Rais Kikwete akubali utendaji wa Chadema Manispaa ya Moshi

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt.Ramadhan Dau pamoja na wadau wengine wakitazama ramani ya jengo jipya la kitega uchumi la NSSF mjini Moshi Kilimanjaro Commercial Complex wakati wa hafla ya ufunguzi. Picha na Ikulu
Moshi. Rais Jakaya Kikwete, amempongeza Meya wa Manispaa ya Moshi, Jaffar Michael kwa kile alichosema ni kusimamia vizuri na kutekeleza  Ilani ya CCM katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Kauli hiyo ya Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa CCM ni nadra sana kutolewa na kiongozi wa CCM, akipongeza utendaji mzuri wa viongozi wanaotoka vyama vya upinzani.
Meya huyo anatokana na chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambacho ndicho kinachoongoza Baraza la Madiwani kwa kuwa na theluthi mbili ya madiwani wote wa Halmashauri.
Rais Kikwete alitoa pongezi hizo juzi wakati akifungua jengo la kisasa la kibiashara lililojengwa katikati ya mji wa Moshi na Shirika la Mfuko wa Hifadhi za Jamii (NSSF) kwa gharama ya Sh64 bilioni.
 “Hata Mstahiki Meya nakupongeza kwa sababu nyinyi hamna Serikali sisi (CCM) ndio wenye Serikali,”alisema Rais Kikwete huku akicheka kwa furaha na kuongeza kusema;
“Kwa hiyo tunawashukuru kwa utekelezaji mzuri wa ilani ya CCM na kwa sababu mnatekeleza vizuri, tutaendelea kuwapeni pesa ya kuhudumia wananchi wa Tanzania,” alisema Rais Kikwete.
Rais Kikwete alitumia tukio hilo kuuagiza mkoa wa Kilimanjaro, kutenga maeneo ya uwekezaji na kumtaka Meya huyo awe ni Meya wa maendeleo kwa kutengeneza mazingira rafiki ya uwekezaji.
Powered by Blogger.