Ushahidi upande wa mashtaka kesi ya Ponda wafungwa

Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda akisalimiana na mkewe kabla ya kuanza kusikilizwa kwa kesi yake katika Mahakama ya Hakimu  Mkazi Morogoro,  jana. Picha  na Juma Mtanda
ADVERTISEMENT
Morogoro. Upande wa mashtaka katika kesi ya jinai inayomkabili Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda, umefunga ushahidi wao baada ya kupeleka mashahidi tisa.Shahidi wa mwisho wa upande wa mashtaka askari E.9295 D/CPL, Juma Koroto kutoka Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai(RCO), Morogoro ambaye alikuwa mpelelezi wa kesi hiyo.
Akiongozwa jana na Wakili wa Serikali, Benard Kongola katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, shahidi huyo alidai kuwa Agosti 11, 2013 alipokea jalada la kosa la uchochezi lenye namba Moro/IR/ 4473 /2013 lililomtuhumu Sheikh Ponda kutoa maneno ya uchochezi Agosti 10 mwaka 2013.
Shahidi huyo alidai kuwa Agosti 19, 2013 mshtakiwa huyo alifikishwa mahakamani hapo kujibu mashtaka yote matatu yanayomkabili.
Upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili Juma Nasoro ulimuuliza shahidi huyo maswali ya msingi ikiwa ni pamoja na kutaka kujua kama Sheikh Ponda alihojiwa baada ya kukamatwa na nani ni mlalamikaji sahihi katika kesi hiyo.
Akijibu maswali hayo, shahidi huyo alidai kuwa hakuwahi kumuhoji mshtakiwa kutokana na kushindikana kukamatwa katika eneo la tukio.
Alisema hata alipokamatwa baadaye, mshtakiwa alikataa kuhojiwa mkoani Morogoro.
Mahakama ilielezwa kuwa mlalamikaji ni Jafert Kibona aliyekuwa RCO kwa wakati huo, lakini kesi hiyo ipo chini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mary Moyo alihairisha kesi hiyo hadi Machi 9 kwa ajili ya kuanza kusikiliza upande wa utetezi.
Powered by Blogger.