Makada CCM wamvaa JK


Aliyekuwa Mwenyekitiwa CCM Mkoawa Dar es Salaam John, Guninita akizungumza na wandishi wahabari, Dar es Salaam jana kuhusiana na kutaka kumshitaki Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda. Picha na Said Khamis
Dar es Salaam. Makada wawili wa CCM wamemuomba Rais Jakaya Kikwete kuhakikisha kabla ya Uchaguzi Mkuu, anaondoa makundi ndani ya chama hicho, ambacho kinakabiliwa na kazi ngumu ya kumpata mgombea wake bila ya kutokea mpasuko.
Kauli hiyo, ilitolewa jana na wenyekiti wa wa zamani wa chama hicho wa Dar es Salaam, John Guninita na Mgana Msindai wa Singida walipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mambo mbalimbali ya kisiasa.
Wenyeviti hao wa zamani walitishia kumpeleka mahakamani mkuu mpya wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda kwa madai kuwa amekuwa akiwadhalilisha kwa kuwaita vibaraka wa kada mwingine wa CCM, Edward Lowassa katika mikutano yake na waandishi wa habari.
Tayari wameshamuandikia barua ya kusudio la kumfungulia mashtaka iwapo hataomba radhi kwa vitendo hivyo, lakini Makonda aliwajibu kuwa alitoa maneno hayo kwa niaba ya chama na kwamba aliyetakiwa kufungua kesi ni Lowassa.
Jana kwenye mkutano na waandishi wa habari, Guninita, ambaye alisema mwenyekiti mwenzake alikuwa na udhuru, alidai kuwa katika kipindi cha hivi karibuni chama hicho kimekumbwa na changamoto ambazo zinatakiwa kutafutiwa ufumbuzi haraka kutokana na baadhi ya viongozi kutokuwa na uchungu na kutotetea chama hicho kwa ajili ya kukijenga.
“Mwenyekiti wa chama, Rais Kikwete kwa kutumia uzoefu anaoufanya wa kutafuta maridhiano katika nchi mbalimbali za Afrika, atumie uzoefu huo kuondoa mpasuko ndani ya chama chetu,” alisema Guninita.
“Hivi sasa chama kinapotea, kila mtu anafanya anavyotaka. Chama cha miaka ya nyuma si cha sasa, viongozi tulikuwa tukiandika barua za malalamiko na yalikuwa yanashughulikiwa, lakini hivi sasa hata ukiandika hakuna anayekusikiliza wala kukujibu.”
Hata hivyo, katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipotafutwa kuzungumzia tuhuma hizo haikupatikana.
ADVERTISEMENT
Akizungumzia kukashifiwa kwao na makonda, ambaye pia ni katibu wa hamasa wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Guninita alisema: “Licha ya kumtaka atuombe radhi, amekataa sasa tumepanga kwenda mahakamani.
“Mimi siwezi kutukanwa na kijana mdogo, nimekuwa mkuu wa wilaya miaka 25 iliyopita, nimekuwa mwenyekiti wa UVCCM kwa miaka kumi... UVCCM ni sehemu ya kuwapika vijana kuja kuwa viongozi, lakini sasa imekuwa sehemu ya kuzalisha watu wanaopiga viongozi.”
“Taratibu za kuwasiliana na mawakili wangu zimekamilika na Jumatatu tunatarajia kwenda mahakamani kwani alichotufanyia Makonda hatuwezi kukiacha hivi hivi,” aliongeza
Guninita alisema: “Eti Makonda ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya, Rais ana uhuru wa kuteua lakini hapa niseme tu kuwa wanaomshauri walikosea kabisa kama mtu anateuliwa kwa kumpiga mtu tena kiongozi mkubwa serikali iliyopita ni jambo la hatari.”
Makonda alionekana kumfanyia fujo mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba katika kongamano la kujadili Katiba Inayopendekezwa lililofanyika kwenye hoteli ya Blue Pearl jijini Dar es salaam.
Hata hivyo, Makonda alipoulizwa kuhusu uamuzi wa makada hao alisema: “Siwezi kuzungumzia kitu ambacho hakinihusu. Mimi niulizie wananchi wa Dar es Salaam wanapataje maji, migogoro ya ardhi inakwisha vipi na matatizo ya machinga yatakwisha vipi.”
Aliongeza kusema: “Hata kesho (leo) nitakuwa na ziara ya kutembelea ujenzi wa maabara kwa shule mbili hivi maeneo ya Manzese kwani unaweza kusema ujenzi umekamilika kumbe bado.”
Mwaka jana, Makonda aliwatuhumu makada hao kuwa ni wahaini, waongo na wazandiki na kusema kama nia yao ni kusaka urais kwa ajili ya mtu fulani basi watambue kuwa mtu huyo amekosa sifa za katika uchaguzi mkuu wa mwakani.
Powered by Blogger.