Moto mwingine waleta hasara Dar na Mwanza

engo lililopo Mtaa wa Libya na Mosque likiwaka moto jijini, Dar es Salaam jana. Picha na Said Khamis
Dar es Salaam / Mwanza. Siku nne baada ya kuungua kwa nyumba iliyosababisha vifo vya watu sita wa familia moja, Dar es Salaam, moto mwingine umeteketeza sehemu ya juu ya jengo la ghorofa mbili la Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) lililopo katikati ya jiji.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova, alisema hakuna mtu aliyefariki wala kujeruhiwa katika tukio hilo lililotokea kwenye makutano ya Mitaa ya Libya na Mosque, Wilaya ya Ilala.
Kamanda Kova alisema Polisi walipata taarifa jana saa 5.30 asubuhi kuwa kunguru ndio walisababisha hitilafu ya umeme na jengo hilo kushika moto na kutekekeza mali ambazo thamani yake haijafahamika.
Alisema moto huo ulioanza taratibu na kuongezeka ghafla kutokana na mitungi ya gesi iliyokuwamo kwenye jengo hilo.
Meneja wa NHC Mkoa wa Dar es Salaam, Jackson Maagi alisema jengo hilo lilikuwa na familia zaidi ya 10 na kwamba shirika hilo litahakikisha kuwa waathirika wanapatiwa nyumba za kuishi wakati utaratibu mwingine ukiendelea kufanyika. 
“Tungekuwa sisi ni chanzo cha tukio hilo tungesema tuwafidie lakini kwa kuwa sisi siyo chanzo, tutawapa nyumba kwa ajili ya kujihifadhi, labda pengine chanzo halisi kitakapopatikana ndipo tutajua tufanye nini,” alisema Maagi.
Hata hivyo, mmoja wa wakazi katika jengo hilo, Ahlim Abdullah alisema jengo hilo lilikuwa na familia nne katika ghorofa ya kwanza na ofisi kadhaa katika ghorofa ya pili iliyoteketea kwa moto.
Akizungumzia chanzo cha moto huo, alisema: “Waliokuwa nje wanasema walimwona kunguru akisababisha shoti na moto kuanza kusambaa.”
Kamanda wa Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jeswald Nkongo alisema baada ya kupewa taarifa kuwa kuna moto, walituma gari la kwanza kwa ajili ya kufanya tathmini ya ukubwa wa moto ndipo walipobaini kuwa ulikuwa mkubwa na tayari ulikuwa umeshaanza kusambaa.
Wananchi walalamika
Baadhi ya wananchi waliofika mapema katika eneo hilo walikitupia lawama Kikosi cha Zimamoto kwa kufika mapema lakini kilichelewa kuanza kuuzima moto kwa sababu ambazo hazikufahamika.
“Jengo limeanza kuungua limekuja gari likiwa na maji kidogo, wamekaa muda mrefu hawajui wafanye nini hadi tulipoanza kusaidia kuwatoa watu waliokuwa ndani.
Kama wangekuwa na miundombinu mizuri jengo hili lisingeungua kiasi hiki, Serikali ina mbinu za kukamata Wamachinga,” alisema mmoja wa wananchi waliokuwapo katika tukio hilo, Selemani Vitus.
Shuhuda mwingine wa tukio hilo, Abubakar Ali alisema hasara hiyo ingeweza kudhitibiwa iwapo Serikali ingekuwa na vifaa vya kisasa vinavyowezesha watu kuzima moto kwenye majengo marefu.
Ilivyokuwa
Wakati mwandishi wa habari hii alipokuwa akiwasili katika eneo la tukio, alishuhudia moshi mkubwa ukitoka ndani ya jengo hilo sehemu ya juu huku polisi wakiweka uzio kuzuia mamia ya watu waliokuwa wakisogea karibu.
Ghafla moto huo uliongeza kasi na kuezua mabati upande mmoja wa jengo hilo, jambo lililowalazimisha askari kuwataka watu waliokuwa kwenye majengo ya karibu kuondoka.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, watu wawili waliokuwa katika jengo la jirani walikuwa wakikataa kutoka huku wakikitaka Kikosi cha Zimamoto kuhakikisha kuwa moto huo haufiki mahali walipo. Hata hivyo, askari waliingia katika jengo hilo na kuwatoa.
18 wanusurika Mwanza
Watu 18 wamenusurika baada ya moto kuteketeza nyumba moja na maduka katika Mtaa wa Igoma Magharibi B, Kata ya Igoma jijini Mwanza na kusababisha hasara ya zaidi ya Sh50 milioni.
Moto huo ulioanza jana saa 11.00 alfajiri, uliteketeza nyumba ya Fares Peter iliyokuwa na watu wanne na duka la Raphael Lukigwa likiwa na bidhaa mbalimbali.
Akizungumza kwenye eneo la tukio jana, Lukigwa alisema chanzo cha mto huo ni hitilafu ya umeme na kwamba uliteketeza nyumba na duka lote.
Mkazi wa Mtaa wa Igoma Magharibi, Mussa Iddi alisema: “Umeme ndiyo chanzo kwani miundombinu iliyopo hapa siyo bora. Tunaomba Tanesco iboreshe miundombinu ya usambazaji.”
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Igoma Magharibi, Edwin Shija alisema hakuna kifo kilichotokea.
Imeandikwa na Raymond Kaminyonge, Kalunde Jamal na Beatrice Moses, Goodluck Eliona na Aidan Mhando, Mwananchi.
-
Powered by Blogger.