Wajawazito feki washtukiwa BVR Dar

Mkazi wa Mtoni Mtongani jjijini Dar es Salaam, Gathi Kibacho (kushoto) akibonyeza sehemu maalumu katika mashine ya BVR kuchukua alama za vidole alipokuwa akijiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura. Kulia ni Msimamizi wa uandikishaji, Frank Ernest. Picha na Venance Nestory
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa Mkoa wa Dar es Salaam, unaendelea pamoja na kujitokeza kasoro kadhaa, ikiwa na pamoja na baadhi ya watu kutumia mbinu mbalimbali ili kukwepa foleni.
Katika Kituo cha Bwawani Shule, Mtoni Kijichi, wanawake wawili waliojifanya wajawazito, walibainika kufanya udanganyifu huo huku mmoja akiwa tayari amejiandikisha.
Gazeti hili lilishuhudia mzozo huo baada ya wasichana wawili kupitishwa kutokana na hali zao.
Hata hivyo, mmoja wa majirani ambaye anawafahamu, alidokeza kuwa anawafahamu wasichana hao na hawakuwa na wajawazito.
Mmoja alikuwa amekwishajiandikisha na aliwahi kuondoka mapema kabla ya mwenzake aliyekuja kwa staili hiyo na kushtukiwa.
Baada ya mzozo huo, aliondoka taratibu eneo la tukio ndipo baadhi ya watu walipoanza kumkimbiza kubaini iwapo  ni mjauzito au la.
Kuona hivyo, msichana huyo, aliyatoa makaratasi aliyokuwa ameyafunga tumboni mithili ya ujauzito na kuyatupa, huku akikimbia na kutokomea katika vichochoro vya Mitaa ya Mtoni Kijichi.
Mmoja wa wasimamizi wa kituo hicho, alisema kuwa hawana kawaida ya kuwakagua isipokuwa wanachoangalia ni hali za watu wakiwamo wajawazito, walemavu, wazee na wenye watoto wachanga.
Mbali na kasoro hiyo, baadhi ya vituo vya kuandikisha wapigakura vimeongezewa mashine za BVR ili kukabiliana na ongezeko la watu katika vituo hivyo kabla ya kazi hiyo kufungwa Julai 31.
Hata hivyo, bado kuna msongamano mkubwa wa watu katika vituo vingi na kusababisha baadhi yao kupigana kwa waliochukua namba na wale ambao ni wapya.
Vituo kadhaa Jimbo la Temeke vimeonekana kuwa na msongamano mkubwa wa wananchi licha ya kuongezewa mashine.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Mtoni, Kata ya Mtoni, Omary Mateso alisema kadiri siku zinavyokwenda ndivyo kasi ya uandikishaji inavyoongezeka. Alisema siku ya kwanza waliandikisha watu 495 na siku ya pili watu 587.
Mwandishi msaidizi katika Kituo cha Shule ya Msingi Mtoni, Abdallah Luambano alisema kutokana na mwitikio wa wananchi, waliamua kuomba mashine nyingine ili kuongeza ufanisi.
“Changamoto tunayokabiliana nayo ni kuharibika kwa mashine au wakati mwingine kushindwa kusoma alama za vidole vya baadhi ya watu hasa wanawake kutokana na kupaka mafuta mikononi,” alisema.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mbuyuni, Selemani Mpoyo alisema tatizo kubwa lililopo kwenye vituo ni utaratibu unaotumika kuandikisha watu. Alisema jana walikuwa wanaandikisha majina, lakini siku inayofuata watu waliowahi kituoni hawakubali kuanza na majina ya jana.
Katika Kituo cha Shule ya Msingi Kibondemaji, Mbagala, uandikishaji ulikwenda vizuri.
Mwenyekiti wa Mtaa za Zakhem Mbagala, Rajab Masunga alisema walianza na mashine tatu za kuandikisha, lakini kutokana na wingiwa watu wameongezewa nyingine tatu.
Katika kituo cha uandikishaji cha Shule ya Msingi Mbagala, pia mashine ziliongezwa na kuthibitishwa na Mwenyekiti wa Mtaa wa Mbagala, Said Makacha.
Kituo cha Shule ya Msingi Makamba, Temeke mashine pia ziliongezwa sanjari na Kituo cha Shule ya Msingi Makamba, lakini kilielezwa kuwa hakikuwa na utaratibu mzuri wa kuandikisha.
Taharuki kwenye vituo
Baadhi ya wananchi walilazimika kuzipiga kavukavu kutokana na wengine kutaka kuwapita wenzao waliofika vituoni mapema.
Shuhuda wa tukio hilo, Mohamed Hamad alisema watu waliopigana walikuwa wakigombania nafasi ya kuwahi kujiandikisha na polisi walipopata taarifa walifika na kumkamata mmoja.
 Akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina lake, msimamizi wa kata hiyo amekiri kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa mtu huyo alishikiliwa na kuwekwa mahabusu kwa muda na baadaye alichukuliwa kwenda kuandikishwa, kisha akaachiwa huru.
Msimamizi wa mawakala wa Chama cha CUF, Kombo Mhina ameeleza kuwa kuna baadhi ya watu 10 waliokuwa wamebaki jana na wakaandikana majina, lakini leo wamejikuta wako 90, jambo ambalo limesababisha ngumi katika Kituo cha Shule ya Msingi Makumbusho.
Naye Juma Yusufu alieleza kuwa uandikishaji unafanyika kwa kujuana.
Alisema mtu akitoka anamwita mwingine aingie  wakati amechelewa na kuna wakati mtu unakwenda kujiandikisha kitambulisho kinatoka na jina la mtaa wa mbali na unapojiandikishia.
Baadhi ya vituo hali ni shwari licha ya kulalamikiwa kwenda kwa kusuasua katika maeneo ya Tandale, Sinza na Manzese.
Katika Kituo cha Sinza D, idadi ya watu waliojitokeza kujiandikisha ilikuwa si kubwa kama maeneo ya Tandale, lakini malalamiko makubwa yalikuwa katika ufanisi wa mashine za BVR.
Mara kwa mara mashine hizo zimekuwa zikisumbua, hivyo kusababisha watendaji kusimamisha kazi kwa muda ili kufanya matengenezo. Jambo hili limechangia kutuweka kituoni kwa muda mrefu, alifafanua  Rajab Hassan (34), mmoja kati ya watu waliokuwa kwenye foleni hadi saa saba mchana.
Hata hivyo, baada ya kufika  saa moja na nusu asubuhi, mwandikishaji alikana kumtambua na hivyo kulazimika kukaa tena kwenye foleni. Hadi gazeti lilipokuwa likipita kwenye kituo hicho saa saba mchana kijana huyo alikuwa bado hajajiandikisha.
Mkuu  wa Kituo cha Sinza D, ‘A’  Abdallah Amour, akizungumzia tatizo la kusuasua kwa uandishi kunakosababishwa na matatizo ya mashine, alisema kuwa ni kweli kuwa mashine hizo zimekuwa zikipata matatizo, lakini mafundi wao wamekuwa wakizishughulikia.
Mwananchi lilishuhudia misururu mirefu katika maeneo ya Shule ya Tandale Magharibi na Shule ya Mpakani, Manzese karibu na eneo la Mabibo.  Licha ya kutawaliwa na amani, kulikuwa na malalamiko hayohayo ya kwenda taratibu kazi ya uandikishaji kulikosababishwa na kususua  kwa mashine.
Mnyika alonga
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika  ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iongeze mashine za uandikishaji  katika maeneo mbalimbali ili kuendana  na  wingi wa  wananchi waliopo katika mkoa wa Dar es Salaam.
Kauli ya Nec
Mkurugenzi wa NEC, Julius Malaba alisema  jana kuwa suala la mashine kufanya kazi usiku ni kawaida ila lazima watu katika eneo husika wakubaliane.
Kuhusu kuharibika kwa mashine, Malaba alisema timu ya wataalamu wa IT inapita kila kituo  ambacho kimebainika mashine zake kutofanya kazi vzuri na kuzirekebisha.“Hii iliwahi kutokea Arusha, kuna sehemu wadau walikubaliana  na wakaendesha uandikishaji hadi usiku, kuhusu mashine tulishasema tutaziongeza ili kukidhi mahitaji kadiri siku zinavyokwenda na kila mmoja mwenye sifa, ataandikishwa,” alisema.
“Suala la  mashine  kukutwa na majina kabla haijaanza kufanya kazi nitalifuatilia nijue ukweli wake.,” alisema Malaba.
Imeandikwa na Peter Elias, Suzan Mwillo, Emma Kalalu, Maimuna Kubegeya na Colnely Joseph.
Powered by Blogger.