Kuanguka kwa Mugabe kwageuzwa utani


Baada ya Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe kuteleza na kuanguka katika Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Harare, watu wengi duniani wamechukulia kitendo cha kuanguka kwa rais huyo kama staili ya kutembea wakiwa na lengo la kumdhihaki.
Katika nchi mbalimbali za Afrika na Ulaya watu wamekuwa wakitembea kama vile wanataka kuanguka wakimuigiza Rais Mugabe. Rais Mugabe ambaye ameiongoza nchi hiyo tangu mwaka 1980, alizaliwa Februari 21, 1924, ambapo mwezi huu atatimiza umri wa miaka 91.
Picha mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha Mugabe akishiriki shughuli mbalimbali, lakini kwa stahili kama alivyoanguka uwanja wa ndege.
Kutokana na picha zilizotengenezwa kusambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii, rais huyo aliagiza picha hizo zifutwe kwakuwa hazina maana.
Baadhi ya picha za Mugabe kwenye mitandao ya kijamii, zinaonekana akikimbizwa na polisi, nyingine akiteleza kwenye barafu na akishangilia mchezo wa kriketi uwanjani.
Picha zake kila mtu alizitumia kwa namna alivyoona inafaa kwani watu wengine walizitengeneza na kuonyesha kwamba anacheza muziki.
Moja ya picha iliyoonekana kuwavutia watu wengi ni ile iliyotengenezwa na kuwekwa kwenye moja ya picha Hussein Bolt akiwa anachomoka kwenye mbio za mita 100, huku akiwa sambasamba na mkimbiaji huyo maarufu duniani.
Pia, picha nyingine ambayo ilionekana kuwavuta watu wengi na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii ni ile Mugabe anaonekana akikimbizwa na kiboko katika moja ya mbuga za wanyama za Afrika.
Rais huyo alianguka hivi karibuni kwenye uwanja huo wakati akirejea Zimbabwe akitoka Ethiopia ambako alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), akichukua nafasi ya Rais wa Mauritania, Mohamed Ould Abdel Aziz.
Mugabe alianguka kwa bahati mbaya wakati akijiandaa kuingia kwenye gari yake kuelekea Ikulu mjini Harare.
Baada ya kuanguka chini, rais huyo alisaidiwa na wasaidizi wake ambao walimuinua na kundelea na ratiba yake kama kawaida.
Kutokana na tukio hilo, vyombo vya habari viliripoti kwamba, Ikulu ya nchi hiyo iliwasimamisha kazi walinzi 27 wa Rais Mugabe, kwa kushindwa kuthibiti tukio hilo.
Powered by Blogger.