Mabilioni yahitajika kunusuru homa ya bonde la ufa


“Haya ni magonjwa hatari kwa binadamu na mifugo, tuliomba tangu Novemba lakini bado hatujapata, tukichelewa kufanya chanjo mifugo yetu ipo hatarini,” alisema Telele.
Dar es Salaam. Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi imeomba Sh30.2 bilioni Hazina kwa ajili ya chanjo ya ugonjwa wa bonde la ufa ambao ni hatari kwa binadamu na wanyama.
Wizara hiyo imesema ugonjwa huo ambao ulikuwa tishio mwaka 2006/07 hujirudia kila baada ya miaka mitano na unaweza kutokea mwaka huu kama mvua kubwa zitanyesha.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk Titus Kamani alithibitisha wizara hiyo kuomba fedha hiyo ili kuendesha chanjo za magonjwa manne ya mifugo lakini bado Hazina haijawapatia.
Magonjwa mengine ni homa ya mapafu ya ng’ombe, magonjwa ya miguu na midomo na sotoka kwa mbuzi.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Kaika Saning’o Telele naye alithibitisha wizara hiyo kuomba Sh30 bilioni kwa ajili ya kufanya chanjo nchi nzima.
“Haya ni magonjwa hatari kwa binadamu na mifugo, tuliomba tangu Novemba lakini bado hatujapata, tukichelewa kufanya chanjo mifugo yetu ipo hatarini,” alisema Telele.
Habari za uhakika kutoka wizarani hapo zinasema wizara hiyo iliomba fedha hiyo kupitia barua ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Yohana Budela yenye kumbukumbu namba PD/185/471/01/07 ya Novemba 10, 2014.
“Kuna uwezekano wa kutokea mlipuko wa Homa ya Bonde la Ufa katika msimu wa mvua za masika zinazotarajia kuanza mwishoni mwa Februari,” ilisema sehemu ya barua hiyo.
Hata hivyo, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na Naibu wake, Mwigulu Nchemba walipotafutwa kuzungumzia suala hilo, simu zao zilikuwa zikiita bila ya kupokelewa.
Katika maombi hayo kwa Katibu Mkuu, wizara ilisema ugonjwa wa homa ya bonde la ufa ni hatari kwa mifugo na binadamu umekuwa na tabia ya kujirudia kila baada ya miaka mitano na mara ya mwisho ulitokea mwaka 2006/07.
Takwimu za wizara hiyo zinaonyesha kwamba Tanzania ina ng’ombe milioni 22.8, mbuzi milioni 18 na kondoo milioni 7 na kwamba mifugo hiyo iko katika hatari ya kupata magonjwa hayo.
Kuhusu homa ya mapafu ya ng’ombe inaelezwa na Katibu Mkuu kwamba wilaya 45 zimethitishwa kuwa na maambukizi na kwamba ng’ombe milioni 15 wako katika hatari ya kupata maambukizi ya ugonjwa huo.
Pia, ugonjwa wa miguu na midomo nao tayari umeripotiwa kuwapo kwenye mikoa 16 ya Tanzania Bara na ng’ombe 513,867 wameshapata maambukizi. Ng’ombe milioni 11 wako katika hatari ya kuambukizwa kama chanjo haitapatikana mapema.
Kuwapo kwa ugonjwa huo kutasababisha biashara ya mifugo na mazao yake kwenda nje ya nchi usitishwe.
Pia, ugonjwa wa sotoka ya mbuzi unaendelea kusambaa. Hadi sasa ugonjwa huo umeripotiwa kwenye wilaya 33 na mbuzi milioni 10 wako katika hatari ya kuambukizwa.
Ugonjwa wa kichaa cha mbwa unaendelea kusambaa kwa kasi katika wilaya zote.
Takwimu kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii zinaonyesha kuwa watu wengi wanapata maambukizi kutokana na kuumwa na mbwa ambao tayari wameshaambukizwa.
Idadi ya mbwa walio katika hatari ya kupata maambukizi hayo ni kati ya milioni 3.5 hadi milioni 4.
Njia kuu ya kuzuia kuenea na kusambaa kwa maambukizi ya magonjwa hayo ni kuchanja mifugo yote kwa wakati. Alisema magonjwa manne yaliyoanishwa ukiacha ugonjwa wa miguu na midomo, yapo kwenye orodha ya magonjwa ambayo yameorodheshwa kama majanga kwa kitaifa.
“Ni wajibu wa Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi kuagiza chanjo hizo mapema iwezekanavyo na kuzisambaza kwenye wilaya zote na kisha kusimamia shughuli za uchanjaji wa mifugo yote iliyo kwenye hatari ya kupata maambukizi.
Powered by Blogger.