TAHAKIKI-FUNGATE YA UHURU

 


DIWANI : FUNGATE YA UHURU

MWANDISHI: MOHAMED S. KHATIBU

WACHAPISHAJI: DUP

MWAKA: 1988

UTANGULIZI

Fungate ni kipindi cha siku saba baada ya harusi.Ni kipindi ambacho Bwana na bibi harusi hula na kunywa tena milo ya kuchagua wakati wote wa fungate.Fedha na vifaa vitumiwavyo na maharusi huwa ni vya kuazima au kuchangiwa(si lazima viwe vyao) Wanapewa  kutoka kwa ndugu na jamaa zao na wanawekewa vijana wa kuwahudumia.Wachangaji hufanya hivyo kwa sababu wanajua kuwa fungate ni ya muda mfupi(siku saba tu),hivyo huvumilia.

Fungate ni lazima iwe na kikomo.Ikizidisha kikomo hicho ibadili jina labda iitwe unyang’anyi,ulimbwende,uvivu,uzembe au jina lolote lenye kashfa hasa unafiki au usaliti.Mwandishi wa diwani hii ameimwaga ghadhabu hiyo kwa hao maharusi waliohesabu ukarimu waliotendewa  kuwa ni upumbavu.

Uhuru ni neno linalopendwa sana na wanasiasa wa ubepari au ujamaa.Hekaheka za uhuru(kudai,kuomba au kupigania) zinaweza kufananishwa na shughuli za kutafuta mchumba,kupeleka posa kulipa mahari,na kufunga ndoa.

Katika kipindi chote cha uhuru, watu, hususani viongozi,hufurahi na kufanya sherehe ambazo huwagharimu raia-mali na vitu mbalimbali.Lakini kwa kuwa uhuru ni kitu cha thamani kama maharusi,raia hukubali kugharimia sherehe hizo.Lakini sherehe za uhuru kama fungate hutazamiwa iwe ya muda mfupi –labda mwezi  mmoja au miwili.

Raia wanchi zilizopata uhuru barani Afrika walikuwa na shauku ya kupata maendeleo lakini hawajafikia lengo lao hadi sasa kwa sababu viongozi wetu wanaendeleza Fungate ya Uhuru.Hivyo viongozi wanchi za Afrika wamewasaliti wananchi wao waliowachagua.Katika utangulizi mwandishi anasema;

Nikate tamaa?

Kwani twendavyo hatufiki,

Vile ipasavyo hayakamiliki,

Mambo yalivyo ni unafiki,

Tumesalitiwa!

 

MAUDHUI

Fungate ya Uhuru ni diwani inayojadili kwa mapana sana juu ya matatizo mbalimbali yanayokwamisha ujenzi wa jamii mpya hapa Tanzania.Matatizo hayo ni  kama vile usaliti,unafiki,wizi,hujuma,udanganyifu,rushwa pamoja na uongozi mbaya.

DHAMIRA KUU: UJENZI WA JAMII MPYA.

Mwandishi anajadili kwa kiasi kikubwa suala la ujenzi wa jamii mpya.Mwandishi anaitaka  jamii  itupilie mbali unyonyaji ,uonevu, dhuluma,udanganyifu,wizi,unafiki,umasikini,uongozi mbaya na ukandamizaji wa watu wa tabaka la chini ili kuijenga jamii kwa upya.Jamii ambayo hatamu zote za uongozi (utawala,siasa na uchumi) zitakuwa mikononi mwa wakulima na wafanyakazi kwa misingi ya haki na usawa.

Itikadi ya kujenga jamii mpya ilijengeka juu ya siasa ya ujamaa na kujitegemea ambayo ilitangazwa mwaka 1967 baada ya kutangazwa kwa  Azimio la Arusha.Hadi 1988,mwandishi anaandika diwani hii anaonesha kuwa bado hatujafanikiwa kujenga jamii mpya hapa Tanzania.Hii inatokana na sababu zifuatazo;

Kwanza,bado kuna dhuruma, usaliti,unyonyaji na wizi wa mali za umma.katika  shairi laWingu’’ mwandishi anasema;

Bado,

Wingu limetanda,

Limetanda.

Na kutughubika ghubi,

 

Mvua,

Lakini hainyeshi,

Hainyeshi,

Ukame umetanda waa!

 

Mimea,

Tulipanda kwa miongo,

Kwa miongo,

Yote imekauka!

Pia katika shairi la Wizimwandishi ameonesha dhahiri kuwa wizi umo ikuluni,bomani,kanisani,misikitini na hekaluni.Mwandishi ameonesha kuwa dini za wabariki wezi,polisi hulinda wezi na majeshi huhalalisha wizi.katika ubeti wa 1 mwandishi anasema;

Wizi umo;

Kanisani,

Msikitini,

Hekaluni

Wanyang’anywao ni waumini.

Pili,Bado kuna matabaka katika jamii zetu.Mwandishi ameonesha kuwa kuna tabaka la wenye nacho na tabaka la wasionacho.Tabaka la juu (utawala) unaolinyonya tabaka la chini(tawaliwa).Mfano katika shairi la “Fungate” mwandishi ameonesha jinsi tabaka tawala linavyofurahia maisha kwa kuishi katika majumba mazuri, kutembelea magari ya kifahari, n.k.

Katika shairi laWaja wa Mungumwandishi anaonesha jinsi tabaka la chini linavyoishi kwa shida.Kwa mfano, kula kwa shida, kulala kwa shida, kuvaa kwa shida, hawapati elimu na huduma nzuri za afya.

Tatu,Bado kuna uongozi mbaya katika jamii zetu.Mfano katika shairi la “Viongozi wa Afrikamwandishi anashutumu vikali viongozi wanaotumia  madaraka  yao  vibaya na kugandamiza watawaliwa.Mwandishi anasema;

Viongozi wa Afrika,

Wanaotawala kwa mabavu,

Kujifanya ni washupavu,

Wao wachache ni werevu,

Na umma wote ni mpumbavu,

Wanafiki,

Wazandiki”.

Pia katika shairi la “Njama” mwandishi anaonesha  jinsi viongozi wanavyotumia njama mbalimbali kulinyonya tabaka tawaliwa.Viongozi wanatumia njama mbalimbali ili kuhakikisha kuwa hakuna anayewapinga wala kuhoji hata kidogo.

Nne,Bado kuna unyonyaji wanaofanyiwa wakulima katika kuuza mazao yao.Mwandishi ameonesha kuwa wakulima hunyonywa na kudhurumiwa na kupewa bei kidogo wakati  wa kuuza mazao yao.Katika shairi la “Naona linadhihirisha haya katika ubeti wa 6,Mwandishi anasema;

Naona

Wanakwenda gulioni

Mazao kuyazabuni

Wanapata bei duni

Na kubaki maskini

Unyonge ulele.

Kutokana na matatizo ya wizi,rushwa,uongozi  mbaya,dhuluma, uonevu na unyonyaji ndiyo maana tumeshindwa kujenga jamii mpya.

Mwandishi ameonesha mbinu mbalimbali ambazo jamii inapaswa kuzitumia ili  kuijenga jamii mpya na hizo ndizo  dhamira ndogo ndogo za diwani hii kama zifuatazo;

 

1.     UONGOZI MBAYA

Uongozi mbaya ni kikwazo kikubwa  katika ujenzi wa jamii mpya.Katika shairi laFungate” mwandishi ameonesha jinsi viongozi wanavyotumia madaraka yao vibaya kwa kuwanyonya wananchi wa kawaida.Katika ubeti wa 1 mwandishi anasema;

 

Fungate ya uhuru,bado inaendelea,

“Harusi” wana nuru,wazuri wanavutia,

Wengi inawadhuru,na tena wanaumia

Mwandishi anaeleza kuwa tangu tupate uhuru hadi leo bado viongozi wetu wapo Fungate wakila na kunywa huku wananchi wakiendelea kuteseka na maisha magumu,hivyo mwandishi anaitaka jamii kuung’oa  uongozi mbaya na kusimika uongozi uliobora unaowajali wananchi wake .

Katika shairi la “Viongozi wa Afrikamwandishi anakemea viongozi wanaotumia madaraka yao vibaya kwa kujinufaisha wao wenyewe, wenye hisa katika viwanda,mabenki,makampuni au mashamba ya mabepari kuwa ni wasaliti.Mwandishi anawakemea wale viongozi wenye upendeleo,wanaotumia pesa za umma kwa kuendeshea sherehe.Mwisho anawakemea viongozi wanaopokea rushwa na amewaita magaidi au mafisadi.

Katika shairi la Utawala mwandishi amehimiza kuangusha utawala wa kibepari ambao unawanufaisha wachache na walio wengi hunyonywa,hugandamizwa,huonewa na kunyanyaswa na hao wachache.

Katika shairi la “Kinyang’anyiro” mwandishi anaonesha jinsi viongozi walivyokimbilia kushika madaraka (hasa enzi za uhuru) lakini wanashindwa kuleta maendeleo hapa nchini.

Kwa ujumla mwandishi anapendekeza kuwa, ili tujenge jamii mpya lazima tuwe na uongozi bora.

2.  UMOJA NA USHIRIKIANO

Mwandishi anaona kuwa  ili tujenge jamii mpya ni muhimu tuungane  sote tuwe kitu kimoja.Katika shairi la “Unganeni mwandishi anawataka wananchi wote wa Afrika kuungana ili kuendeleza mapambano ya kuleta haki na usawa. Anasema:-

Wafanyakazi wa Afrika,tuunganeni,

Na wakulima kadhalika,tushikaneni,

Makabwela  mnaosumbuka,tukutaneni,

Tujiandae kwa mapambano yalo marefu,

Ushindi ni wetu”.

Mwandishi anaitaka jamii hasa tabaka la chini kuungana na kuendeleza mapambano dhidi ya viongozi wanafiki,mabepari, mamwinyi,wanaonyonya,wanaonyanyasa,wanaowatesa, wanaowadhulumu na kuwagandamiza watu wa tabaka la chini. Katika shairi la “Nikizipata Bunduki‘’anapendekeza  matumizi ya silaha ili kuondokana na matatizo hayo yote.Hivyo ili tujenge jamii mpya ni lazima tuungane tuwe kitu kimojakwani ‘’Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu’.

 

3. UJASIRI NA KUJITOA MHANGA

Mwandishi anaona ili kuijenga jamii kwa  upya ni muhimu kuwa na ujasiri,kutoogopa vitisho.Katika shairi la “Gorila ubeti wa1 mwandishi anasema;

Gorila,jasiri!

Wa Afrika,shujaa,mshupavu,umevinjari,

Mtutu shika,mevaa,ukakamavu,uko tayari,

Gorila,ruwaza,wa kizazi kipya

Mwandishi anaitaka jamii hasa vijana kuwa jasirii na shujaa katika harakati za kuleta mapinduzi.Pia wanamapinduzi wanatakiwa wawe wavumilivu kwa sababu ujenzi wa jamii mpya sio lelemama,ni safari ndefu yenye vikwazo vingi.

Vile vile katika shairi la “Umma mwandishi anahimiza ujasiri katika kuleta mapinduzi katika jamii. Mwandishi nasema:-

Umma,

Uliovinjari,kuangamiza mtabaka,

Hima,

Uwe tayari,wala usiwe na shaka,

Ongoza mapinduzi,

Ya wafanyakazi,

Hadi ushindi.

Hivyo mwandishi anaitaka jamii ijitoe mhanga ili kufanikisha suala la ujenzi wa jamii mpya.

 

4. KUFANYA MAGEUZI (MAPINDUZI)

Mwandishi anapendekeza mbinu ya kufanya mageuzi ili kufanikiwa katika suala zima la ujenzi wa jamii mpya.Katika shairi la “Umma mwandishi anawaasa wanajamii wajiandae kuangamiza matabaka yaliyokithiri katika jamii.

Mwandishi anapendekeza mbinu mbalimbali za kufanya mageuzi (mapinduzi) ambazo ni;

Kwanza,jamii hasa watu wa tabaka la chini waungane ii kuondoa viongozi wanaotumia madaraka waliyopewa kwa manufaa yao binafsi. Katika shairi la “Ungameni” mwandishi anasema;

Msimamo wa kitabaka,tuwekeni,

Bepari wote kuwashika,wawe ndani,

Na mamwinyi bila ya shaka,wambaroni,

Tusizubae,kazi ianze,twangoja nini?

Wakati ni huu.

Pili,mwandishi anapendekeza kutumia silaha katika mageuzi hayo ikiwa unyonyaji hautaondoka kwa amani.Mfano Katika shairi la “Siku Itafikana “Nikizipata Bunduki”na“Utawala” mwandishi anapendekeza yafanyike mgeuzi  ili kuuangusha utawala unaojinufaisha na kuendeleza matabaka katika jamii.

Katika shairi la “Mjamzito”mwandishi anaonesha jinsi watu wanavyoogopa harakati za mapinduzi katika jamii zetu.

Katika mashairi ya “Ni vita si Lelemama” na “Maendeleo ya Umma” mwandishi anaonesha jinsi suala la mageuzi lilivyo gumu, ingawa anamatumaini kuwa umoja na ushirikiano wetu utatufanya tushinde.Pia anaamini kuwa unyonyaji na uonevu hautadumu milele,kwani kuna siku,saa,dakika na nukta itafika uovu wote utaondolewa kwa nguvu.

Katika shairi la “Joka La Mdimu” mwandishi anatoa mfano wa tawala dhalimu zilizoondolewa kwa nguvu kwa ushirikiano wa tabaka la chini. Katika shairi hili mwandishi anaonesha jinsi wananchi walivyoshirikiana katika kuutokomeza ukoloni hapa nchini.

Hivyo ili nasi tufanikiwe kujenga jamii mpya hatuna budi kufanya mapinduzi (mageuzi).

 

5. SUALA LA  UZALENDO

Uzalendo ni ile hali ya kuipenda nchi kwa dhati na hata kuifia. Msimamo wa mwandishi ni kuwa hataihama nchi yake hata kwa kutishiwa njaa,maafa au umaskini.Pia ataipigania nchi yake ili iwe salama.Hivyo hata sisi hatuna budi kuipigania nchi yetu kwa hali na mali ili kuondoa udhalimu uliopo.Katika shairi la Nchi Yangu”  mwandishi anasema;

Naipenda nchi yangu,

Naipenda,naipenda nitakufa naipenda.

Tailinda nguvu zangu,tailinda,

Tailinda kwa maafa tailinda,

Sitakwenda kwa wenzangu,

Sitakwenda,sitakwenda hata sifa sitakwenda,

Nitakwenda huku kwangu,nitaganda,

Nitaganda kwa ulofa nitaganda.

Mwandishi anaona kuwa,tukiwa na uzalendo na nchi yetu tutafanikiwa kujenga jamii mpya,kwani usaliti wa viongozi wetu utaanguka na kila mmoja ataipenda nchi yake kwa  dhati.

 

6. UKOLONI MAMBOLEO

Ukoloni mamboleo ni ile hali ya nchi kupata uhuru wa bandia (kisiasa) lakini njia zote za uchumi hutawaliwa au hubaki mikononi mwa mabepari au watu wa nchi nyingine.Katika shairila “Ruya  mwandishi anasema;

Ruya,menitoa shamba,mji kuuramba niwe utumwani?

chini umwinyini,

nimo kifungoni!

Ni ‘’huru’’ machoni!

 

Ruya,hivyo wanitimba,kunifunga kamba,za ukoloni,

Njozi niondokee!

Mwandishi anaona kuwa wazungu ndio walioondoka katika ardhi ya Afrika lakini unyonyaji bado upo na unaendelea.Viongozi waliochukua madaraka baada ya uhuru bado wanaendeleza zile taratibu zilizoachwa na wakoloni.

Katika shairi la “Kunguru mwandishi anaonyesha athari za ukoloni mamboleo hapa nchini.Katika shairi hili mwandishi anazungumzia juu ya kuondoka kwa ukoloni mamboleo.Hivyo mwandishi anaonesha kuwa ili tujenge jamii mpya ni lazima tupige vita ukoloni mamboleo ili tuwe na uhuru wa kuamua mambo yetu wenyewe.

7.  WIZI WA MALIYA UMMA

Mwandihi wa diwani hii ameshindwa kuficha hasira yake dhidi ya wizi.Ameutaja wazi kuwa wizi umo kanisani,msikitini,Ikuluni na bomani.Waandishi wengi hukwepa kutaja ukweli kama huu. Asemacho mwandishini kwamba,sehemu zote za jamii zimeoza. Zamani watu wengi waliamini kuwa viongozi wa dini wana maadili wasiyoweza kuyakiuka.Kwa hiyo,maovu hayo yasingetokea huko. Lakini sasa viongozi hao na wale wa Ikulu wamejiunga na wahalifu. Lililo baya zaidi ni kuwapo kwa “Walinzi” wanaolinda hao wezi.Katika shairi hili la “wizi” mwandishi anasema;

Wizi umo;

Kanisani,

Msikitini,

Hekaluni,

Wanyang’anywao ni waumini.

Kwa kifupi wizi umehalalishwa na kubarikiwa na kuonekana kama ni jambo la kawaida kabisa.

Mwandishi  hasemi tufanyeje  lakini kwa mtiririko na mantiki ya mashairi yake mengine,mwandishi anashauri ufumuaji na usafishaji wa jamii nzima.Katika  shairi la“Kunguru” mwandishi pia anajadili Suala la wizi .Japo amefumba  lakini anawaelimisha wasomaji kuhusu wezi waliotimuliwa na kutawanywa.Baada ya muda wezi wakajitayarisha kwa mbinu tofauti na kuendeleza wizi wao. Mwandishi anatanabaisha raia kuhusu kuwapo kwa wezi hawa na marafiki zao.Katika shairi la “Joka la Mdimuni mwandishi anatanabaisha watu kuhusu uwezekano wa wakoloni kurudi kwa umbo tofauti lakini kwa athari zile zile.Katika shairi la “Naona  mwandishi anaonesha taabu wanazopata wakulima na malipo duni wanayopewa kwa mzao yao.Anamaliza kwa msimamo huu;

‘’Naona

Ni fukara wakulima

Wamepigwa ulitima

Kwa wengine ni neema

Kwao wao ni nakama

Wamekosa haki!

 

8. KUPIGA VITA UKASUKU WA VIONGOZI WETU

Mwandishi amekemea tabia za viongozi na watendaji wengine kukubali kila lisemwalo bila kufikiri au kwa hofu tu,si nzuri.Tabia hii ya ukasuku anauita ugonjwa unaohitaji tiba (tiba yenyewe hakuitaja).Ugonjwa huu hudunisha akili.Mwandishi anaonyesha  chanzo na athari zake.Katika shairi la “Ukasuku” mwandishi anasema;

Kupea kwa ukasuku

Rais huhubiri

Wabunge hukariri

Wasomi huhariri

Na taifa husimama”.

Mwandishi  anawachunguza viongozi wa bara la Afrika na kuwaona kuwa ni mabepari,madikteta,wenye ukabila,wabadhirifu wasiojali raia wao wapenda hongo.Wote amewakemea na kuwakanya wasitende hivyo. Amewapa majina yanayowafaa- wahaini, wasaliti, majasusi n.k.Mwandishi anastahili pongezi kwa kuweza kuwakemea, badhi ya viongozi badala ya kuwasifu.

UJUMBE

v Uongozi mbaya,wizi wa mali ya umma,rushwa na kukosekana kwa haki,ukasuku na matumizi mabaya ya mali ya umma ni vikwazo  kikubw katika ujenzi wa jamii mpya hapa nchini.

v Umoja na ushirikiano ni njia moja wapo ya ujenzi wa jamii mpya hapa nchini.

v Mfumo wa ujamaa ni mfumo wa pekee utakaomkomboa mtu mnyonge,yaani ndiyo utakaoleta hali nzuri kwa wakulima na wafanyakazi.

v Ili tujenge jamii mpya ni lazima tuwe na ujasiri wa kujitoa mhanga,tuwe wazalendo na nchi yetu na tufanye mapinduzi (mageuzi ya kweli) katika jamii.

v Ukoloni mamboleo ni kikwazo cha ujenzi wa jamii mpya hapa nchini.

v Mapenzi ya kweli ni yale yasiyojali fedha au hali ya mtu.

 

FALSAFA

Mwandishi anatetea itikadi ya ujamaa yenye kuleta haki na usawa kwa kila mtu.Analaani wizi,dhuluma na majivuno ya kirasimu. Mwandishi angependa nchi iongozwe kwa haki na usawa.Vile vile anatetea mapenzi ya kweli katika maisha.

 

MSIMAMO

Mwandisi ana msimamo wa kimapinduzi,kwani ameonesha matatizo mbali mbali yanayozikumba jamii zetu na mbinu za kuondokana na matatizo hayo.Miongoni mwa matatizo hayo ni uongozi mbaya,wizi wa mali ya umma,rushwa na dhuluma, n.k.

 

FANI

1. MITINDO

Mwandishi wa diwani ya FUNGATE YA UHURU ametumia mitindo ifuatayo:-

(a) Mitindo changamano

Huu ni mtindo unaohusisha mashairi yenye kutumia mtindo wa kimapokeo na mtindo  wa kisasa.

(i) Mtindo wa kimapokeo

Huu ni mtindo unaofuata au unaozingatia urari wa vina, mizani na beti za mashairi.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kimapokeo katika diwani hii ni”Kuntu Sauti ya Kiza” (uk. 33), “Ladha ya Maji Katani” (uk. 35-37),“Mcheza Hawi Kiwete” (uk.37-38), “Sakubimbi” (uk.44), “Paka Shume” (uk.45), “Uwapi Uzuri Wako” (46-47), “Ua Si Ruwaza Njema” (uk.47-48) na “Wewe Peke Yako” (uk.45).  Kwa mfano, katika shairi la “Ua Si Ruwaza Njema” (uk.47-48), mshairi anasema:

“Ua huvishwa mgeni, Mtukufu akifika,  

Ni koja la asumini, shingoni linajiweka, 

Mara utalibaini, walinzi wamelishika, 

Ua si ruwaza njema, tunzo ya mtu kupewa”.

 

(ii)  Mtindo wa kisasa / kimamboleo

Huu ni mtindo usiofuata au usiozingatia urari wa vina, mizani na beti za mashairi.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kisasa au kimamboleo katika diwani hii ni “Maendeleo ya Umma” (uk. 2-4), “Mjamzito” (uk. 7-8), “Ukasuku” (uk.30-31), “Mwinyi mpe ‘Ndiyo’ ” (uk.32),  “Siku itafika”(uk.39-40) na”Kinyang’anyiro” (uk.43-44).  Kwa mfano, katika shairi la “Ukasuku” (uk.30-31), mshairi anasema:

                  ‘’Athari za ukasuku,

                  Akili mufilisi,mawazo mepesi,na hayana kasi,

                  Vipawa vimedumaa’’

( b ) Mtindo wa tenzi

   Ni mtindo ambao mshororo (mstari)mmoja wa shairi huundwa na kipande kimoja tu.Aghalabu,mshororo mmoja wa ubeti wa shairi la mtindo wa tenzi huwa na mizani ( silabi ) kati ya 6 hadi 11 tu.Tenzi huwa na ulinganifu wa silabi za mwisho kwa kila mshororo au mstari wa ubeti.Mashairi yaliyotumia mtindo huu wa tenzi katika diwani hii ni’kunguru na Naona.Katika shairi la kunguru mshairi anasema;

“Kunguru hawakushituka,  

Ila kuzidi kucharuka, 

Raia wakakusanyika, 

Pambano jipya kuliweka.

 

Zikatumika na bunduki,  

Wengine wengi kufariki,  

Haba wakahama miliki,  

Lobaki hawabadiliki”.

 

(c)  Mtindo wa kidato

Huu ni mtindo ambao mshairi hutumia baadhi ya mistari iliyofupishwa maneno au silabi tofauti na mistari mingine ambayo huwa na silabi au maneno mengi.Mbinu ya kidatu hutumiwa na mshairi kwa lengo maalumu hususani katika kufikisha ujumbe wake kwa jamii iliyokusudiwa.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kidato katika diwani hii ni “Maendeleo ya Umma” (uk.2-4), “Tumesalitiwa!” (uk. 5), “Haki” (uk.5), “Mjamzito” (7-8), “Nikizipata Bunduki” (uk. 11-13), “Ruya” (uk. 13-14), “Pungo” (uk. 16-18), “Viongozi w Afrika” (uk.21 -22), “Afrika” (uk. 22-23),”Ukasuku” (uk. 30-31) “Si Wewe?” (uk. 38-39),  “Siku Itafika” (uk.39-40) na “Kinyang’anyiro” (uk. 43-44).  Kwa mfano, katika shairi la “Nikizipata Bunduki” (uk.11-13), mshairi anasema:

“Ningekuwa na Sauti,  

Malaya ngewapa kazi, ya shamba na ofisini, 

Na wezi na majambazi, wangekuwa viwandani, 

Wakosefu,

Marufuku, si wachafu, 

Si halifu,

Sauti haziwalishi”

                                                    

(d)   Mtindo wa kikufu au pindu

Huu ni mtindo ambao neno au sehemu ya neno ya mshororo wa kwanza inayomalizia huanzia katika mshororo wa ubeti unaofuata.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kikufu au pindu katika diwani hii ni “Nataka Kusema” , “Mkata”, “Kinyang’anyiro” na “Nyayo”.  Kwa mfano, katika shairi la “Nataka Kusema”, mshairi anasema:

“Nataka, kusema yote,  

Yote yaniumizayo moyo, lakini;  

Nna kitata, siwezi kutamka!  

 

Nataka kutema mate, 

Mate, yanichafuayo moyo, lakini;  

Yamekauka, jelezi menishika!”

 

(e)  Mtindo wa kuandika vibwagizo katika mashairi

Kwa kawaida vibwagizo au viitikio hupatikana katika kipera cha nyimbo lakini baadhi ya washairi hutumia mbinu ya kuandika vibwagizo au viitikio katika mashairi wanayoyatunga.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa kuandika vibwagizo katika mashairi kwenye diwani hii ni “Sakubimbi”  (uk. 44),  “Paka Shume” (uk. 45), “Nia Yangu Sigeuzi”  (uk.46) na “U Wapi Uzuri Wako” (uk.46-47).

 

Katika shairi la “Sakubimbi”  (uk. 44), mshairi anasema:

“Usijione mwerevu, umestaarabika,  

Yakakuvimba mashavu, na kichwa kukupanuka,  

Huo sio ushupavu, ni ujinga natamka.

         

                   Kibwagizo:

                   Umelichimba kaburi, mzima utajizika, 

Huna tena ujasiri, sakubimbi umefika”

 

Katika shairi la “U Wapi Uzuri Wako”  (uk. 46-47), mshairi anasema:

“Sasa ni chano cha mji, watu wajichanyatia,  

Umekwisha ujuwaji, haya zimekupotea,  

Yale usoyataraji, kwako yamekuhamia.

 

Kibwagizo:

U wapi uzuri wako, ya wapi maringo yako”.

 

(f)  Mtindo wa mashairi yenye vina vitatu

Kwa kawaida mashairi ya kimapokeo huwa na mshororo (mstari) mmoja unaoundwa au unaogawanywa katika vina viwili yaani kina cha kati na kina cha mwisho.Mwandishi wa diwani hii ametumia baadhi ya mashairi yenye mstari mmoja unaoundwa kwa vina vitatu,yaani kina cha kwanza,kina cha pili na kina cha tatu.Mashairi yaliyotumia mtindo wa mashairi yenye vina vitatu katika diwani hii ni “Dafina”,  “Mkata” na “Waja wa Mungu”.Kwa mfano, shairi la  “Waja wa Mungu” , mshairi anasema:

Duniani, nguo mbovu matakoni, mafakiri,  

Lakini, nguo tele kabatini,  mabepari,

Abadani, hawa si waja wa Mungu!”

 

(g)  Mtindo wa mashairi yenye vina vinne

Mashairi ya kimapokeo huwa na mshororo (mstari)  mmoja unaoundwa au unaogawanywa katika vina viwili yaani kina cha kati na kina cha mwisho.Mwandishi wa diwani ya FUNGATI YA UHURU ametumia baadhi ya mashairi yenye mstari mmoja unaoundwa kwa vina vinne,yaani kina cha kwanza, kina cha pili, kina cha tatu na kina cha nne.Mashairi yaliyotumia mtindo wa mashairi yenye vina vinne katika diwani hii ni “Ruya” na “Gorila”.

Katika shairi la “Ruya”, mshairi anasema:

Ruya, unanitonesha, donda lilokwisha, hapo zamani,

Njozi niondokeya!”

 

Katika shairi la “Gorila”, mshairi anasema:

“Gorila, jasiri!,

Wa Afrika, shujaa, mshupavu, umevinjari,

Mtutu shika, mevaa, ukakamavu, uko tayari,

Gorila, ruwaza, wa kizazi kipya”.

 

(h) Mtindo wa kuhoji

Huu ni mtindo unaotumiwa na washairi wa kuuliza maswali ambayo ama majibu yake yako wazi au hayako wazi.Mashairi yaliyotumia mtindo wa kuhoji au  kuuliza maswali katika diwani hii ni “Si wewe?”  “Tumesalitiwa!”  na “Ruya”.Kwa mfano, katika shairi la “Si Wewe?” mshairi anasema:

 

 

 

“Si wewe?  

Nilokuanzisha kula ubwabwa wa mapenzi,  

Ikawa wauchakua kwa ufizi,  

Ukatapika kwa kuona jelezi,   

Hukujua kutafuna,   

Ni wewe umwanagenzi!  

 

Si wewe?  

Lonililia kwa kwikwi kaamua kukubeba,  

Nikakunyonyesha ziwa la mahaba,   

Kapapia hukusubiri kushiba,  

Na sasa umepaliwa,  

Ni wewe unayejutia”.

 

(i)  Mtindo wa msisitizo au takriri

Huu ni mtindo ambao neno moja linatokea mwanzoni na linarudiwa katika mishororo au mistari ya ubeti wa shairi .Mashairiyaliyotumia mtindo wa msisitizo au takriri katika diwani hii ni “Nchi Yangu”,Dafina”.Kwa mfano katika shairi la “Nchi Yangu” ,mshairi anasema:

              “Naipenda nchi yangu,  

Naipenda, naipenda nitakufa naipenda. 

Tailinda nguvu zangu, tailinda,

Tailinda kwa maafa tailinda,  

Sitakwenda kwa wenzangu, 

Sitakwenda,sitakwenda hata sifa sitakwenda,

Nitakwenda huku kwangu,nitaganda,

Nitaganda kwa ulofa nitaganda

 

(j)  Mtindo wa nafsi

Huu ni mtindo ambao mshairi anaweza kutumia nafsi umoja,nafsi wingi au nafsi kundi kwa lengo la kufikisha ujumbe au maudhui fulani kwa jamii.Kuna nafsi za aina tatu (3),yaani nafsi ya kwanza (umoja na wingi),nafsi ya pili (umoja na wingi)na nafsi ya tatu (umoja na wingi).  Mwandishi wa diwani hii ametumia mtindo wa nafsi kama ifuatavyo:-

(i)  Matumizi ya nafsi umoja (nafsi ya kwanza umoja na nafsi ya pili umoja):

Mshairi huzungumzia jambo linalomhusu mtu mmoja pekee.  Hujumuisha ahadi,matamanio, sifa, mawaidha na maonyo. Mashairi yaliyotumia nafsi ya kwanza umoja ni “Nikizipata Bunduki” , “Ruya”,  “Nataka Kusema” na “Mkata”.Kwa mfano kama mshairi la “Nikizipata Bunduki  mshairi anasema:

 

Nikivipata Vitara,  

Nitawachinja wakubwa,wanaonyonya masikini,  

Namali zao kukabwa, kugaiwa watu duni, 

Tafilisi,  

Ubinafsi, kwa upesi,  

Na kwa kasi,  

Sauti haziwafishi!”.

 

Pia mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya pili umoja katika diwai hii ni “U Wapi Uzuri Wako”,“Si Wewe?”,“Paka Shume” na “Sakubimbi”.  Kwa mfano katika shairi la “U Wapi Uzuri Wako”,mshairi anasema:

“Sasa ni chano cha mji, watu wajichanyatia,  

Umekwisha ujuwaji, haya zimekupotea,  

Yale usoyataraji, kwako yamekuhamia”.

 

(ii)  Matumizi ya nafasi wingi (nafsi ya kwanza wingi)

Mshairi huzungumzia jambo au suala lialohusu kundi fulani la watu akiwemo nayeye mwenyewe.Mashairi yaliotumia mtindo wa nafsi ya kwanza wingi katika diwani hii ni “Unganeni!” ,“Utawala”,“Ukasuku” ,“Ni Vita Si Lelemama” na “Siku Itafika” .Kwa mfano katika shairi la “Unganeni”,mshairi anasema:

“Kunyonywa pia kunyanyaswa, tukataeni,  

Kuteswa na kukandamizwa, tukupingeni,  

Si kusengenyewa si kuteswa, tuchukieni,  

Tujadhibike, turaghibike, tujadibike,   

Potelea mbali!”.

 

(iii)  Matumizi ya nafsi kikundi (nafsi ya tatu wingi)

Mshairi huonekana ama akisimulia hadithi, akitoa hotuba au akizungumzia kundi fulani la watu kuhusu suala au jambo muhimu.  Mashairi yaliyotumia mtindo wa nafsi ya tatu wingi katika diwani hii ni “Naona” (uk. 41-42),  “Maendeleo ya Umma”  (uk.2-4),  “Viongozi wa Afrika”  (uk.21-22),  “Wengine”  (uk.24), “Wizi”  (uk.25), “Waja wa Mungu (uk.27) na “Kunguru” (uk.26-27).  Kwa mfano katika shairi la “Naona”  (uk.41-42), mshairi anasema:

“Naona  

Jasho lawatiririka 

Na majembe na mashaka 

Wakulima wameshika  

Mashamba yao kufyeka  

Ni wachapakazi!

 

 

 

Naona

Ni fukara wakulima  

Wamepigwa ulitima  

Kwa wengine ni neema  

Kwao wao ni nakama  

Wanakosa haki!”

 

 

2.   MUUNDO

Mwandishi wa diwani ya FUNGATE YA UHURU ametumia miundo tofautitofauti kwa kuzingatia vigezo mbalimlbali kama ifuatavyo:-

Ø Kigezo cha idadi ya mishororo:

Kwa kuzingatia kigezo cha idadi ya mishororo kwa kila ubeti mshairi ametumia miundo ifuatayo:-

(a)  Muundo wa tathnia

Ni  muundo ambao kila ubeti unaundwa na mistari miwili .Shairi lililotumia muundo wa tathnia katika diwani hii ni”Mjamzito” (uk.7-8), Mshairi anasema :

Mjamzito amelazwa thieta! 

Lazima kupasuliwa.

 

Chake kitoto, Tumboni kinatweta, 

Hawezi kujifungua”.

 

(b)  Muundo wa tathilitha.

Huu ni muundo ambao kila ubeti unaundwa kwa mistari mitatu.  Mashairi yaliyotumia muundo wa tathilitha katika diwani hii ni “Fungate”,  “Waja wa Mungu”, “Sakubimbi”,  “Paka Shume”,  “Wewe Peke Yako” “Nia Yangu Sigeuzi”  na “U Wapi Uzuri Wako” .Kwa mfano, katika shairi la “Fungate” , mshairi anasema:

“Karamu za fahari, mabembe ya kupepewa,  

Na mafumba mazuri, wamekwisha jijengea, 

Watembea kwa magari, hivi zimewazowea”.

 

(c)  Muundo wa tarbia:

Ni muundo ambao kila ubeti unaundwa kwa mistari minne.Mashairi yaliyotumia muundo wa tarbia katika diwani hii ni “”Nahodha Mtwesi   “Gorila” ,“Kunguru”  (uk.26-27),  “kuntu Sauti ya Kiza” “Ni Vita Si Lelemama” ,“Wingu” ,“Mcheza Hawi Kiwte” na “Ua Si Ruwaza Njema” Kwa mfano, katika shairi la “Nahodha Mtwesi”,mshairi anasema:

“Nahodha mtwesi, Chombo chenda joshi,  

Stadi wa kukisi, hupendi ubishi,  

Mahiri, jasiri wa ari, hukeri, 

Hatwendi mrama”

 

(d)  Muundo wa takhimisa.

Ni muundo kila ubeti unaundwa kwa mistari mitano. Mashairi yaliyotumia muundo wa takhimisa katika diwani hii ni “Unganeni”, “Tumesalitiwa” ,“Ningekuwa na Sauti”, “Wizi” “Utawala” (uk.28-29), “Njama” ,“Nyayo”  na Ladha ya Maji Katani ,Kwa mfano, katika shairi la  “Tumesalitiwa” mshairi anasema:

Nikate tama?  

Kwani twendavyo, hatufiki. 

Vile ipasavyo, hayakamiliki.  

Mambo yalivyo, ni unafiki  

Tumesalitiwa!”

 

(e)  Muundo wa sabilia:

Ni muundo unaohusu mashairi yanayoundwa kwa mistari sita na kuendelea katika kila ubeti.  Mashairi yalyotumia muundo wa sabilia katika diwani hii ni “Maendeleo ya Umma” (uk.2-4), “Nchi Yangu” (uk.6), “Dafina”, “Nikizipata Bunduki” ,“Pungo” ,“Mkata”,  “Viongozi wa Afrika” ,“Wengine” , “Ujamaa” ,Mwinyi Mumpe Ndiyo” ,“Si Wewe?”  “Siku Itafika”  na “Naona” .Kwa mfano, katika shairi la “Pungo”,mshairi anasema:

             “Kilingeni mwari ametulia,  

Na mganga anamwangalia,   

Pepo anajitamkia,   

Jina anamtajia,  

Na chanzo cha udhia,  

Mwele tamwachia, 

Awe huria.  

Na fiya,  

Pamoya,  

Na wana”

 

 

 

 

Ø Kigezo cha idadi ya vipande:

Kwa kuzingatia idadi ya vipande  kwa kila mshororo katika ubeti wa shairi, mwandishi wa diwani ya FUNGATE YA UHURU ametumia miundo ifuatayo:-

(a)  Muundo wa kipande kimoja (ukwapi)

Huu ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na kipande kimoja tu.  Mifano ya mashairi ya muundo wa kipande kimoja katika diwani hii ni “Maendeleo ya uma” (uk.2-4),  “Pungo”, “Viongozi wa Afrika” ,“Wengine” , “Wizi”,“Kunguru”,  “Utawala” ,“Njama” ,“Wingu” ,“Si Wewe?” , “Siku Itafika”,“Naona”,  “Kinyang’anyiro”  na “Joka la Mdimuni”.Kwa mfano katika shairi la “Kunguru”, mshairi anasema:-

 

 

“Kunguru wakabadilika,  

Uchafu wao wakaweka, 

Maradhi yakaongezeka, 

Nibadala ya kutoweka”

 

(b)Muundo wa vipande viwili (ukwapi na utao)

Huu ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na vipande viwili, yaani kipande cha kwanza (ukwapi) na kipande cha pili (utao).Mifano ya mashairi ya muundo wa vipande viwili katika diwani hii ni “Fungate”,”Nataka Kusema” , “Nyayo”,  “Kuntu Sauti ya Kiza” ,  “Ni Vita Si Lelemama”,  “Ladha ya Maji Katani”  “Mcheza Hawi Kiwete” , “Sakubimbi”, “Paka Shume”, “Wewe Peke Yako” ,“Nia yangu Sigeuzi”, “U Wapi Uzuri Wako” na “Ua Si Ruwaza Njema”.Kwa mfano katika shairi la “Ua Si Ruwaza Njema”. mshairi anasema:

 

“Ua tunzo ya mahaba, wapenzi wanahusika,  

Ishara ya usuhuba, wawili kukutanika,  

Lakini na makahaba, na wao hujipachika,   

Ua si ruwaza njema, tunzo ya mtu kupewa”.

 

(c)  Muundo wa vipande vitatu (ukwapi, utao na mwandamizi).

Huu ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstari) wa ubeti wa shairi kunakuwa na vipande vitatu, yaani kipande cha kwanza (ukwapi), kipande cha pili (utao) na kipande cha tatu (mwandamizi).  Mifano ya mashairi ya muundo wa vipande vitatu katika diwani hii ni “Dafina”  (uk.8-10)  “Mkata” (uk.19-20) na “Mja wa Mungu”  (uk.27).  Kwa mfano, katika shairi la  “Mja wa Mungu”  (uk.27). Mshairi anasema:

 

 

“Duniani,ni maradhi ni masikani, mafakiri,  

Lakini, dawa tele kabatini, mabepari, 

Abadani, hawa si waja wa Mungu!”!.

 

(d)  Muundo wa vipande vinne

Huu ni muundo ambao kwa kila mshororo (mstai) wa ubeti wa shairi kunakuwa na vipande vinne.  Mifano ya mashairi ya muundo wa viipande vine katika diwani hii ni “Ruya”  (uk.13-14) na “Gorila” (uk.14-15).  Kwa mfano katika shairi la “Gorila” (uk.14-15), mshairi anasema:

“Gorila, jasiri!  

Wa Afrika, wavuka, mingi mito, yenye hatari,  

Wa panda shuka, inuka, na uzito, wa lako gobori, 

Gorila, ruwaza wa kizazi kipya”.

 

Ø Kigezo cha aina ya vituo:

Kwa kuzingatia kigezo cha aina ya vituo, mwandishi wa diwani ya FUNGATE YA UHURU ametumia miundo ifuatayo:-

(a)  Muundo wa kituo bahari

Kituo bahari ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao hujirudia kwa kila ubeti.Mashairi yaliyotumia muundo wa kituo bahari katika diwani hii ni “Dafina”, “Ningekuwa na Sauti”, “Gorila,”Waja wa Mungu”  “Mcheza Hawi Kiwete”,“Njama”,“Ladha ya Maji Katani”,“Kinyang’anyiri”  na “Ua Si Ruwaza Njema” .

 

Katika shairi la “Ua SiRuwaza Njema”  (uk.47-48), mshairi anasema:

“Ua tunzo ya mahaba,  wapenzi wanahusika,  

Ishara ya usuhuba, wawili kukutanika,  

Lakini na makahaba, na wao hujipachika, 

Ua si ruwaza njem, tunzo ya mtu kupewa

 

Ua likiwa mtini, hua linanawirika,  

Huwa na kubwa thamani, hapo lilipojishika,

 Likitiwa mikononi, si muda linanyauka, 

Ua si ruwaza njem, tunzo ya mtu kupewa”.

                                 

(b)  Muundo wa kituo nusu bahari

Kituo nusu bahari ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao sehemu tu ha mshororo (mstari) hujirudia kwa kila ubeti wa shairi.  Mara nyingi katika kituo nusu bahari, kipande kimoja tu cha mshororo wa mwisho wa ubeti hurudiwa katika beti za mashairi. Mashairi yaliyotumia muundo wa kituo nusu bahari katika diwani hii ni ”Kuntu Sauti ya Kiza”  na  “Si Wewe?”  .

Katika shairi la ”Kuntu Sauti ya Kiza” (uk.33), mshairi anasema:

“Si mlaji wa vinyesi, mizoga na masalia, 

Hayarambi makamasi,na banguzi kubugia, 

Hata samaki wa tasi, shombo analikimbia, 

Kuntu Sauti ya Kiza, nyuki hatwai vichafu.

 

 

 

Nyuki hatui topeni, na zizini kuingia, 

Sijamwona karoni, mikojo kufakamia, 

Haingii na chooni, hata chenye mazulia,  

Kuntu Sauti ya Kiza, nyuki hatwai vichafu”.

 

(c)  Muundo wa kituo kimalizo

Kituo kimalizio ni mstari wa mwisho wa ubeti wa shairi ambao haujirudiirudii kwa kila ubeti.Hii ina maana kuwa kwa kila ubeti wa shairi kunakuwa na mstari wa mwisho (kituo) wa tofauti na usiofanana na beti nyingine.  Mashairi yaliyotumia muundo wa kituo kimalizio katika diwani hii ni “Fungate” , “Unganeni”,“Maendeleo ya Umma”  Nchi yangu, “Nahodha Mtwesi”, “Mjamzito” ,“Nikizipata Bunduki”,  “Ruya”,“Pungo”  (uk.16-18),  “Nataka Kusema”, “Mkata”,“Viongozi wa Afrika”,“Afrika”, “Wengine”,“Wizi” ,“Kunguru” ,“Utawala” ,“Ukasuku”  “Nyayo”,“Ni Vita Si Lelemama” ,“Wingu” ,“Siku Itafika” ,”Joka la Mdimuni’’ na “Naona”.

 

Katika shairi la “Nataka Kusema”  (uk.18), mshairi anasema:

“Nataka kutema mate,   

Mate yanichafuayo,moyo, lakini: 

Yamekauka, jelezi menishika!

 

Nataka, kulia kite,  

Kite, yanikeketayo moyo, wenzangu,  

Hayatatoka, machozi yametweka!”

 

3.  MANDHARI

Mshairi wa diwani ya FUNGATE YA UHURU ametumia mandhari yafuatayo:-

(a)             Mandhari ya bara la Afrika.

Mshairi anazungumzia kero, shida au matatizo mbalimbali yanayolikabili bara la Afrika, ikiwemo nchi ya Tanzania, kupitia mashairi ya “Unganeni” ,“Nikizipata Bunduki” ,“Gorila” ,“Viongozi wa Afrika” ,“Afrika”,“Ni Vita Si Lelemama”  na “Utawala” .Mshairi ametaja baadhi ya nchi za bara la Afrika kama vile Tanzania, Afrika ya Kusini na Namibia.Pia, mshairi ametaja jina la chama cha kisiasa kimojawapo kinachoopatikana nchini Tanzania , Chama cha Mapinduzi, kudhihirisha kwamba yanaoongelewa kwenye diwani yake yanahusu nchi ya Tanzania.Jina hili la chama cha kisiasa limetajwa katika shairi la “Ni Vita Si Lelemama”  (uk.34).  Mandhari ya bara la Afrika yanaibua dhamira za rushwa, umasikini, uonevu, dhuluma, udikteta, uongozi mbaya, unyonyaji, unafiki, usaliti,matabaka, mapinduzi au mageuzi, wizi wa mali ya umma na ushirikiano.

 

(b)  Mandhari ya mabara ya Amerika na Ulaya.

Mshairi anajadili namna nchi zilizoendelea, zikiwemo nchi za bara la Amerika na Ulaya, zinavyonyonya, zinavyoonea na zinauvyokandamiza nchi zinaendelea zzinamiliki uchumi na siasa za nchi zinazoendelea.  Mshairi anatumia mandhari haya katika shairi la “Afrika”.Mandhari ya mabara ya Amerika na Ullaya yanaibua dhamira za ukoloni mamboleo, unyonyaji, umasikini na ukombozi wa kisiasa.

 

(b)             Mandhari mengine yanayotajwa katika diwani hii ni ikulu, kanisani, msikitini, bomani, ofisini, shambani, dukani, gulioni na gengeni.katika shairi la “Wizi” . na mandhari ya nyumbani katika shairi la “Mkata”.  Mandhari yote haya yanaibua dhamira za umasikini, unyonyaji, uongozi mbaya, wizi wa mali ya umma, dhuluma, unafiki, usaliti na matumizi mabaya ya vyombo vya dola

 

C)MATUMIZI YA LUGHA

Mwandishi ametumia lugha sanifu yenye lahaja ya Kiunguja.Lugha hii imejaa misemo mbali mbali,tamathali za semi na taswira.

Misemo

Imetumika kwa wingi.

Mfano:

·        Nahodha mtwesi chombo chenda joshi (uk 5)

·        Waja wa Mungu (uk 20)

·        Paka shume (uk 34)

·        Utakiona cha mtema kuni (uk 24)

·        Joka la mdimuni (uk 31) n.k.

TAMATHALI ZA SEMI

Tashibiha

Mfano shairi la “Mkata” (uk 15):-

·        Kitandani nilalapo kama dema la samaki…

·        Mbu ndani kama ndege wa vitani…

·        Matopeni hujazika mithili nimo karoni…

·        Nimekoni kama ndizi natokota na kufoka

 

Sitiari

Mfano shairi la “Uwapi Uzuri Wako” (uk 35)

·        Sasa ni chano cha maji, watu wajichanyatia

·        Bao la mkahawani, kila mtu akaliya

·        Sasa jamvi la wageni,wajapo huwapokeya.

Kejeli

·        Shairi la “Fungate” (uk 1) linakejeli tabia za baadhi ya viongozi wetu wanaoendelea kuifaidi Fungate ya Uhuru.

·        Shairi la “Kuntu Sauti ya Kiza” mwandishi anatumia nyuki kukejeli baadhi ya tabia chafu za watu.

Tafsida

Mwandishi ametumia Tafsida kuyasema maneno makali, machafu, matusi.Mfano shairi la “Paka Shume” linajadili suala la kumendea vitu vya watu kwa njia isiyo halali.Hata neno lenyewe fungate ni tafsida.

MBINU NYINGINE ZA KISANAA

Takriri

Katika shairi la “Mkata” (uk 15), “Dafina” pamoja na shairi la “Nchi Yangu”baadhi ya maneno yamerudiwa sana.

Mjalizo

Katika shairi la “Mkata” (uk 15).

Mdokezo

Katika shairi la “Mwinyi Mpe Ndiyo”

 

UJENZI WA TASWIRA

·        Neno Fungate linaleta taswira ya ulimbwende wa maharusi linaashiria  viongozi.

·        Shairi la “Mjamzito” (uk 5) linajenga taswira ya viongozi waoga katika jamii. Viongozi wasioweza kutatua matatizo ya wananchi.

·        Shairi la “Paka Shume(uk 34) linajenga taswira ya udokozi.

·        Shairi la “Viongozi wa Afrika”(uk 15) linajenga taswira ya viongozi wanaotumia madaraka  vibaya.

 

JINA LA KITABU

Kwa ujumla jina la kitabu Fungate ya Uhuru linasadifu  yale yaliyomo ndani ya kitabu.Mwandishi  ameonesha jinsi viongozi wetu walivyo kwenye fungate ya Uhuru.Hali kadhalika wananchi bado wanaendelea kugharamia sherehe mbali mbali za viongozi kwa njia ya michango kama vile kodi,mchango wa mwenge, n.k.

 

KUFAULU KWA MWANDISHI

Kimaudhui

v Mwandishi amefaulu Kuonesha matatizo mbali mbali ya jamii zetu na mbinu za kuyaondoa/kuyatatua matatizo hayo.

Kutofaulu kwa Mwandishi

v Mashairi mengi yanahusu  siasa na hivyo kuwa kama mahubiri ya kisiasa.

v Amesisitiza mfumo wa chama kimoja badala ya mfumo wa mageuzi  na kitabu hiki kiliandikwa wakati mfumo wa mageuzi umepamba moto dunia nzima.

v Kumfanyia Mwinyi kampeni ni udhaifu,hii ni kutokana na ukweli kuwa Rais Mwinyi hakuweza kuondoa matatizo aliyoyajadili na ndiyo maana hadi sasa yapo.

v Amekemea uongozi mbaya,lakini hakuonesha chanzo cha uongozi mbaya na mbinu mbali mbali za kuwapata viongozi bora hapa nchini.

v Kutumia lahaja ya Kiunguja ni udhaifu mwingine wa mwandishi,kwani anakinyima Kiswahili sanifu uwanja wa kukua na kuenea

 

 

Powered by Blogger.