Ndege ya JWTZ yaanguka, rubani wake ajiokoa kwa parachuti



Ndege ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) baada ya kuanguka katika uwanja wa ndege Mwanza. Picha kwa hisani ya Ray Naluyaga.
Mwanza. Hali ya taharuki ilitanda kwenye Uwanja wa Ndege wa Mwanza baada ya ndege ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuanguka na kuteketea kwa moto.
Ndege hiyo ambayo ilidaiwa kuwa ni ya kivita na ilikuwa mpya ilianguka saa mbili asubuhi na kuteketea kwa moto, huku rubani wake akinusulika kifo baada ya kuruka kutoka angani kwa kutumia parachuti.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatika uwanjani hapo zilidai kuwa ndege hiyo ilikuwa inaongozwa na rubani ,Peter Augustino Lyamunda.
Waandishi wa habari mkoani hapa walifika kwenye uwanya huo muda mfupi baada ya kutokea kwa ajali hiyo, ambapo baadhi ya maofisa wa JWTZ walikataza wanahabari wasipige picha wala kuripoti kitu chochote kuhusu ajali hiyo.
Kutokana na kuzuiliwa kwa waandishi wa habari, hakuna taarifa yoyote iliyotolewa kuhusu ajali hiyo. Gazeti hili jana lilimtafuta Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Esther Madale hakupatikana, lakini baadhi ya maofisa wa uwanja huho ambao hawakutaja majina yao walidai kuwa suala hilo linahusu mamlaka nyingine, na wao hawawezi kulizungumzia.
Hata hivyo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo naye alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo hakuweza kupatikani kwa kuwa alikuwa kwenye kongamano la viongozi wa dini.
Uwanja wa ndege wa Mwanza umekuwa na matukio kaadha ya ajali za ndege ikiwamo ndege kushindwa kuruka kutokana na hitilafu mbalimbali.
Powered by Blogger.