Wizara ya Nishati yaahidi kusimamia ushindani wa haki


Dar es Salaam. Serikali imesema itasimamia ushindani wa kibiashara wa haki na kutengeneza mazingira wezeshi kwa waagizaji wa mafuta nchini ili kuhakikisha kuwa wafanyabiashara hao wananufaika na biashara hiyo.
Akifungua semina ya waagizaji wa mafuta iliyofanyika jana, jijini hapa, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage alisema wizara yake kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati, Maji na Mafuta (Ewura) itazingatia ubora wa bidhaa na gharama nafuu za uagizaji wa mafuta.
Mwijage aliongeza kuwa sasa ni wakati ambao waagizaji wanahitaji kwenda kwenye mfumo wa kuwa na mlipaji mmoja wa mafuta yanayoagizwa, tofauti na mfumo uliopo sasa wa kuagiza pamoja lakini kila mmoja analipa peke yake.
“Pia, itaondoa usumbufu kwao kuanza kumfuatilia mfanyabiashara mmoja mmoja,” alisema Mwijage na kuipongeza Benki ya FNB kwa kudhamini semina hiyo muhimu.
Aliwataka wadau waliohudhuria semina hiyo kuanza pia kusomesha wataalamu wazawa ili waweze kufanya kazi katika sekta ya gesi na mafuta.
Alisema Watanzania watatakiwa kujaza nafasi za kazi zinazopatikana nchini na siyo watu wa nje.
“... inahitaji mafunzo ili kuinua uelewa wa watu juu ya suala la kuomba mikopo na dhamana,” alisisitiza Waziri Mwijage.
Meneja Mkuu wa Umoja wa Waagizaji wa Mafuta nchini (PIC), Michael Mjinja alisema semina hiyo inalenga kuwaleta pamoja waagizaji wote wa mafuta zaidi ya 40 ili kuangalia uwezekano wa kulipa kwa pamoja.
Aliongeza kuwa sekta ya mafuta ni sekta ambayo ina watumiaji wengi hivyo wanajaribu kuweka nguvu zaidi ili wadhaminiwe na benki.
Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa FNB, Dave Aitken alibainisha kuwa katika kipindi cha miaka mitano tangu kuanzishwa kwa benki hiyo, ajenda yao imekuwa ni kusaidia watu kwa kuwajengea uwezo.
Alisema benki hiyo ambayo ndiyo pekee Afrika inayofanya kazi India, imeanzisha warsha ya kutoa mafunzo kwa waagizaji wa mafuta kwa sababu ndiyo wadau wao muhimu.
Aliwataka wadau wa mafuta kushirikiana na benki yake katika kutengeza fursa.
Powered by Blogger.