Rais Kikwete apewa Tuzo ya Utawala Bora

Jakaya Kikwete

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete ametunikiwa Tuzo ya Utawala Bora Afrika kwa mwaka 2015 kutokana na jitihada zake za kudumisha na kuimarisha utawala bora nchini.
Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, ilieleza kuwa Rais Kikwete ametunikiwa tuzo hiyo na Taasisi ya African Archievers Awards yenye makao makuu nchini Afrika Kusini.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Kikwete anaungana na Askofu  Desmond Tutu wa Afrika Kusini aliyekuwa wa kwanza kupewa tuzo hiyo mwaka 2011 kutokana na mchango wake wa kutetea haki za binadamu, usawa na amani.
“Rais Kikwete ameteuliwa kutoka miongoni mwa watu 1,202 ambao majina yao yaliwasilishwa kwenye jopo la kimataifa, linalojitegemea na lenye wajumbe kutoka Uingereza na Afrika Kusini kwa ajili ya uteuzi,” ilisema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo iliongeza kuwa, kutokana na tuzo hiyo, Rais Kikwete  amealikwa kwenda kuipokea nchini Afrika Kusini kesho mjini Johannesburg.
Hata hivyo, Rais Kikwete hataweza kwenda kutokana na kukabiliwa na majukumu mengi, hivyo badala yake atakwenda Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Asha Rose Migiro.
Katika barua ya kumjulisha Rais Kikwete kuhusu uteuzi wake, Mtendaji wa African Achievers Awards, Rex Indaminabo alisema:  “Uongozi wa African Achievers Awards unayo furaha kukujulisha juu ya uteuzi wako wa kupokea  Tuzo katika kundi la Utawala Bora Afrika.”
Mtendaji huyo aliongeza: “Ni kwa furaha na heshima kubwa kuwa wajumbe wa Bodi ya Ushauri na Taasisi ya Uongozi na Menejimenti wanakupongeza kwa mafanikio haya.”
posted Saturday, July 25, 2015 | by- Bakari Kiango, Mwananchi
Powered by Blogger.