Wafanyabiashara walia na Tanesco


Dodoma. Kukosekana kwa umeme kwa wakazi wa mjini hapa kwa muda wa wiki mbili sasa, kumezua maswali hali inayosababisha baadhi ya wafanyabiashara kufunga biashara zao.
Kutokana na tatizo hilo, wakazi hao wametafsiri kuwapo kwa mgawo wa umeme wa saa 12 huku kukiwa hakuna taarifa zozote kutoka ofisi za Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)  Mkoa wa Dodoma.
Mfanyabiashara Emmanuel John anayeuza duka la vifaa vya ofisini katika Mtaa wa Uhindini alisema kuwa, kwa muda wa wiki mbili sasa analazimika kufunga duka kutokana na kukosekana kwa umeme mchana kutwa.
Kibaya alilalamikia tatizo la kukatika kwa umeme bila kupewa taarifa zozote na kusema: “Kama ni bili tumelipa, tunafanya kubahatisha tu kuja kazini kama tutapata umeme au hapana.”
Fransis Nkya mfanyabiashara wa bucha la nyama alisema, wakati mwingine nyama huwa inaharibika kutokana na kukosekana kwa umeme mfululizo hali inayo wasababishia hasara.
Mji wa Dodoma umekuwa ukisikika milio ya majenereta ambayo yanatumika kama mbadala wa Tanesco hali inayodaiwa kuwaumiza wafanyabiashara wengi wanaotegemea umeme huo.
Ofisa Habari wa Tanesco, Innocent Lupenza alipoulizwa kuhusiana na suala hilo alisema kuwa yupo kwenye kikao na kumtaka mwandishi amtumie ujumbe mfupi wa maandishi.
Alipotumiwa ujumbe huo alisema kuwa yupo nje ya mkoa na kumtaka mwandishi amweleze kinachoendelea, alipoelezwa alijibu kuwa siyo kweli.
“Nchi nzima ilikuwa hapo, si ungesikia au ulikuwa unamaanisha vipi?” alihoji Lupenza kwenye ujumbe mfupi wa simu ya mkononi.
 
Posted Friday, July 24, 2015 | by- Rachel Chibwete, Mwananch
Powered by Blogger.