Obama awagusa Wakenya, awataka kuacha ukabila


Rais wa Marekani, Barack Obama (kulia), akiwasalimia wananchi wa Kenya kwenye Ukumbi wa Safaricom Arena baada ya kuwahutubia mjini Nairobi jana. Picha na AFP
ADVERTISEMENT
Nairobi, Kenya. Rais wa Marekani, Barack Obama amezungumzia safari yake ya kwanza aliyoifanya Kenya, mwaka 1988 na kupoteza begi lake baada ya kushuka katika Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA).
Akizungumza na Wakenya katika Uwanja wa Kasarani, jijini Nairobi, Obama alisema anamshukuru dada yake, Auma Obama kwa kumpokea katika safari hiyo miaka kadhaa iliyopita.
Obama alisema anafurahia kufika nchini humo akiwa rais wa kwanza wa Marekani.
Obama alipokwenda Kenya wakati huo, begi lake lilipotea na baada ya kufuatilia aliambiwa kwamba lilisafirishwa hadi Afrika Kusini na ndege aliyokuwa amepanda.
Katika hotuba yake, Obama alimshukuru pia Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta kwa ukarimu wake na mapokezi makubwa aliyoyapata.
Pia  aliwaomba radhi ndugu zake wa Kijiji cha Kogello kwa kutofika huko kwa ajili ya kuwasalimia.
Rais huyo alisema anatambua juhudi zilizofanywa na wazee wakati wa kupigania uhuru akiwamo babu yake ambaye alikuwa ni mmoja wa wapiganaji katika Jeshi la Kings African Riffles (KAR).
“Babu yangu alikuwa Burma akitumikia Waingereza. Baada ya vita alifungwa kwa muda kwa kupinga ukoloni,” alisema Obama.
Rais Obama alisema ameona mabadiliko makubwa nchini humo, ikiwamo kukua kwa uchumi wa Kenya.
Alisema zamani Afrika Kusini ndiyo iliyokuwa na uchumi mkubwa, lakini sasa Kenya inakaribia kuifikia Afrika Kusini kiuchumi.
Rushwa inazuia uchumi Kenya
Rais Obama alisema rushwa imekuwa changamoto kubwa kwa nchi nyingi za Afrika na tatizo hilo limekuwa likisababisha ukiukwaji wa haki za binadamu na kuathiri shughuli za Serikali.
“Urasimu ni kikwazo cha utawala bora na mfumo wa utoaji haki, Serikali haina budi kujenga mazingira mazuri kwa watu wake na kupambana na rushwa,” alisema Rais Obama, huku akishangiliwa na watu waliohudhuria mkutano huo.
Alisema rushwa inarudisha nyuma maendeleo ya uchumi na aliwataka Wakenya kubadilisha mtazamo wao juu ya rushwa ili waweze kukabiliana na tatizo hilo.
Rais Obama alisema licha ya kuahidi kuwapatia kinamama na vijana mabilioni ya fedha, wasi wasi wake mkubwa ni rushwa ambayo imekuwa ikikwamisha ukuaji wa uchumi wa nchi hiyo.
Pia, alizungumzia ugaidi na kuwataka Wakenya kuongeza juhudi za kupambana nao.
ADVERTISEMENT
 Obama ameahidi kushirikiana na Kenya katika kupambana na magaidi likiwamo kundi la Al-Shabaab ambalo limekuwa likiishambulia Kenya na kusababisha mamia ya watu kupoteza maisha.
Kenya, Marekani kudhibiti ugaidi
Katika uwanja huo ambako maelfu ya watu walikusanyika kumsikiliza Rais Obama, alisema amezungumza na Rais Uhuru Kenyatta kuhusu nchi hizo mbili zitakavyopambana na ugaidi.
“Kwa kiasi kikubwa tumepunguza nguvu ya Al Shabaab, lakini haimaanishi kwamba tumefanikiwa kutatua tatizo la ugaidi,” alisema Rais Obama.
Alisema Serikali ya Marekani inafurahia juhudi za Kenya katika kukabiliana na mashambulizi ya kigaidi na kwamba atashirikiana na nchi hiyo katika kudhibiti makundi ya kigaidi nchini humo.
“Ugaidi ni mbaya, sasa tunaomboleza waliouawa Westgate na Garissa na katika maeneo mengine. Kenya ipo njia panda katika kufikia malengo yake,” alisema Rais Obama.
Rais Obama alilazimika kutoa kauli hiyo kutokana na mashambulizi ya kigaidi yaliyotokea katika jengo la Westgate na kusababisha watu 67 kupoteza maisha na wengine 148 kufariki dunia Aprili mwaka huu kwenye Chuo Kikuu Cha Garissa baada ya Al-Shabaab kushambulia chuo hicho.
Mbali na hayo, Obama aliwataka Wakenya kuheshimu haki za binadamu na kuacha vitendo vya udhalilishaji kwa wanawake, huku akionya raia wa nchi hiyo kuacha kuwaozesha wasichana wadogo.
“Mimi ni Mwafrika ninayeishi Marekani, naumia sana ninapoona watu wananyimwa haki zao kutokana na sheria kupindishwa, hili halikubaliki,” alisema.
Katika hatua nyingine; Rais Obama aligusia suala la mapenzi ya jinsia moja, lakini Rais Kenyatta alisema kwamba suala la haki za binadamu katika upande wa mapenzi ya jinsia moja halikubaliki na kwamba, hoja hiyo haina mashiko kwa raia wa nchi hiyo.
Demokrasia na ukabila
Pia, aliwataka Wakenya kuimarisha demokrasia na kutumia fursa mbalimbali kuwawezesha vijana kuinuka kiuchumi.
Pia, aliwaonya Wakenya kuacha tabia ya kubaguana kwa majina yao ya mwisho na kutupilia mbali siasa za ukabila kwa sababu zinaharibu maendeleo ya Taifa hilo.
“Watu hawafai kuhukumiwa kwa sababu ya majina yao ya mwisho au dini.  Tukianza kubaguana kwa misingi ya kikabila na ukiutazama uchumi wa Kenya, mwisho tutaumia,” alisema.
Lakini wakati watu wengi wakifurahia ziara ya Rais Obama, wafanyabiashara wa 44 walikuwa wakilalamika jana kwa kushindwa kufungua biashara zao baada ya kufungwa kwa Barabara ya Thika kutokana ziara hiyo. Obama aliondoka jana kwenda Ethiopia.
Imeandikwa na Peter Elias kwa msaada wa mashirika ya habari.
Powered by Blogger.