Kumekucha Yanga, Azam

Mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe (chini) akishindwa kufunga bao huku beki wa Al Khartoum, Hamza Daoud akimtazama wakati wa mchezo wa mwisho wa Kundi C wa mashindano ya Kombe la Kagame uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jana. Yanga ilishinda 1-0. Picha na Anthony Siame
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Fainali ya Kombe la Kagame imekuja mapema, hicho ndicho unachoweza kusema baada ya wawakilishi wa Tanzania Bara, Yanga na Azam kukutana katika mchezo wa robo fainali itakayopigwa Jumatano kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga imekata tiketi ya kuivaa Azam baada ya kuifunga Al Khartoum 1-0 shurkani kwa bao pekee la Amissi Tambwe ambaye katika mchezo alipoteza nafasi nyingi za kufunga.
Ushindi huo unawafanya mabingwa hao wa Tanzania Bara kufikisha pointi tisa, na kushika nafasi ya pili katika Kundi A akiwa nyuma kwa pointi moja kwa vinara Gor Mahia  (10),
Al Khartoum imeshika nafasi ya tatu ikiwa na pointi saba.
Mchezo kati ya Yanga na Azam utakuwa ni marudio ya fainali ya Kombe la Kagame 2013 iliyochezwa kwenye uwanja huo, ambao Yanga ilibuka na ushindi wa mabao 2-0.
Pia mchezo huo utakuwa ni utangulizi wa mchezo wa Ngao ya Jamii itakayochezwa Agosti 22 baina ya timu hizo.
Katika mchezo wa jana, Yanga ilianza mchezo huo taratibu na dakika ya 3, kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’ alifanya makosa kwa kurudisha mpira vibaya uliomkuta mshambuliaji wa Al Khartoum, Amin Ibrahimu, lakini kabla ya kupiga shuti Mbuyu Twite aliwahi na kutoa mpira huo nje.
Yanga ilitumia dakika 14 kabla ya kufika kwa mara ya kwanza langoni mwa Al Khartoum kwa kutumia shambulizi la kushtukiza kupitia Joseph Zutah aliyepia pasi ndefu kwa Busungu, lakini beki wa Wasudan hao walikuwa makini kukoa hatari hiyo.
Wasudan hao walitawala mchezo kwa kufanya mashambulizi mengi, lakini safu ya ulinzi ya Yanga ilikuwa makini kuwadhibiti wasilete madhara golini kwao.
Tambwe alifunga bao lake la kwanza katika mashindano hayo akiunganisha kwa kichwa kona iliyopigwa na Haruna Niyonzima katika dakika 29, na kuamsha shangwe kwa mashabiki wa Yanga.
Kuingia kwa bao hilo kulifanya Yanga kujiamini na kuanza kushambulia kwa kutumia mipira mirefu na krosi na dakika 34, Tambwe nusura afunge bao la pili baada ya kuunganisha krosi ya Zutah kwa kubinuka tikitaka, lakini mpira wake haukulenga lango.
ADVERTISEMENT
Al Khartoum ilifanya mashabulizi yake kupitia Atif Khalifa, Domenic Abui na Amin Ibrahim, lakini mashuti yao yote yaliishia mikononi mwa Barthez na mengi yalitoka nje na kuifanya Yanga kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0.
Kocha wa Yanga, mwanzoni mwa kipindi cha pili alimtoa Oscar Joshua na kumwingiza Haji Mwinyi katika jitihada zake za kupunguza mashambulizi ya Wasudani.
Niyonzima alipiga shuti lililogonga mwamba na kumkuta Coutinho akiwa yeye na lango, lakini shuti la Mbrazili huyo lilishindwa kulenga lango na kutoka nje katika dakika ya 56, wakati mashabiki wa Yanga wakiwa hawaamini kilichoteka, Tambwe naye akiwa yeye na kipa alishindwa
kuunganisha krosi ya Msuva kwa kupiga shuti juu katika dakika 58.
Licha ya mchezo huo kuwa wa kukamilisha ratiba na kutafuta nafasi ya pili, ulikuwa wa bahati mbaya kwa Al Khaetoum, kwani walipoteza nafasi nyingi za wazi kama ilivyokuwa kwa Yanga.
Kasi ya mchezo ilikuwa juu kwa kila timu kushambulia kwa zamu kadri inavyopata nafasi ya kufanya hivyo na kuufanya mchezo kushindwa kutabirika mshindi hadi kipenga cha mwisho, ingawa Yanga ilikuwa ikiongoza kwa bao hilo tangu dakika ya 30.
Awali, mashabiki wa Gor Mahia baada ya timu yao kushinda 3-1 dhidi ya Djibout Telecom, walikuwa wakiimba kwa kusema ‘tunaitaka Yanga, tunaitaka Yanga’.
Mabingwa hao wa Kenya, Gor Mahia imemaliza kwa kishindo hatua ya makundi kwa ushindi huo mnono, shukrani kwa mabao ya Geogre Odhiambo katika dakika ya 13,  Michael Olunga alipachika bao la pili dakika ya 28 na Enock Agwanda alipachika bao la tatu dakika 79, huku Said
Hassan akifunga bao la kufutia machozi wa Telecom.Akizungumzia mchezo huo, Kocha wa Yanga, Hans van Pluijm alisema wapo tayari kuvaana na Azam kwani kuingia katika mashindano ni kuwa tayari kukutana na mpinzani yoyote.
Yanga: Ally Mustapha, Joseph Zutah, Oscar Joshua/ Haji Mwinyi, Pato Ngonyani, Kelvin Yondani/Nadir Haroub, Mbuyu Twite, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amissi Tambwe, Malimi Busungu na Andrey Coutinho/ Godfrey Mwashiuya.
Al Khartoum: Mohamed Ibrahim. Amin Ibrahim, Hamza Daoud, Saleheldim Mahamoud, Samawal Merghani, Wagdi Awad, Anthony Agay, Domenic Abui, Atif Khalif, Badreldin Eldoon na Ahamed Adam.
Powered by Blogger.