Chadema Mbeya yasema mwisho wa CCM Oktoba


Mbunge wa Mbeya mjini Joseph Mbilinyi
Mbeya. Mwenyekiti wa Chadema mkoani hapa, Joseph Mwachembe maarufu kwa jina la China amesema chama chake hakina ndoto ya kuwapo kwa serikali ya mseto awamu ya tano ya uongozi wa nchi, kwa vile kimejiandaa kushinda kuanzia ngazi ya urais, ubunge hadi udiwani .
China alisema Chadema inaamini kwa niaba ya Watanzania kwamba mwisho wa utawala wa CCM ni Oktoba mwaka huu, hoja za baadhi ya watu kwamba CCM ikikosa wabunge wengi ikubali kuunda serikali ya mseto ni propaganda za wafuasi wa CCM.
Alitoa kauli hiyo alipoulizwa maoni ya chama chake kuhusu taarifa kwamba upinzani watapata wabunge wengi, lakini rais atatoka CCM katika uchaguzi ujao na kuishauri CCM ijiandae kuunda serikali ya mseto.
Hivi karibuni mwanasiasa mstaafu Kanali Edmund Mjengwa (68) aliishauri CCM iwe na mawazo ya kujiandaa kuunda serikali ya mseto ikiwa rais atatoka CCM na wabunge wengi ndani ya Bunge wakawa ni wa upinzani.
Naye Mbunge wa zamani wa Musoma Vijijini, Paul Ndobho alitoa kauli kama hiyo alipozungumza na mwandishi wetu Kanda ya Ziwa.
Akifafanua hoja zake jana, China aliwasihi Watanzania kushika moja la kuwachagua wagombea wa chama kuanzia rais hadi madiwani ili kuundwa kwa serikali itakayofanya kazi kwa uhakika zaidi .
Alisisitiza kwamba Chadema itashinda kwa wingi viti vya udiwani, ubunge na urais na kwamba hawana ndoto za kuwapo kwa mseto.
Naye Mwenyekiti wa CUF mkoani hapa Yassin Mrotwa akitoa maoni yake alisema CUF ina uhakika kwamba CCM imefika kikomo kwa sababu Watanzania wamechoshwa na ufisadi uliopo serikalini.
Wafanyakazi wamechoshwa na kukopwa fedha zao kupitia mishahara hata mifuko ya hifadhi, wakulima wamechoshwa kukopwa mahindi na mpunga,” alisema na kuongeza: “Kibaya zaidi ni kwamba CCM haina mgombea safi na makini.”
ADVERTISEMENT
Mrotwa alisema mazingira ya chama chake kushinda urais ni makubwa kuliko hesabu za wabunge na madiwani na kwamba kinachotakiwa ni CCM kujiandaa kukabidhi madaraka kwa utulivu.
Kuhusu maoni ya kuwapo kwa serikali ya mseto, alisema haiwezekani kwa vile katiba iliyopo na hata inayopendekezwa haijaruhusu kuwapo kwa serikali ya aina hiyo. Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM mkoani Mbeya, Bashiru Madodi alipoulizwa maoni yake kuhusu suala hilo alisema chama chake hakina ndoto ya kuwapo kwa serikali ya mseto kwani kitapata ushindi wa kishindo kuanzia madiwani, wabunge hadi rais.
Madodi alisema CCM imejipanga kuwakata ngebe wapinzani kwa kuwapoka baadhi ya majimbo na kwamba imejipanga haina wasiwasi.
“Kwa CCM kufikiria kuunda serikali ya mseto hiyo haitatokea ni ndoto za wachache’’ alisema.
Naye mchambuzi wa masuala ya siasa, Dk Stephen Mwakajumulo alipouulizwa kuhusu suala hilo alisema pamoja na kukua kwa demokrasia, CCM ikijipanga kwa kuteua wagombea wanaopendwa na wananchi itapata wabunge wengi kuliko wa upinzani.
“Lakini CCM itaingia mkenge kama itawateua wagombea watakaopendwa na wapiga kura za maoni badala ya wananchi wengi, lakini ikiwateua wapendwa wa wananchi itashinda majimbo na kata nyingi sana,’’ alisema. Alisema serikali ya mseto kwa CCM haitakuwapo mwaka ujao kwa vile upo uhakika wa CCM kushinda sana wagombea wake.
Lakini Mwenyekiti wa Chama cha APPT –Maendeleo mkoani hapa, Godfrey Davis alisema mawazo ya serikali ya mseto ni mazuri na changamoto kwa vyama vya siasa kuweka mazingira mazuri ya kudumisha amani ya nchi.
Davis alisema serikali ya mseto ni nzuri katika nchi za kidemokrasia na kwamba ndiyo maana hivi sasa waziri mkuu anapigiwa kura na wabunge ya kukubalika.
Alisema kama Serikali ya mseto haitakuwapo upo uwezekano wa kuchafua nchi kwa vile wabunge wanaweza kupiga kura ya kutokuwa na imani na rais au waziri mkuu mara tatu jambo ambalo rais anaweza kulivunja bunge.
Powered by Blogger.