uongo zinazotolewa na viongozi wetu.Ameonesha kuwa viongozi wetu hawasemi ukweli bali uongo ndio umetawala midomo yao.Katika shairi hili mwandishi analaani vibaya viongozi ambao hawafiki vijijini kwa wananchi waliowachagua  ili kujionea hali halisi ya maisha wanayoshi.Mwandishi anasema:-

“Afadhali kuimba ukweli,

Wimbo mchomo mkali,

Wimbo, unalilia hali,

Ya vijiji vilivyo mbali,

Kwa wale wasio kauli.”

Katika shairi la “Udongoni” mwandishi anawakumbusha viongozi wajibu wao katika jamii.Mwandishi anasema:-

“Lanikumbusha wajibu,

Kujenga si kuharibu,

Naahidi kujaribu,

Kulinda tulichojenga.”

Mwandishi anaona kuwa Uongozi bora ni msingi mkubwa katika ujenzi wa jamii mpya hivyo anaiasa jamii kupiga vita  Uongozi mbaya  ili kujenga jamii endelevu hapa nchini.

4.     KUWEPO NA DEMOKRASIA YA KWELI

Demokrasia ni mfumo wa kuendesha serikali iliyochaguliwa na watu kwa manufaa ya watu wenyewe.Demokrasia inahitajika sehemu yoyote ile ili kuwaruhusu wananchi kutoa maoni yao kwa uhuru bila wasi wasi au kikwazo chochote.Katika shairi la“Mjanja yu Mashakani” mwandishi anasema;

Kumezuka mkatao,miaka ya themanini,

Watu wafanya jutio,hawasemi chinichini,

Hawasemi tena ndio,haitoki midomoni,

Wamevumilia sana,mwisho wa uvumilivu.

Mwandishi anajadili  kuhusu mfumo wa demokrasia ambao umejitokeza miaka ya 1980 kote ulimwenguni.Mfumo huu ni ule wa kupinga sera ya chama kimoja na kuingia katika mfumo wa vyama vingi (mageuzi).Katika shairi hili mwandishi anaonesha kuwa mfumo wa vyama vingi umewaamsha wananchi wengi kutoka usingizini na kuanza kutetea haki zao.Hata hivyo,mwandishi anaonesha kuwa wale viongozi waliojilimbikizia madaraka na vyeo mbali mbali wamehofia sana mfumo huu na hivyo hufanya kila mbinu ili kuudidimiza.Viongozi wanaong’ang’ania madaraka ndio wanaohofia mfumo huu.

Shairi la “Kademokrasi Kametoweka”linapinga uongozi mbaya barani Afrika.Mwandishi ameonesha kuwa demokrasia inapopokonywa na viongozi wachache,udikteta huota mizizi na kuung’oa huchukua muda mrefu.Hali hii inasababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe katika baadhi ya nchi barani Afrika.Mfano wa nchi hizo ni Jamuhuri ya Watu wa Kongo,Uganda,Burundi,Sierra Leone,n.k.Utawala wa nguvu hurudisha nyuma maendeleo ya bara la Afrika na nchi nyingine za ulimwengu wa tatu ambako hakuna demokrasia ya kweli.Mwandishi anasema:-

Barani mabavu yatumika,

Dikteta asijeanguka,

Na majungu pia ayapika,

Udikteta pasi shufaka,

Nasimulia ya Afrika

Mwandishi anaonesha kuwa mabavu yanatumika ili kumlinda dikteta asije akaangushwa kwa kufuata mfumo wa demokrasia ya kweli.Madikteta hao hutumia vyombo vya dola kama vile polisi, jeshi,magereza na mahakama ili kutetea maslahi yao.Kwa ujumla anatoa pendekezo kuwa, ili tuweze  kujenga jamii mpya hatuna budi kujenga na kudumisha demokrasia ya kweli katika harakati zetu za maisha.

 

5. MATABAKA

Matabaka ni hali ya watu kuishi kufuatana na madaraka walionayoya,uchumi na siasa n.k.Msanii ametumia vielelezo halisi kufikisha ujumbe kwa jamii.Katika shairi la “Wimbo wake Hotubani” mwandishi anasema;

Magavana majimboni,

Wasambazao nchini,

Wapewa kubwa idhini,

Na watune ofisini,

Wasoingia shambani,

Kwa sifa madarakani.

Mwandishi anadhihirisha matabaka yaliyopo nchini mwetu. Magavana wanawakilisha tabaka la juu (viongozi) na punda na ngamia wamechorwa kitaswira kuwakilisha wananchi wanyonge wanaoteswa na kunyanyasika.

Katika shairi la “Wengi Wabaki Taabuni  mwandishi anasema;

Mesikia  kilio gizani,

Jamaa apita njiani,

Ghafla akakabwa kooni,

Kapigwa kabari ya kihuni,

Yaitwa demokrasi guni.

Mwandishi anaonesha kuwa,kuna matabaka ya aina mbili katika jamii yaani tabaka la wachache wanaofurahia maisha na tabaka la wengi wanaoteseka taabuni.

Kwa ujumla mwandishi ameonesha kuwa mgawanyiko wa watu katika matabaka huleta utengano katika jamii.Ili tuweze kufaulu kuijenga jamii mpya (endelevu) hatuna budi kupiga vita matabaka yaliyoshamiri katika jamii.Lengo liwe kuijenga jamii yenye kufuata misingi ya haki na usawa.

6.KUEPUKA VITA (UHASAMA)

Vita husababisha uhasama katika jamii.Huleta ugomvi na kutokuelewana miongoni mwa watu.Vita hurudisha nyuma maendeleo ya jamii.Vita huleta athari mbaya katika jamii.Mfano vifo,umasikini,ugumu wa maisha.Katika shairi la “Tishio la Binadamu”,mwandishi  anasema:-

Mashindano ya silaha,yamekuwa ni mchezo,

Wakubwa wanaona raha,kwa silaha waziundazo,

Mabomu yaso na silaha,ndiyo yanawapa uwezo,

Urusi na Marekani, dunia mwaipa adha”

Mwandishi anaitahadharisha dunia kuwa vita kuu vinanukia.Hii ni kutokana na uhasama uliopo kati ya nchi na nchi pamoja na utengenezaji wa silaha kali kutoka Urusi na Marekani.Kutokana na hali hii dunia nzima sasa iko mashakani juu ya vita.Mwandishi anaendelea kueleza kuwa mashindano ya silaha yamekuwa ni mchezo na nchi kubwa zinaona fahari kuzitengeneza.Hivyo mwandishi anaitaka jamii  itakayojengwa iepukane daima na suala la vita.

 

7.SUALA LA MAPENZI

Mwandishi amejadili aina mbali mbali za mapenzi katika diwani hii kama ifuatavyo;

Mosi,mapenzi  ya mtu na nchi yake.Haya mapenzi tunayaona katika shairi la “Daktari Askari” ambapo tunona kuwa,wakati wa vita kati ya Uganda na Tanzania raia,wanajeshi,manesi,n.k.walijitolea kwa moyo wa dhati kwenda kupigana ili kuikomboa nchi yao.Mapenzi haya ni ya kweli na dhati.Mapenzi ya Iddi Amini Dada kwa nchi yake hayakuwa ya dhati ndiyo maana alitumia mabavu kuiongoza nchi yake.

Pili,Mapenzi mengine kati ya mtu na nchi yake yanapatikana katika shairi la“Ngulu Wapaona”Katika shairi hili msanii anaonesha umuhimu wa kuwa na  mapenzi na kwenu  (nchi yako) hata kama ni porini. Msaanii anamtaka kila mtu kuthamini kwao hata kama kuna karaha.Anaonesha kuwa kwenu ni kwenu  na ukuthamini na kukuheshimu kwa raha na Baraka.

Tatu,mapenzi kati ya mwanamme na mwanamke.Mapenzi haya mwandishi ameyagawa ktika makundi makuu  mawili ya mapenzi ya dhati na yale ya udanganyifu.Mashairi yanayoongelea mapenzi ya dhati ni yale ya “Daktari Askari”,Thomas na Doto”,“Manzese Mpaka Ostabei”pamoja na lile la“Takukumbuka Daima.”

Mashairi yanayoongelea mapenzi ya udanganyifu ni kama vile “Usiwe Mwonja Asali”, “Fikra za Waungwana”.

Mapenzi ya dhati ni  ya kuheshimiana,Mapenzi yasiojali hali au kipato cha mtu. Mapenzi ya uaminifu. Mapenzi kati ya Daktari Adam na Eva katika shairi la “DaktariAskari” yalikuwa ya dhati, bila kujali kwao au utaifa.Hali kadhalika mapenzi kati ya Thomas na Doto yalikua ya dhati bila kujali rangi au taifa.Na mapenzi kati ya Mashaka na Dorothy yalikuwa ya dhati bila kujali pesa au utajiri. Mapenzi ya dhati husababisha uvumilivu katika maisha.Mapenzi ya dhati huzaa matunda mema katika ndoa,yaani hujenga ndoa za uaminifu.Hivyo mapenzi ya dhati huzaa ndoa za kudumu,ndoa zisizojali rangi,utajiri,utaifa au hali ya mtu.Ndoa za uaminifu zilizotokana na mapenzi ya dhati Katika diwani hii ni zile kati ya daktari Adam na Eva, pamoja na ile ya Mashaka na Dorothy.

Mapenzi ya udanganyifu nayo pia huzaa ndoa za udanganyifu na mara nyingi ndoa hizo huwa hazidumu.Katika shairi la “Usiwe Mwonja Asali”,msanii anaonesha jinsi mapenzi ya udanganyifu yanavyosababisha uchumba wa udanganyifu.Msanii anaishauri jamii kuwa ukiwa na mchumba msiwe na tabia za kujamiiana ovyo,bali mpaka mtakapooana.

Katika shairi la “Fikra za Waungwana” mwandishi anadhihirisha wazi jinsi mapenzi ya udanganyifu yanavyosababisha ndoa za ulaghai. Mwandishi anasema:-

Mume wangu nakupenda, Joseph amenikuna,

Nimekula naye tunda, ninampenda sana,

Na usifanye inda, mimi ni wako kimwana,

Nitaishi kwa mpango, kwako na kwake Joseph.”

Kwa ujumla  mwandishi anaitaka jamii yetu idumishe mapenzi na ndoa za dhati.

 

5.     NAFASI YA MWANAMKE PAMOJA NA UHURU WAKE KATIKA JAMII.

Mwandishi  amemchora mwanamke katika nafasi mbali mbali kama ifuatavyo;

Mosi,amemchora kama mwanamapinduzi na jasiri.Katika shairi la “Daktari Askari”mwanamke ameoneshwa akifanya kazi za kimapinduzi sawa na zile za mwanamme.Mwanamke anapigana vita ili aikomboe nchi yake.

Pili,mwanamke amechorwa kama mtu mwenye mapenzi dhati katika jamii.Katika shairi la “Manzese Mpaka Ostabei” linamwonesha Dorothy akiwa na mapenzi ya dhati kwa Mashaka . Hali kadhalika katika shairi la “Daktari Askari linamwonesha Eva akionesha mapenzi ya dhati kwa Daktari Adam.

Tatu,mwanamke amechorwa kama kiumbe laghai, asiye mwaminifu hususani katika suala a mapenzi na ndoa. Haya yote tuayoyaona katika shairi la “Fikra za Waungwana”.

Mwisho,mwanamke amechorwa kama mzazi na mlezi katika jamii.Katika shairi la “Manzese mpaka Ostabei”,mwanamke amechorwa kama mzazi na mlezi na hii nafasi inawakilishwa na Dorothy ambaye alimzaa mtoto na kumlea baada ya kuolewa na Mashaka.

Kuhusu uhuru wa mwanamke,msanii ameleta mjadala juu ya uhuru wa mwanamke,uhuru wa kuolewa na wanaume wawili kama afanyavyo mwanaume kwa kuoa wake wawili au zaidi.

Katika shairi la “Fikra za Waungwana” mwandishi anasema;

Mume wangu nakupenda, Josefu amenikuna

Nimekula naye tunda, nampendelea sana,

Ila usifanye inda, mimi ni wako kimwana,

Nitaishi kwa mpango, kwako na kwake Josefu.”

 

Msanii anajadili dhamira hii kupitia  mhusika Anna.Katika shairi hili, Anna ana mume wake (Nania) lakini kwa upande mwingine anampenda Josefu ambaye ni  mume wake wa pili. Anna haoni sababu ya kutokuwa na wanaume wawili.

Msanii anaonesha kuwa uhuru anaoutaka Anna ni wa kuishi au kuwa na wanaume wawili na huo ndio msimamo wa Anna.

Hata baada ya kesi yake kupelekwa mahakamani,Anna alibaki na msimamo huo huo.Hali kadhalika majaji walishindwa kutoa hukumu,kwani hakuna sheria inayozuia mwanamke kuwa na wanaume wengi kama walivyo wanaume ambao huwa na wanawake wengi.

Lakini swali la kujiuliza ni kuwa, je  mwanamke ana haki ya kuwa na wanaume wawili katika jamii?,Hakuna sheria inayomzuia mwanamke kuwa na wanaume wawili lakini mila na desturi ndiyo zinazomzuia mwanamke kuwa na waume wawili. Hivyo ni kutokana na kasoro hizo ndiyo maana anapinga kasoro hizo,kudai uhuru wake wa kuolewa na wanaume wawili kwa wakati mmoja kama mwanaume anavyooa wake wawili au zaidi kwa wakati mmoja. Hivyo anaishauri jamii kuona inaweka wazi sharia zinazohusiana na suala hili.Majaji walishindwa kuhukumu kesi ya Nania- hii ni kwasababu hakuna kifungu cha sheria kinachomzuia mwanamke kuolewa na wanaume wawili kwa wakati mmoja.

UJUMBE

v Ni lazima tujitoe mhanga ili kutetea wanyonge

v Dhuluma,unyonyaji,kutowajibika pamoja na uongozi mbaya ni baadhi ya vikwazo vinavyokwamisha ujenzi wa jamii mpya.

v Mashindano ya kutengeneza silaha kwa mataifa makubwa huhatarisha amani duniani.

v Demokrasia ya kweli ndiyo njia pekee ya kuendeleza mfumo wa mageuzi hapa nchini na katika nchi nyingine za ulimwengu wa tatu.

v Mgawanyiko wa watu katika matabaka husababisha kukosekana kwa umoja na mshikamano katika jamii.

v Mapenzi ya dhati yanahitajika katika jamii na ni lazima yadumishwe. Mapenzi ya ulaghai yapigwe vita kwa hali zote.

v Suala la mapenzi na ndoa waachiwe wawili wanaopendana na si maamuzi ya wazazi.

FALSAFA

Ø Mwandishi anaamini itikadi itakavyowatetea wanyonge, yenye kuleta haki na usawa kwa kila mtu. Analaani wizi, dhuluma,udikteta,unyonyaji na kila aina ya uovu.Vile vile anatetea uhuru katika mapenzi na ndoa.

MSIMAMO

Ø Mwandishi wa diwani hii ana msimamo wa kimapinduzi kwani ameonesha matatizo mbali mbali yanayozikumba jamii zetu na mbinu za kuondokana na matatizo hayo. Miongoni mwa matatizo hayo ni uongozi mbaya, ulanguzi, dhuluma,rushwa,n.k pamoja na namna ya kuyatatua matatizo hayo.

 

FANI

1. MTINDO

Mwandishi wa diwani ya UCHUNGU TAMU ametumia mitindo ifuatayo:-

(a) Mtindo wa masimulizi

 Ni mtindo ambao mwandishi au mshairi anamuumba mhusika katika shairi akisimulia hadithi ili kufikisha maudhui yaliyokusudiwa kwa jamii.Mashairi yaliyotumia mtindo huu katika diwani hii “Chatu na Kuku”, “Dakitari Askari”, “Thomas na Doto” na “Manzese Mpaka Ostabei” .Mashairi haya unapoyasoma utadhani unasoma hadithi kuliko tungo za kishairi.

Katika shairi la “Chatu na Kuku” , Babu anaonekana akimsimulia Mjukuu wake hadithi baina ya marafiki wawili, ambao ni Chatu na Kuku.Mwandishi anaonesha masimulizi ya Babu kama ifuatavyo:-

“… … hapo zamani sana,

Katika enzi zao za ujana,

Asemacho alikiona.

 

Ati chatu aliwahi kuwa rafiki ya kuku,

Mie nikaguna kwa dukuduku,

Labda chatu wa mbali si wa huku,

Si chatu yule mwenye mabaku.

 

… … Naam hadithi ikasonga,

Chatu na kuku wakala amini,

 “Tushirikiane tusifanyiane maovu, 

Lakini kila mmoja akae kwake!”

 

Katika shairi la “Manzese Mpaka Ostabei” ,kuna mianzo maalumu ya kifomula ya hadithi za fasihi simulizi kama ifuatavyo:-

“Hadithi njoo,

Manzese uende,

Kariakoo upite, 

Mwisho  wako Ostabei …

 

… … Na hadithi ikaawa,

Tamu na isoisha hamu”.

 

(b)  Mtindo wa tenzi

Ni mtindo ambao mshororo (mstari) mmoja wa shairi huundwa na kipande kimoja tu. Aghalabu,mshororo mmoja na ubeti wa shairi la mtindo wa tenzi huwa na mizani (silabi) kati ya 6 hadi 11 tu.

Tenzi huwa na ulinganifu wa silabi za mwisho kwa kila mshororo au mtari wa ubeti.Mashairi yaliyotumia mtindo wa tenzi katika diwani hii ni “chanzo ni Wenye Kauli”, “Wimbo Wake Hotubani”,“Kademokrasi Katoweka” . “Wengine Wabaki Taabuni” , “Shairi la Udongoni”. 

“Usiwe Mwonja Asali  na “Takumbuka Daima” .Kwa mfano, katika shairi la “Takukumbuka Daima” , mshairi anasema;

              “Takukumbuka daima, 

Kazi ikija hatima, 

Nitarudi himahima, 

Nikuone wa heshima.

 

Wajua moyo wangu, 

Kwako hauna ukungu, 

Kukuaga ni uchungu, 

Kama kuikosa mbingu”.

 

( c )  Mtindo wa kidato

Ni mtindo ambao mshairi hutumia baadhi ya mistari iliyofupishwa maneno au silabi tofauti na mistari mingine ambayo huwa na silabi au maneno mengi.Mbinu ya kidato hutumiwa na mshairi kwa lengo maalumu hususani katika kufikisha ujumbe wake kwa jamii iliyokusudiwa.Mashairi yaliyotumia mtindo huu katika diwani hii ni “Chungu Tamu” , “Chatu na Kuku” ,“Dakitari Askari” , “Wanajua Kuvumilia”,”Ngulu Wapaona” , “Chungu na Tamu ,“Thomas na Doto” na “Manzese Mpaka Ostabei” . Katika shairi la “Chungu Tamu ,Mshairi anasema:

“Mekumbusha pia matumaini,          

Ya wale walio chini, 

Wavuja jasho la ziada, 

Na kunyimwa faida.

 

Matumaini yao, kesho kuwa nafuu,

Sikwamba wende juu, 

La, ila angalau wasile makombo,

Ya mfumo ulo  kombo”

 

( d) Mtindo wa majibizano

Ni mbinu inayotumiwa na wasanii kuumba wahusika wa kazi za kifasihi wanaozungumza kwa kupokezana.Mashairi yaliyotumia mtindo wa majibizano katika diwani hii ni “Chatu na Kuku”  na “Dakitari Askari.  Katika shairi la “Chatu na Kuku” kuna majibizano kati ya Babu na Mjukuu kama ifuatavyo:-

“Babu akageuza kiazi kisiungulie, 

Akasema tulia “”mzee”. 

Ati mie “mzee! 

Vuli kumi na tano zilikuwa bado kwangu

 

Niliuliza: “Kuku alizikwaje?” 

Ati kuku walichimba kwa mikono na kucha, 

Na chatu alitumia meno yake,

haya!

 

Nilimuuliza babu tena, 

 “Hadithi ya kweli?” 

Babu akameza funda la kiazi na maji”

 

Katika shairi la “Dakitari Askari”  kuna majibizano kati ya Evadora Wesana na Adam Kiende, pia Luteni Bwege na Kapteni Adam Kiende, kama ifuatavyo:-

“Kweli wewe nasoma Makerere, 

Na hii Kapteni yetu, 

Yeye napenda wewe,  

Cheo gani iko ndani ya jeshi ya adui?” 

“Kapteni”, nilijbu.

 

Luteni akauliza,

“Doctors  where college?  

Safari hii nikaogopa makofi,

 “Makerere”. Jibu fupi.

( e) Mtindo wa kuhoji

Ni mtindo unaotumiwa na washairi wa kuuliza maswali ambayo ama majibu yake yako wazi au hayako wazi.Mashairi yaliyotumia mtindo wa kuhoji katika diwani hii ni pamoja na “Thomas na Doto”, “Chatu na Kuku”, “Dakitari Askari”  na “Manzese Mpaka Ostabei”.

 

Katika shairi la “Thomas na Doto”, mtindo wa kuhoji (kuuliza maswali) umetumika ka ifuatavyo:-

 

 

 

 

“Kwahiyo mama alia,  

Mzee afoka kwa kukemea, 

Kwa nini mweusi wachukua? 

Weupe hujajionea? 

Wakasema wakasema, 

Thomas kimya kainama”.

 

Katika shairi la “Dakitari Askari”, mtindo wa kuhoji (kuuliza maswali) umetumika katika beti hizi;

“Kweli wewe nasoma Makerere,  

Na hii Kapteni yetu, 

Yeye napenda wewe, 

Cheo gani iko ndani ya jeshi ya adui?  

“Kapteni”, Jibu fupi

 

Luteni akauliza.  

“Doctors where college?  

Safari hii nikaogopa makofi, 

“Makerere” Jibu fupi.

 

( f )  Mtindo wa msisitizo au takriri

Ni mtindo ambao neno moja linatokea mwanzoni na linarudiwa katika mishororo au mistari ya ubeti wa shairi.Shairi lililotumia mtido wa msisitizo au takriri katika diwani hii ni “Manzese Mpaka Ostabei” .Mshairi anasema:

“Sijui,

Je hiyo harufu ya dhuluma, 

Je vishindo vya majambazi, 

Je, je, je … … je, nyingi, 

Jiji salama, 

Watu hadaa,

Yayumkinika, labda. 

 

 

 

Hadithi yawanogea,

Naona mwajiramba na kutumbua macho,

Kigori anawababaisha,

Kigori mke wa Kitwana,  

Wote weusi wa mkaa, 

Jirani zao waliwatania,  … …

 

Ndiyio,  

Dorothy alikuwa binti Shibe, 

Dorothy rafiki yake Mashaka, 

Mashaka bini njaa, 

Njaa ya kila kitu, pamoja nay a kupendwa … …”

( g ) Mtindo wa kikufu au pindu

Ni mtindo ambao neno au sehemu ya neno ya mshororo inayomalizia huanzia katika mshororo (mstari) wa ubeti unaofuata.Shairi lililotumia mtindo wa kikufu au pindu katika diwani hii ni“Manzese Mpaka Ostabei” . Mshairi anasema:

Ndiyo, 

Dorothy alikuwa binti Shibe,  

Dorothy rafiki yake Mashaka,  

Mashaka bini njaa,  

Njaa ya kila kitu, pamoja na ya kupendwa…  …”

 

( h) Mtindo wa nafsi

 Ni mtindo ambao mshairi anaaweza kutumia nafsi umoja, nafasi wingi au nafasi kundi kwa lengo la kufikisha ujumba ua maudhui Fulani kwa jamii.  Kuna nafasi za aina tatu (3), yaani nafasi ya kwanza (umoja na wingi), nafasi ya pili (umoja na wingi) na nafasi ya tatu (umoja na wingi). Mwandishi wa diwani hii ametumia mtindo wa nafasi kama ifuatavyo:

(i)  Matumizi ya nafsi umja (nafsi ya pili umoja)

Katika mtindo huu mshairi huzungumzia jambo au suala linalomhusu mtu mmoja pekee.  Hujumuisha sifa,mawaidha na maonyo.Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya pili umoja katika diwani hii ni “Usiwe Mwonja Asali” na “Ngulu Wapaona” .  Kwa mfano katika shairi la “Usiwe Mwonja Asali” (uk. 36-37), mshairi anasema:

“Basi umwitaye mwali,  

Yafaa umwache mbali, 

Umwambie kwa kauli,  

Ukishamjua hali, 

Sahau kamba ni mwali, 

Usiwe mwonja asali”.

 

(ii)  Matumizi ya nafsi wingi (nafsi ya kwanza wingi)

Katika mtindo huu mshairi huzungumzia jambo au suala linalohusu kundi fulani la watu,akiwemo na yeye mwenyewe.Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya kwanza wingi katika diwani hii ni “Chini ya mti Mkavu” , na “Chanzo ni Wenye Kauli”.  Kwa mfano katika shairi la “Chini ya Mti Mkavu”, mshairi anasema: 

“Tulio wengi twajua, hawa wanatudhulumu,  

Chakula kutumezea, kwa niaba ya kaumu,  

Kwa maringo watembea, matumbo yenye karamu, 

Lakini yajulikana, kujua tu haitoshi”      

(iii)  Matumizi ya nafsi kikundi (nafsi yatatu wingi)

Katika mtindo huu mshairi huonekana ama akitoa hotuba, akisimulia hadith au akizungumza na kundi fulani la watu kuhusu suala au jabo  muhimu.Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya tatu wingi katika diwani hii ni “Mjanja Yu Mashakani”, “Wanajua Kuvumilia”, “Chatu na Kuku” , “Chungu Tamu”, “Dakitari Askari”. “Thomas na Doto” (uk. 37-42) na “Manzese Mpaka Ostabei”.  Kwa mfano katika shairi la “Mjanja Yu Mashakani”, mshairi anasema:

“Na wengi wametambua, ukweli ulifichika,

Wongo wameugundua, hasira zimewawaka,

Hasira isopungua, kwa ishirini miaka, 

Mana ililimbikizwa na kusakamwa moyoni”

 

( j)  Mtindo wa kuandika jibu katika mashairi

Mwandishi ameonesha upekee wake katika kuandika diwani kwa kutunga shairi lenye jibu.Mtindo wa kuandika jibu katika mashairi umejitokeza katika shairi la “Takukumbuka

daima” .Mshairi anasema:

“Moyoni nitatetema, 

Kukuaga wangu mwema, 

Ulaya mmenituma,  

Nashukuru kwa heshima.

 

Takukumbuka daima, 

Kazi ikija hatima, 

Nitarudi himahima, 

Nikuone wa heshima”

 

 

Jibu:

“Safari na iwe njema,  

Nakutakia uzima,  

Nitauguza mtima,  

Takukumbuka daima”.

 

2.  MUUNDO

Mwandishi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia miundo tofautitofauti kwa kuzingatia vigezo mbalimbali kama ifuatavyo:-

Ø Kigezo cha idadi ya mishororo:

Kwa kuzingatia kigezo cha idadi ya mishororo kwa kila ubeti,mshairi ametumia miundo ifuatayo:-

(a) Muundo wa tarbia

 Ni muundo ambao kila ubeti unaundwa na mistari minne.Mashairi yaliyotumia muundo wa tarbia katika diwani hii ni “Chungu Tamu” , “Tishio la Binadamu” , “Chatu na Kuku” .  “Chini ya Mti Mkavu” .  “Mjanja Yu Mashakani” ,  “Wanajua Kuvumilia” , “Radi ya Kiangazi” ,  “Shairi la Udongoni” , “Fikira za Waungwana” , “Mfereji Maringo”  na “Takukumbuka Daima”.Kwa mfano, katika shairi la “Chini ya Mti Mkavu”, mshairi anasema:

“Tulio wengi twajua, hawa wanatudhulumu,  

Chakula kutumezea, kwa niaba ya kaumu,   

Kwa maringo watembea, matumbo yenye karamu, 

Lakini yajulikana kujua tu haitoshi”.

(b)  Muundo wa takhmisa:

Ni muundo ambao kila ubeti unaundwa  kwa mistari mitano.Mashairi yaliyotumia muundo wa takhmisa katika diwani hii ni “Kademokrasi Katoweka”  na “Wengine Wabaki Taabuni” .  Kwa mfano, katika shairi la “Kademokrasi Katoweka”  (uk.30-31), mshairi anasema

“Barani mabavu yatumika, 

Dikiteta asije anguka,  

Na majungu pia ayapika, 

Udikiteta pasi shufaka, 

Nasimulia ya Afrika”.

 

(c)  Muundo wa sabilia

i muundo unaohusu mashairi yanayoundwa kwa mistari sita na kuendelea katika kila ubeti.  Mashairi yaliyotumia muundo wa sabilia katika diwani hii ni “Dakitari Askari”,“Chanzo ni Wenye Kauli” ,

 “Wimbo Wake Hotubani” , “Ngulu Wapaona” ,  “Chungu na Tamu”, “Usiwe Mwonja Asali” ,  “Thomas na Doto” , “Manzese Mpaka Ostabei”  na “Wasia” .  Kwa mfano katika shairi la “Usiwe Mwonja Asali” , mshairi anasema:

“Basi umwitaye mwali,  

Yafaa umwache mbali,  

Umwambie kwa kauli,  

Ukishamjua hali, 

Sahau kamba ni mwali, 

Usiwe mwonja asali”.

Ø Kigezo cha idadi ya vipande:

Kwa kuzingatia idadi ya vipande kwa kila mshororo katika ubeti wa shairi,

Mwandishi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia miundo ifuatayo:

(a)  Muundo wa kipande kimoja (ukwapi)

Ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na kipande kimoja tu.  Mifano ya mashairi ya muundo wa kipande kimoja katika diwani hii ni “Chungu Tamu” (uk. 1) “Chatu na Kuku” (uk.2-10),  “Wanajua Kuvumilia” (27), “Shairi la Udongoni” (uk.35-36), “Takukumbuka Daima” (57),  “Wasia”  (uk. 58),  “Thomas na Doto” (uk. 37-42),  “Usiwe Mwonja Asali” (uk. 36-37), “Chungu na Tamu” (uk. 34-35), “Ngulu Wapaona”  (uk.33-34),  “Wimbo Wake Hotubani” (uk. 29-30) na “Chanzo ni Wenye Kauli” (uk. 28).  Kwa mfano, katika shairi la “Takukumbuka Daima” (uk. 57), mshairi anasema: 

“Moyoni nitatetema, 

Kukuaga mwangu mwema, 

Ulaya mmenituma, 

Nashukuru kwa heshima”

 

(b)  Muundo wa vipande viwili (ukwapi na utao):

Huu ni muundo ambao kw akila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na vipande viwili, yaani kipande cha kwanza (ukwapi) na kipande cha pili (utao).  Mifano ya mistari ya muundo wa vipande viwili katika diwani hii ni “Tishio la Binadamu” (uk.1-2), “Chini ya mti Mkavu” (uk.10), “Mjanja Yu Mashakani”  (uk.26-27),  “Radi ya Kiangazi” (uk.32-33),  “Fikira za Waungwana”  (uk. 54-56)mshairi anasema:

“Ana unanichukia, si ajabu hunitaki,  

Sijui nilokosea, kwako mimi sipendeki, 

Josefu nd’o wamjua, wampenda kwa malaki,  

Ana wangu wa nyumbani, sema nakusikiliza”.

Ø Kigezo cha aina ya vituo:

Kwa kuzingatia kigezo cha aina ya vituo, mwandishi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia muundo wa kituo kimalizio.  Kitu kimalizio ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao haujirudirudii kwa kila ubeti.  Hii ina maana kuwa kwa kila ubeti wa shairi kunakuwa na mstari wa mwisho (kituo) wa tofauti na usiofanana na beti nyingine.  Mashairi yote ya diwani hii yametumia muundo wa kituo kimalizio.

Katika shairi la “Chini ya Mti Mkavu” (uk.10), mshairi anasema. 

“Yametusibu jamani, wote tulio nchini, 

Mioyo yaenda chini, kicheko cha maskini, 

Twajilamba midomoni, hatunacho cha tumboni, 

Utii umetuponza, laiti tungelijua.

 

Tulio wengi twajua, hawa wanotudhulumu, 

Chakula kutumezea, kwa niaba ya kaunu, 

Kwa maringo watembea, matumbo yenye karamu,  

Lakini yajulikana, kujua tu haitoshi”,

 

Katika Shairi la “Chungu Tamu ”  (uk. 1), mshairi anasema: 

“Mekumbusha pia matumaini, 

Ya wale walio chini, 

Wavuja jasho la ziada, 

Na kunyimwa faida.

 

Matuini yao, keshokuwa nafuu, 

Si kwamba uende juu, 

La, ila angalau wasile makombo,  

Ya mfumo ulo kombo

 

3.  MADHARI

Mshairi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia mandhari yafuatayo:-

(a)  Mandhari ya bara la Afrika.

Mshairi anazungumzia matatizo mbalimbali yanayolikabili bara la Afrika, zikiwemo nchi za Tanzania na Uganda, kupitia mashairi ya “Dakitari Askari” (uk. 11-26),  “Kademokrasi Katoweka”  (uk.30-31). “Thomas na Doto” (uk.37-42) na “Manzese Mpaka Ostabei” (uk. 42-54).  Baadhi ya maeneo ya Tanzaniayanayotajwa ni Ostabei, Manzese, Buguruni, Bukoba, Kagera, Forodhani, Tabora na Shule ya Sekondari Mchanganyiko iliyopo Dar es Salaam.  Eneo la Uganda linalotajwa ni Chuo Kikuu cha Makerere, Mandhari ya bara la Afrika yanaibua dhamira za umasikini, uonevu, dhuluma, udikteta, uongozi mbyaya, unyonyaji, athari za vita, ukombozi, usaliti, matabaka na mapenzi.

 

(b)  Mandhari ya nchi za Urusi na Marekani.

Mshairi anajadili namna nchi zilizondelea, zikiwemo Urusi na Marekani, zinavyoona ufahari kushindana kutengeneza silaha za moto, kama vile mabomu na silaha nyingine za kisasa.  Mshairi anahofia kutokea vita ya tatu ya dunia.  Mshairi anatumia mandhari haya katika shairi la “Tishio  la Binadamu” (uk. 1-2).  Mandari ya nchi za urusi na Marekani yanaibua dhamira za athari za vita, ukombozi wa kifikra, ukombozi wa kisiasa, hofu udikteta na ufahari.

 

(c)  Mandhari mengine yanayotajwa katika diwani hii ni hotelini, baa, jeshini, nyumbani kwa kuku, nyumbani kwa chatuk msituni, kambini, ufukweni na jikoni

 

4.  WAHUSIKA

Mwandishi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia baadhi ya wahusika waliotajwa majina yao waziwazi kama ilivyo katika riwaya na tamthiliya kama ifuatavyo:-

(a)  Katika shairi la “Dakitari Askari”(uk. 11-26), mshairi ametumia wahusika wafuatao:  Adam Kiende, Evadora Wesana, Luteni Bwege, manesi, Meja Mtanda, Josefu Manyai, Idi Amini Dada na Daktari Ngalakere.

 

(b)  Katika shairi la “Thomas na Doto” *uk. 37-42(, mshairi ametumia wahusika wafuatao:  Thomas, Doto, Mzee Roland (Baba wa Thomas), Rosalind (mama wa Thomas) na Roda (dada wa Thomas).

 

(c)  Katika shairi la “Manzese Mpaka Ostabei”(uk. 42-54), mshairi ametumia wahusika wafuatao:  Dorothy, Mashaka, Waziri Jonathan Shide (baba wa Dorothy), mama Dorothy, baba Mashaka, mama Mashaka na Gabrieli (mtoto wa Waziri wa Ulanguzi, msomi na jirani wa kina Dorothy).

 

(d)  Katika shairi la “Chatu na Kuku” (uk. 2-10), mshairi ametumia wahusika wafuatao:  Chatu, Kuku, Paku, Watoto wa Nyoka na Vifaranga vya Kuku.

 

Kadhalika, mwandishi wa diwani ya CHUNGU TAMU ametumia wahusika vikundi kama ifuatavyo:-

(a)  Wahusika wanasiasa

Mshairi amewatumia wahusika wanasiasa katika mashairi ya “Chungu Tamu” (uk.1), “Chini ya Mti Mkavu” (uk. 10), “Mjanja Yu Mashakani” (uk. 26-27), “Wanajua Kuvumilia” (uk.27), “Wimbo Wake Hotubani” (uk. 29-30), “Shairi la Udongoni” (uk. 35-36) na “Chanzo ni wenye Kauli” (uk. 28).  Wahusika hawa wanawakilisha yafuatayo:-

v Tabaka la  juu (tawala) linalonyonya, linalodhulumu, linaloonea na linalokandamiza tabaka la chini.

v Viongozi wasiowajibika na wazembe.

v Viongozi wanaoongoza kidikteta (kwa mabavu).

v Viongozi wasaliti na wanaotumia mali za umma kwa maslahi yao binafsi.

 

(b)  Wahusika wakulima (walima korosho na mihogo), wavujajasho, watwana, punda na ngamia.

Mshairi amewatumia wahusika hawa katikamashairiya “Chungu Tamu” (uk.1), “Chini ya Mti Mkavu” (uk.10),  “Mjanja Yu Mashakani”  (uk.26-27), “Wanajua Kuvumilia” (uk. 27) na “Wimbo Wake Hotubani” (uk.29-30).  Wahusika hawa wanawakilisha watu wa tabakala chini, masikini na wanaonyonywa na kukandamizwa na watu wa tabaka la juu (viongozi na matajiri)

 

(c)  Wahusika waganga (madaktari, matabibu, manesi).

Mshairi amewatumia wahusika hawa katika shairi la “Dakitari Askari”(uk. 11-26) kuwakilisha watu wachapakazi, wazalendo, wawajibikaji na wenyekujitolea katika kazi yao ya utabibu na majukumu mengine wanayopewa.

 

 

(d)  Wahusika mapadri.

Mshairi amewatumia wahusika hawa katika shairi la “Daktari Askari” (11-26) kuwakillisha watu wavumilivu, waaminifu, wanyenyekevu na wanaojitolea maisha yao kueneza habari za Mungu bila malipo yoyote.  Mshairi anawawakilisha watu wanaofanya kazi za wito; wasiofikiria kulipwa chochote.  Kimsingi watu wasio na wito hawawezi kuvumilia kazi ya kumtumikia Mungu kupitia upadri.  Mshairi anaeleza kuwa Adam Kiende na wenzake walijiunga namafunzo ya upadri.  Mshairi anaeleza kuwa Adam Kiende na wenzake walijiunga na mafunzo ya upadri wakidhani watapata raha eti kwa vile walikuwa wanaona mapdri wanapelekewa mikate na vinono vingine, lakini walishindwa kuendeleakwa sababu hawakuwa na wito.

 

MATUMIZI YA LUGHA

Aina ya lugha iliyotumika ni sanifu yenye misemo,nahau na methali, tamathali za semi,mbinu nyingine za kisanaa pamoja na ujenzi wa taswira.Lugha ya kishairi yenye uchaguzi maalum wa maneno (diction) imetumika.

MISEMO, NAHAU NA METHALI

·        Imetumiwa na mwandishi kwa lengo la kuwasilisha ujumbe kwa jamii husika. Mfano:-

Ø Sasa mwaleta shari (msemo) – uk 7

Ø Umoja ni nguvu (methali) –uk 6

Ø Kuvaa masulupwete (msemo) – uk 48

Ø Ndoa ni fumbo (msemo) – uk 42

Ø Usinawe kwa ulimbo (msemo) – uk 42

Ø Mapenzi hayana mipaka (msemo) – uk 40

Ø Utajichimbia kaburi (msemo) – uk 9

Ø Lakini haikutiwa chumvi mitaani (msemo) – uk 12

TAMATHALI ZA SEMI

TASHIBIHA

Ø Maoni yetu chakavu,sawa nguo ya miaka (uk 2)

Ø Macho yao mekundu mithili wavuta bangi (uk 6)

Ø Kwa msikilizaji husisimua mithili filamu za wachunga ng’ombe

Ø Shaba kama maji (uk 12)

Ø Kichwa chake kama cha kifutu (uk 38)

Ø Mwili ukamjaa harara kama jini lililokosa mbuyu (uk 41)

Ø Tumbo lake kubwa kama pipa (uk 50)

Ø Kichwa kidogo kama cha chatu (uk 50)

Ø Mweusi kama kiatu cha jeshi (uk 50)

Ø Utaonekana kama kinyago cha kuchonga (uk 12),n.k.

TASHIHISI

v Kifo kimeniita (uk 4)

v Njaa inawasaliti (uk 6)

v Kicheche pia ameapa (uk 7)

v Huzuni imenisaliti (uk 10)

v Katika ile baridi kali,mabomu ya mikono,yakatubusu miguuni (uk 16)

v Vichaka vikawakaribisha (uk 38)

v Taa za waka kwa maringo (uk 44)

v Jiji lasema hali ngumu (uk 44)

v Mapenzi hayana mpango, yakikanywa zaidi,hayana akili ati (uk53)

v Mioto ikapasua anga (uk 11), n.k.

SITIARI

§  Ushairi ni sukari tamu (uk 1)

§  Utoto ni kito (uk 2)

§  Yeye alisema dunia ni raha na tabu (uk 2)

§  Umaskini ni mzigo (uk 11)

§  Wote weusi wawa mkaa (uk 45)

TAFSIDA

·        Usiwe mwonja asali (uk 37)

·        Walipenda faragha (uk 51)

·        Dora ana kitu tumboni (uk 54)

·        Nimekula naye tunda (uk 56)

TABAINI

v Kuwaza na kuwazua

v Lakini usikubali raha tu, kumbuka na karaha (uk 13)

v Aponya aua  (uk 17)

KEJELI

·        Nyie yawafalia,mfanyakazi ya kuchoma na kuuza mkaa (uk 45)

·        Wa Manzese atakulisha taka (uk 52)

·        Jina lenye ugonjwa wa kaka (uk 52)

·        Iweje binti shibe aende kwa omba omba (uk 52)

DHIHAKA

Ø Ati mchumba, mchumba siye Baraka (uk 52)

MBINU NYINGINE ZA KISASA

TAKRIRI

Ø Mateka, mateka wapenzi (uk 22),

Ø Adamu, machozi (uk 20)

Ø je je, je….je nyingi (uk 43),

Ø Mateka, Mateka, wapewa (uk 22)

Ø Tukanyata, tukanyata tukakaribia Mbarara (uk 16)

MDOKEZO

Ø Je je je…je nyingi (uk 43)

Ø Si mganga wa tunguli…(uk 14)

Ø Sijui yaah yaah…(uk 44)

Ø Sijui Mashaka…(uk 53)

Ø Kati yao huyu…!(uk 51)

Ø Profesa Idd Amin…(uk 19)

Ø Ikawa nakupenda lakini…

NIDAA

·        Ati mie mzee1!

·        Ghafla mwewe huyu!

·        Umeshituka!

·        Mwauzunika nini!

·        Kwa hamu ya umoja!

TASHTITI

v Hujisikia wezi wakiomba Mungu kabla ya kwenda huko waendako? (uk 13)

v Wewe mwana –kibarua, hujioni? (uk 49)

MJAZIO

Ø Twaona wanaopelekewa chai, mikate, karanga, mayai…(uk 13)

Ø Ndugu mwenyekiti nadhani, labda, pengine, ningependekeza, kwa maoni yangu, kwa mfano tungeliweza….(uk 15)

ONOMATOPEA(TANAKALI SAUTI)

·        Lo! (uk 4)

·        Loooo! (uk 20)

LUGHA YA KIINGEREZA

·        Movement order (uk 14)

·        Surrender (uk 17)

·        Doctor where College? (uk 18)

·        Life President? (uk 19)

·        -Good Doctor (uk 19)

·        My first fiancé (uk 20)

·        But this is war sir (uk 20)

·        Look Adam. My parents are dead. I am alone (uk 23)

·        Sir is that a request or an order? (uk 24)

·        Two doctors fighting for no reason (uk 25) n.k.

TAFASIRI  YA MOJA KWA MOJA

Ø Fomu wani (uk 48)

UJENZI WA TASWIRA

Mwandishi ametumia baadhi ya taswira ili kufikisha ujumbe kwa jamii aliyoiandika. Baadhi ya taswira hizo ni kama vile:-

v Chatu (uk 2)…..Inawakilisha wadhulumaji (wakoloni)

v Kuku (uk2)……Inawakilisha wadhulumiwa (Waafrika)

v Vifaranga (uk 9)….Inawakilisha mali ghafi

v Mjanja (uk 25)….Viongozi wanaoshikilia mfumo wa chama kimoja

v Watwana (uk 25)….Wananchi wanaotaka mabadiliko au uongozi mbovu

v Ngulu (uk 33)….Vijiji, sehemu isiyo na maendeleo, sehemu iliyosahaulika

v Zabibu (uk 42)…..Msichana au mwanamke

MANDHARI

Kitabu hiki kiliandaliwa miaka ya 1980. Na matukio yanayosimuliwa katika kitabu hiki yanazungukia nchi za Afrika ya Mashariki hususani Tanzania na Uganda. Hata hivyo, maudhui ya kitabu hiki yanasadifu kipindi hiki cha  sasa katika nchi yoyote ile ulimwengu wa tatu.

 

JINA LA KITABU

Jina la diwani hii“Chungu Tamu’’ linasadifu yaliyomo ndani ya kitabu. Msanii ameonesha kuwa, baada ya kupita katika machungu na kuamua kupambana nayo ndipo utamu utafuata. Anaitaka jamii itumie kila mbinu kupambana na vikwazo vinavyokwamisha jamii isiweze kuupata utamu (ujenzi wa jamii mpya endelevu).Aidha msanii anaonesha kuwa katika maisha,uchungu na utamu havitengamani.Vile vile msanii ameonesha dhahiri kuwa, wananchi wa kawaida ambao ndio wazalishaji wanakula “Chungu” lakini viongozi ambao si wazalishaji wanakula “Tamu”.

KUFAULU KWA MWANDISHI

KIMAUDHUI

Mwandishi ameongelea masuala ambayo yanaisakama jamii yetu katika wakati huu tulio nao. Ameonesha mbinu mbalimbali za kufuata ili kufanikisha suala zima la ujenzi wa jamii mpya.

KIFANI

Mwandishi amefaulu kutumia miundo changamano,mitindo changamano,lugha ya kishairi pamoja na ujenzi wa taswira.

 

KUTOFAULU KWA MWANDISHI

v Lugha imejaa taswira kwa kiasi kikubwa na hivyo msomaji wa kawaida hawezi kuambulia ujumbe wowote.Hivyo amewanyima baadhi ya wasomaji uhondo wa kazi yake.

v Msanii metumia lugha ya Kiingereza (kigeni) katika baadhi ya mashairi.Huu ni udhaifu wa mwandishi,kwani anakinyima Kiswahili sanifu nafasi ya kuenea.Vile vile kwa mtu asiyefahamu Kiingereza atashindwa kupata ujumbe.

 

Powered by Blogger.